Hamia kwenye habari

Dennis Christensen akipokewa na baba na dada yake katika uwanja wa ndege wa Copenhagen Kastrup, Mei 25, 2022

MEI 25, 2022
URUSI

Dennis Christensen Aachiliwa Huru na Kurudishwa Denmark

Dennis Christensen Aachiliwa Huru na Kurudishwa Denmark

Irina Christensen akimsubiri Dennis aachiliwe nje ya Gereza Na. 3 lililo Lgov, nchini Urusi, Mei 24, 2022

Mei 25, 2022, Dennis Christensen aliwasili nchini Denmark. Alikuwa ameachiliwa kutoka gerezani nchini Urusi siku iliyotangulia, na papo hapo akasafirishwa ili aondoke nchini. Kwa miaka mitano ametumikia kifungo chake katika magereza tofauti.

Dennis anasema hivi: “Nina furaha sana kuachiliwa kutoka gerezani na kuungana tena na mke wangu mpendwa, Irina. Kitia moyo na msaada niliopata kutoka kwa ndugu na dada ulimwenguni pote ni zawadi kutoka kwa Yehova. Ninaendelea kusali kwa ajili ya ndugu na dada zangu jasiri wanaoendelea kuteswa na kufungwa kwa sababu ya imani yao.”

Dennis na Irina wakiwa kwenye uwanja wa ndege wa Moscow Domodedovo

Dennis na Irina wanategemezwa kiroho na kimwili na watu wa familia na marafiki. Walisema hivi: “Tunatazamia kwa hamu kumwabudu Yehova kwa uhuru pamoja na ndugu na dada zetu nchini Denmark.”

Mei 25, 2017, Dennis alikamatwa na kuwekwa mahabusu baada ya maofisa waliofunika nyuso zao na waliokuwa wamebeba silaha kuvamia mkutano wa kutaniko aliokuwa amehudhuria huko Oryol. Baadaye alihukumiwa kwamba alipanga utendaji wa shirika la kidini ambalo mwezi mmoja kabla ya hapo, lilikuwa limetangazwa kuwa lenye msimamo mkali na kupigwa marufuku na Mahakama Kuu ya Urusi.

Kwa mara kadhaa, wenye mamlaka nchini Urusi wamesema kwamba uamuzi wao wa mwaka 2017 wa kupiga marufuku ulihusu tu mashirika ya Mashahidi wa Yehova na hauingilii haki ya Shahidi mmoja-mmoja ya kuabudu. Hata hivyo, Dennis alikuwa Shahidi wa kwanza tu katika kampeni kubwa ya kuwakamata na kuwafunga gerezani Mashahidi wa Yehova katika eneo lote la Urusi na Crimea.

Dennis na Irina, pamoja na ndugu wawili Waturuki waliokuja kuwaona kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Istanbul kabla ndege haijaendelea na safari ya kwenda Denmark

Kufikia sasa, ndugu na dada zetu 91 bado wapo gerezani. Tunasali kwamba Yehova aendelee kuwategemeza ndugu zetu washikamanifu na kuwatendea “kwa njia ya pekee.”​—Zaburi 4:3.