Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kazi ya Kujitolea Yenye Faida ya Kudumu

Kazi ya Kujitolea Yenye Faida ya Kudumu

Kazi ya Kujitolea Yenye Faida ya Kudumu

YESU KRISTO alikuwa akitenda mema na kusaidia wenye uhitaji kwa ukawaida. Kwa mfano, alilisha wenye njaa na kuponya wagonjwa. (Mathayo 14:14-21) Lakini, alitanguliza kazi gani? Tutapata jibu tukichunguza tukio moja lililotukia mapema katika huduma ya Yesu. Tukio hilo linasimuliwa katika sura ya kwanza ya Injili ya Marko.

Yesu alipokuwa Kapernaumu, karibu na Bahari ya Galilaya, alipelekwa kwenye nyumba ya Simoni, au Petro. “Mama-mkwe wa Simoni alikuwa amelala chini akiwa mgonjwa wa homa,” na Yesu akamponya. (Marko 1:29-31) Baadaye, watu wengi kutia ndani wale “waliokuwa na magonjwa ya namna mbalimbali” walianza kukusanyika mlangoni pa nyumba ya Petro, na Yesu akawaponya pia. (Marko 1:32-34) Kisha usiku ukafika na wote wakalala.

Asubuhi iliyofuata “kulipokuwa bado kuna giza,” Yesu aliamka polepole na kutoka katika nyumba, “akaenda mahali pa upweke, na huko akaanza kusali.” Punde si punde, wanafunzi wakaamka pia, wakachungulia nje, na kuona watu wengi sana waliongoja mlangoni. Lakini wafanye nini? Yesu hakuwapo! Mara moja Petro na wenzake walikwenda kumtafuta Yesu, wakampata na kumwambia hivi: “Wote wanakutafuta wewe.” (Marko 1:35-37; Luka 4:42) Ni kana kwamba walimwambia Yesu hivi: ‘Unafanya nini hapa? Jana usiku ulifanikiwa sana kuponya wagonjwa. Leo una fursa nyingine ya kufanya vivyo hivyo!’

Lakini zingatia maneno ambayo Yesu aliwaambia: “Acheni twende mahali pengine, katika miji ya vijiji iliyo karibu, ili nipate kuhubiri huko pia.” Jibu hilo ni la maana. Yesu hakurudi kwenye nyumba ya Petro ili aponye wengine. Alieleza sababu hakufanya hivyo aliposema hivi: “Kwa sababu kwa ajili ya hili [yaani, kuhubiri] nilitumwa.” (Marko 1:38, 39; Luka 4:43) Yesu alimaanisha nini? Kufanya matendo mema kulikuwa muhimu kwake, lakini kuhubiri na kufundisha neno la Mungu kulikuwa kazi kuu ya Yesu.—Marko 1:14.

Kwa kuwa Biblia yasihi Wakristo ‘wafuate hatua za Yesu kwa ukaribu,’ Wakristo wa kweli wana mwongozo ulio wazi inapohusu kazi ya kujitolea ambayo inapasa kutangulizwa. (1 Petro 2:21) Kama Yesu, wao wanasaidia watu wenye uhitaji—jinsi ilivyosimuliwa hapo awali. Vilevile kama Yesu, wao wanatanguliza kazi ya kufundisha ujumbe wa Biblia juu ya habari njema za Ufalme wa Mungu. * (Mathayo 5:14-16; 24:14; 28:19, 20) Lakini, kwa nini tutangulize kazi ya kufundisha ujumbe wa Biblia mbele ya kazi nyingine muhimu za kujitolea?

Kinachofanya Elimu ya Biblia Iwe Yenye Faida

Mithali moja ya Asia yajibu kwa kusema hivi: “Ukipanga kwa mwaka mmoja, panda mbegu. Ukipanga kwa miaka kumi, panda miti. Ukipanga kwa miaka mia moja, elimisha watu.” Naam, ili kuandaa masuluhisho yenye faida ya kudumu, elimu ni muhimu sana, kwa kuwa inakuza uwezo wa mtu wa kufanya maamuzi yatakayoboresha maisha yake. Kwa hiyo, wafanyakazi wa kujitolea zaidi ya milioni sita hutumia wakati, nguvu, na mali zao kuwafundisha watu Biblia bila malipo. Baadhi yao wanafanya kazi hiyo mara kwa mara na wengine wanaifanya wakati wote. Kazi hiyo ambayo Mashahidi wa Yehova wamefanya kwa miaka mingi inanufaisha jumuiya mbalimbali kotekote duniani. Vipi?

Watu wanaposaidiwa kuelewa na kufuata ushauri wa Biblia, wanaelewa vizuri zaidi jinsi ya kukabiliana na matatizo ya maisha. Wanapata nguvu za maadili zinazohitajika kushinda mazoea mabaya. Nelson, kijana mmoja huko Brazili, anaonyesha faida nyingine ya elimu ya Biblia anaposema hivi: “Tangu nianze kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, nimekuwa na furaha kwa sababu sasa nina kusudi maishani mwangu.” (Mhubiri 12:13) Mamia ya maelfu ya watu—vijana kwa wazee—ambao wameanza kujifunza Neno la Mungu hivi majuzi wana maoni kama ya Nelson. Mbali na kuwasaidia wanafunzi kupata kusudi linaloridhisha maishani, ujumbe juu ya Ufalme wa Mungu huwapa tumaini la wakati ujao lenye kutia moyo—tumaini linalofanya maisha yawe yenye maana, haidhuru hali iwe ngumu kadiri gani. (1 Timotheo 4:8)—Soma sanduku “Faida Ambazo Ufalme wa Mungu Utaleta.”

Wanapofundisha Biblia, Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi ya kujitolea yenye faida za kudumu. Zitadumu kwa muda gani? Neno la Mungu lasema hivi: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Ebu wazia, unaweza kushiriki kazi inayoleta faida za milele—hiyo ndiyo kazi ya kujitolea yenye faida kwelikweli! Je, ungependa kujua zaidi kuhusu kazi hiyo? Ikiwa ndivyo, ongea na Mashahidi wa Yehova wanaoishi katika eneo lenu. Hutajuta kamwe ukiamua kukubali mwaliko huu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Mashahidi wa Yehova huiona kazi yao ya kuhubiri kuwa ya lazima kwa Wakristo wa kweli—kama alivyofanya mtume Paulo. Yeye alisema hivi: “Ikiwa, sasa, ninatangaza habari njema, hiyo si sababu ya mimi kujisifu, kwa maana nimewekewa sharti.” (1 Wakorintho 9:16) Hata hivyo, kazi yao ya kuhubiri ni kazi ya kujitolea kwa sababu wamechagua kwa hiari kuwa wanafunzi wa Kristo, wakijua kabisa madaraka yanayoambatana na pendeleo hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Ukipanga kwa mwaka mmoja, panda mbegu. Ukipanga kwa miaka kumi, panda miti. Ukipanga kwa miaka mia moja, elimisha watu”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Anawapa Msaada na Tumaini

Nadine, mwuguzi Mfaransa mwenye umri wa miaka 43 aliye stadi kutibu magonjwa ya nchi za joto, ni mmojawapo wa wale ambao walikuwa wamejitolea kufanya kazi huko Afrika ya Kati. Alipohojiwa hivi majuzi alisema hivi: ‘Watu huniuliza ni kwa nini ninafanya kazi hii. Ninamwamini Mungu, ninapenda watu, na ninataka kujitolea. Na kwa sababu mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova ninasukumwa kutibu wagonjwa na kuwapa wanaoteseka tumaini.’ Kazi ya kujitolea ya Nadine huku Afrika yatia ndani kutoa misaada na kushiriki kazi ya kufundisha Biblia pamoja na Mashahidi wenyeji.

[Picha]

Nadine akiwa Afrika

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Faida Ambazo Ufalme wa Mungu Utaleta

Tafadhali soma maandiko haya katika Biblia yako mwenyewe, ukaone jinsi Mungu anavyoahidi kutimiza mahitaji yafuatayo ya wanadamu:

Afya “Atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”Ufunuo 21:4; Isaya 33:24; 35:5, 6.

Elimu “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”Isaya 11:9; Habakuki 2:14.

Kazi “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine . . . Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”Isaya 65:21-23.

Chakula “Nchi imetoa mazao yake MUNGU, Mungu wetu, ametubariki.”Zaburi 67:6; 72:16; Isaya 25:6.

Hali ya Jamii “BWANA amelivunja gongo la wabaya . . . Dunia yote inastarehe na kutulia.”Isaya 14:5, 7.

Haki “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu.”Isaya 11:3-5; 32:1, 2.