Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Urafiki wa Kimapenzi​—Sehemu ya 3: Je, Tuvunje Uhusiano Wetu?

Urafiki wa Kimapenzi​—Sehemu ya 3: Je, Tuvunje Uhusiano Wetu?

 Urafiki wenu umeendelea kwa muda, lakini sasa wewe umeanza kuwa na mashaka. Je, uendeleze uhusiano huo au uuvunje? Makala hii imekusudiwa kukusaidia kufanya uamuzi huo.

Katika makala hii

 Kukabiliana na mashaka

 Baada ya kuwa na urafiki wa kimapenzi kwa muda, mvulana na msichana wanaweza kugundua kwamba hawapatani kama walivyofikiri mwanzoni. Kwa mfano:

  •   Mmoja anafurahia kwenda ufuoni; mwenzake anafurahia zaidi kwenda matembezi.

  •   Mmoja anapenda kuzungumza sana na kuchangamana na watu; mwenzake ni mnyamavu na hapendi sana kuchangamana na watu.

  •   Mmoja hasemi kweli pindi zote; mwenzake ni mnyoofu nyakati zote.

 Ona kwamba hali zote hizo ni tofauti. Hali ya kwanza inaonyesha wana mapendezi tofauti; hali ya pili inaonyesha wana sifa tofauti; hali ya tatu inaonyesha wana viwango tofauti.

 Jambo la kufikiria: Ni hali gani kati ya hizo tatu ambayo ingekuwa vigumu zaidi kwako kukabiliana nayo iwapo ungefunga ndoa na mtu huyo? Ni hali gani ambayo mnaweza kuishi nayo?

 Mume na mke wanaweza kutofautiana kuhusu mapendezi au sifa, na bado wawe na ndoa yenye furaha. Kwa sababu kwa kweli, kupatana hakumaanishi kwamba lazima mfanane. Katika visa fulani, mume na mke hujifunza kupendezwa na mambo yanayompendeza mwenzi wake. Pia wao hujifunza jinsi sifa za mwenzi wao zinavyoweza kuwanufaisha. a

 Kwa upande mwingine, ni muhimu kwamba mtu unayefunga ndoa naye awe na viwango kama vyako—kuhusu mambo ya kiroho, ya maadili, na kuhusu tofauti kati ya yaliyo sawa na kosa. Ikiwa ana viwango tofauti, hiyo ni ishara kwamba unapaswa kukomesha uhusiano wenu.

 Kwa mfano, fikiria ikiwa hampatani kidini. Kitabu Fighting for Your Marriage kinasema hivi: “Utafiti unaonyesha kwamba ni rahisi zaidi kwa wenzi wa ndoa walio na imani tofauti kutalikiana.”

 Kanuni ya Biblia: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.”​—2 Wakorintho 6:14.

 Kufanya uamuzi

 Biblia inasema kwamba wale wanaofunga ndoa “watakabiliana na matatizo mengi katika maisha haya.” (1 Wakorintho 7:28, Neno: Biblia Takatifu) Usishangae ikiwa utakabiliana na matatizo hayo sasa, wakati wa urafiki.

 Kutoelewana kwa kiwango kidogo hakumaanishi kwamba uhusiano wenu hauwezi kufanikiwa. Swali ni, je, mnaweza kutatua kutoelewana huko kwa amani? Bila shaka nyote wawili mtahitaji ustadi huo mtakapofunga ndoa.

 Kanuni ya Biblia: “Mtendeane kwa fadhili, huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.”​—Waefeso 4:32.

 Kwa upande mwingine, kutoelewana mara nyingi au kwa kiwango kikubwa kunaweza kuonyesha kwamba ninyi wawili hampatani. Ikiwa ndivyo ilivyo, ni afadhali kutambua hilo sasa badala ya kugundua jambo hilo baada ya kufunga ndoa!

Kutoelewana mara nyingi au kwa kiwango kikubwa kunaweza kuonyesha kwamba ninyi wawili hampatani

 Jambo kuu: Ikiwa una mashaka makubwa kumhusu mtu uliye na uhusiano naye au hata kuhusu ikiwa wewe uko tayari kufunga ndoa, usipuuze mashaka hayo!

 Kanuni ya Biblia: “Mtu mwerevu huona hatari na kujificha, lakini wajinga husonga mbele na kupata madhara.”​—Methali 22:3.

 Ukiamua kuvunja uhusiano

 Kuvunja uhusiano kunaweza kuumiza kihisia. Hata hivyo, ikiwa mmoja kati yenu au nyote wawili mna mashaka mazito na yanayoendelea kuhusu uhusiano wenu, huenda ikafaa kuukomesha.

 Unaweza kuukomeshaje? Itafaa sana usifanye hivyo kupitia ujumbe wa simu au barua-pepe, isipokuwa kuwe na sababu nzuri sana ya kutumia njia hizo. Badala yake, tafuteni wakati na mahali panapofaa kuzungumzia jambo hilo muhimu pamoja.

 Kanuni ya Biblia: “Kila mtu amwambie mwenzake ukweli.”​—Zekaria 8:16.

 Je, inamaanisha kwamba wewe ni bure ikiwa uhusiano wenu unavunjika? La hasha. Kumbuka kwamba urafiki wa kimapenzi unapaswa kukusaidia kufanya uamuzi—ikiwa utafunga ndoa na mwenzako au la. Hata ikiwa uhusiano wenu unavunjika, bado unaweza kujifunza masomo muhimu kutokana na jambo hilo.

 Jiulize: ‘Nimejifunza nini kujihusu kutokana na uhusiano huu? Je, umefunua maeneo ambayo ninahitaji kufanyia kazi kabla ya kufunga ndoa? Wakati ujao nitakapoanzisha urafiki wa kimapenzi, nitafanya mambo gani kwa njia tofauti?’

a Ili uelewe vizuri zaidi jinsi changamoto hizi zinavyoweza kuathiri mume na mke, ona makala yenye kichwa “Msaada kwa Ajili ya Familia—Mapendezi Yanapotofautiana” na “Msaada kwa Ajili ya Familia—Maoni Yanayofaa Kuhusu Sifa Zinazokukasirisha.”