Hamia kwenye habari

OKTOBA 21, 2016
UJERUMANI

Mwadhimisho wa Kukombolewa kwa Wafungwa wa Brandenburg Wakazia Hasa Mashahidi wa Yehova

Mwadhimisho wa Kukombolewa kwa Wafungwa wa Brandenburg Wakazia Hasa Mashahidi wa Yehova

SELTERS, Ujerumani—Ukumbusho wa 71 wa Kukombolewa kwa Wafungwa wa Gereza la Brandenburg-Görden uliofanyika Aprili 24, 2016 ulikazia hasa mambo yaliyowapata Mashahidi wa Yehova.

Waziri wa Mambo ya Fedha wa Brandenburg, Daniela Trochowski, akitoa hotuba yake wakati wa mwadhimisho.

Tukio hilo, lililodhaminiwa na Shirika la Brandenburg Memorials Foundation (Stiftung Brandenburgische Gedenkstätten), lilifanyika katika uwanja wa Gereza la Brandenburg an der Havel (linaloonyeshwa kwenye picha hapo juu), lililo kilomita 90 hivi magharibi mwa Berlin. Wageni zaidi ya 200 walihudhuria mwadhimisho huo. Daniela Trochowski, Waziri wa Mambo ya Fedha katika Brandenburg, alitoa hotuba akiwa msemaji aliyealikwa. Alisema hivi: “Hapa, Mashahidi wa Yehova walipewa adhabu ya kifo . . . kwa sababu walikataa kutoa salamu ya ‘Heil Hitler’ kwa msingi wa kidini, kwa sababu walikataa kujihusisha katika hafla za Serikali na mashirika ya Serikali, na kwa sababu walikataa kujihusisha katika utumishi wa kijeshi.”

Sigurd Speidel alikuwa miongoni mwa Mashahidi waliouawa na Wanazi katika Gereza la Brandenburg-Görden.

Wakati wa utawala wa Nazi, mtawala wa Ujerumani aliyeitwa Adolf Hitler, alisema Mashahidi wa Yehova ‘kikundi cha watu kinachostahili kuangamizwa.’ Kati ya watu 2,000 waliouawa katika Gereza la Brandenburg-Görden (kama lilivyoitwa wakati wa utawala wa Nazi) kati ya mwaka wa 1940 na 1945, 127 walikuwa Mashahidi wa Yehova, idadi kubwa zaidi ya watu wa kikundi kimoja kuuawa katika mahali hapo.

Katika programu hiyo ya mwadhimisho iliyofanyika Aprili 24, Jochen Feßenbecker, mwakilishi wa ofisi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani, alimhoji Werner Speidel. Bw. Speidel alieleza kwamba ndugu yake mkubwa Sigurd alikuwa miongoni mwa Mashahidi waliouawa katika Gereza la Brandenburg-Görden. Januari 27, 1943, miezi mitatu hivi baada ya kuhukumiwa na mahakama ya kijeshi, Sigurd aliyekuwa na umri miaka 19 alikatwa kichwa. Wakati wa mahojiano hayo, Bw. Feßenbecker alisoma barua ambayo Sigurd aliwaandikia saa chache tu kabla ya kuuawa. Bw. Speidel alieleza maoni ya familia yao kuhusu maneno ya mwisho ya Sigurd: “Kusoma barua hiyo hakukututia woga. Badala yake, tulijivunia kwamba Sigurd alidumisha imani yake hadi kifo.”

Barua ambayo Sigurd Speidel aliiandikia familia yake ili kuwaaga. Nukuu iliyoonyeshwa hapo juu inasema: “Nimevumilia mambo yote na nimebaki imara, kama ukuta.”

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma, 1-718-560-5000

Ujerumani: Wolfram Slupina, 49-6483-41-3110