Hamia kwenye habari

JANUARI 16, 2020
UINGEREZA

Familia ya Betheli ya Uingereza Yahamia Katika Makao Mapya Huko Chelmsford

Familia ya Betheli ya Uingereza Yahamia Katika Makao Mapya Huko Chelmsford

Januari 1, 2020, familia ya Betheli ya Uingereza ilianza kuhamia katika majengo mapya ya Betheli yaliyo karibu na Chelmsford, Essex. Inatarajiwa kwamba kufikia mwanzoni mwa Machi 2020, wajitoleaji wote wa wakati wote watakuwa wanaishi na kufanya kazi katika ofisi mpya ya tawi.

Tangu mwaka 1959, ofisi ya tawi ya Uingereza imekuwa huko Mill Hill, London. Kazi ya kuhubiri ilipozidi kuongezeka ndivyo kazi ofisini zilivyozidi kuwa nyingi na hivyo ofisi ilipanuliwa ikawa na majengo kadhaa katika maeneo mbalimbali. Udumishaji mwingi sana ulihitaji kufanywa, na washiriki wa Betheli walikuwa wakilazimika kusafiri sana. Kwa muda fulani, ofisi ya tawi ya Uingereza ilitumiwa pia kama kituo cha uchapishaji, na hata kufikia kuchapisha kiasi cha asilimia kumi ya machapisho ya ulimwenguni pote. Baada ya kutumiwa kwa miaka 92, majengo ya uchapishaji yalifungwa na kuuzwa katika mwezi wa Machi 2018. a

Ndugu na dada waliosaidia katika ujenzi wa ofisi mpya ya tawi wakiwakaribisha Wanabetheli waliohamia Januari 1, 2020

Majengo mapya ya ofisi ya tawi ya Uingereza yamejengwa kwa muda wa miaka mitano. Sasa idara zote za ofisi ya tawi ziko katika eneo moja, na hilo linaongeza ubora wa kazi na pia ni njia bora ya kutumia vizuri michango inayotolewa. Majengo hayo yanatia ndani majengo mawili ya kutayarisha video, ofisi, na majengo sita ya makazi yenye uwezo wa kutumiwa na watu 400. Jengo moja linaweza kutumiwa kwa shughuli mbalimbali kama vile ukumbi wa chakula, na kwa ajili ya matukio mengine.

Kufikia sasa, ofisi ya tawi ya Uingereza inasimamia kazi ya kuhubiri katika maeneo mbalimbali kutia ndani visiwa vya Falkland, Guernsey, Ireland, Isle of Man, Jersey na Malta. Sasa, ofisi ya tawi itashughulikia uzalishaji wa rekodi za kusikiliza, video na machapisho ya kielektroni. Pia, ofisi ya tawi itaendelea kusimamia kazi ya kuhubiri na kufundisha inayofanywa na wahubiri zaidi ya 150,000 katika makutaniko zaidi ya 1,800.

Matembezi ya ofisi mpya za Betheli yamepangwa kuanza Aprili 6, 2020. Wageni wanaweza kutarajia kufurahia maonyesho yanayohusu mambo kama vile historia ya Biblia nchini Uingereza na Ireland na sehemu inayotimizwa na Betheli katika tengenezo la Yehova linaloendelea kukua na kubadilika.

Ndugu Stephen Hardy, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Uingereza, amekuwa akihusika katika mradi huu tangu ulipoanzishwa. Anaeleza hisia za ndugu na dada wengi waliohusika katika mradi huu kwa kusema, “Yehova alichochea roho ya ujitoleaji ya ndugu na dada wengi katika eneo letu na kutoka nchi nyingine ili kusaidia katika mradi huu. Matokeo yamekuwa zaidi ya vile tulivyotazamia, yote haya yakimletea Yehova utukufu.”—Waefeso 3:20.

a Sasa machapisho yote yanayotumiwa katika eneo la ofisi ya tawi ya Uingereza yanachapishwa katika ofisi ya tawi ya Ulaya ya Kati, iliyopo Selters, Ujerumani.

 

Picha ya juu inayoonyesha mazingira yenye kuvutia ya ofisi ya tawi ya Uingereza

Dada akiandaa sehemu ya machapisho kwa ajili ya wageni katika eneo la mapokezi

Ndugu na dada wajitoleaji wakisikiliza katika mkutano wa kujifunza mambo ya msingi uliofanyika katika moja kati ya kumbi mpya

Ndugu na dada wakifurahia chakula cha mchana katika ukumbi wa chakula, sehemu ambayo inaweza kubadilishwa kwa ajili ya kazi mbalimbali

Kibao cha barabarani kilichoandikwa “Barabara ya Ufalme,” kilichowekwa katika mwingilio wa Betheli