Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ponografia Ni Raha Isiyodhuru?

Je, Ponografia Ni Raha Isiyodhuru?

Maoni ya Biblia

Je, Ponografia Ni Raha Isiyodhuru?

MNAMO mwaka wa 1850 na kuendelea, wachimbuzi fulani wa vitu vya kale walipoanza kuchimbua magofu ya Pompeii, wao walishtushwa na vitu walivyopata. Michoro na sanamu nyingi zilizoonyesha wazi mambo ya kingono zilitapakaa kotekote miongoni mwa michoro mingine maridadi. Wenye mamlaka walishangazwa sana na michoro hiyo na sanamu hizo na kuziweka katika vyumba vya siri vya kuhifadhi vitu vya kale. Ili kuiorodhesha michoro hiyo na sanamu hizo chafu, wenye mamlaka hao walibuni neno “ponografia”—linalotokana na maneno ya Kigiriki pornē na graphos yanayomaanisha “kuandika kuhusu makahaba.” Leo ponografia inafafanuliwa kuwa kuonyesha tabia za kimahaba katika vitabu, picha, sanamu, sinema, na kadhalika, kwa kusudi la kuamsha nyege.”

Leo, ponografia imeenea sana na kukubaliwa na watu wengi katika jamii ya kisasa. Wakati mmoja ponografia ilipatikana katika sinema fulani tu za kimahaba na katika mitaa ya makahaba, lakini sasa imeenea kwa wingi katika jamii nyingi. Nchini Marekani pekee, ponografia ni biashara inayochuma zaidi ya dola bilioni kumi kila mwaka!

Watu wanaotetea ponografia wanadai kwamba hiyo inasisimua ndoa zisizo na furaha. Mwandishi mmoja anasema hivi: “Ponografia huleta mawazo mazuri. Hiyo hufundisha jinsi ya kufurahia ngono.” Wengine husema kwamba ponografia huwasaidia watu wazungumze waziwazi mambo ya kingono. “Ponografia huwasaidia wanawake,” anadai Wendy McElroy.

Lakini wengine hawakubaliani na maoni hayo. Inasemekana kwamba ponografia inaleta matokeo na mitazamo mibaya. Wengine wanaona kwamba ponografia inachangia sana ubakaji na namna nyingine za jeuri dhidi ya wanawake na watoto. Ted Bundy, ambaye ni maarufu kwa kuua watu wengi, anakiri kwamba “alipenda sana kutazama ponografia yenye jeuri.” Yeye anasema hivi: ‘Mtu hatambui jambo hilo haraka wala halitambui kuwa tatizo zito. Lakini yeye huanza kutamani sana mambo ya kingono yanayohusisha jeuri. Sipati maneno ya kuelezea jinsi hali hiyo inavyositawi hatua kwa hatua. Hamu hiyo haiji baada ya muda mfupi.’

Kwa sababu ya maoni yanayotofautiana na kuenea kwa ponografia leo, huenda ukajiuliza, ‘Biblia inatoa ushauri gani kuhusu jambo hilo?’

Biblia Inasema Waziwazi Kuhusu Ngono

Biblia inazungumzia mambo ya kingono waziwazi bila kuficha. (Kumbukumbu la Torati 24:5; 1 Wakorintho 7:3, 4) Solomoni alishauri hivi: “Umfurahie mke wa ujana wako, . . . maziwa yake yakutoshe sikuzote.” (Mithali 5:18, 19) Mashauri ya wazi kuhusu mahusiano ya kingono, kutia ndani mipaka inayopasa kuwekwa watu wanapofurahia mahusiano hayo yametolewa. Ngono nje ya ndoa na vilevile namna nyingine za ngono zilizopotoka zimekatazwa.—Mambo ya Walawi 18:22, 23; 1 Wakorintho 6:9; Wagalatia 5:19.

Hata viwango hivyo vinapofuatwa, watu wanapaswa kuwa na kiasi na kuonyeshana heshima. Mtume Paulo aliandika hivi: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila kutiwa unajisi.” (Waebrania 13:4) Shauri hilo ni kinyume kabisa na nia na ujumbe wa ponografia.

Ponografia Hupotoa Ngono

Badala ya kuonyesha ngono kuwa njia nzuri ya kuonyeshana upendo kati ya watu wawili waliooana kwa heshima, ponografia hushusha hadhi ya tendo la ngono na kulipotoa. Ngono isiyo na heshima na iliyopotoka huonyeshwa kuwa yenye kufurahisha na ya kutamanika. Ponografia inakazia kujiridhisha kibinafsi bila kumfikiria yule mtu mwingine.

Wanawake, wanaume, na watoto wanaonwa kuwa tu vyombo vya kutosheleza hamu ya ngono. Ripoti moja inasema kwamba “urembo unapimwa kwa kuangalia jinsi ambavyo mwili umeumbika, na hilo hutokeza matazamio yasiyoweza kutimizwa.” Ripoti nyingine inamalizia kusema kwamba “kuwafanya wanawake waonwe kuwa si kitu, wanaotamani ngono nyakati zote, na kutumiwa vibaya na wanaume, wenye kuvua mavazi na kufunua uchi wao ili kupata pesa na kujifurahisha, si kuwatendea kwa usawa, heshima na kwa ubinadamu.”

Kinyume cha hilo, Paulo aliandika kwamba upendo “haujiendeshi bila adabu, hautafuti masilahi yao wenyewe.” (1 Wakorintho 13:5) Biblia inawahimiza waume ‘kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe’ na ‘kuwapa heshima,’ si kuwaona wanawake kama tu vyombo vya kujifurahishia kingono. (Waefeso 5:28; 1 Petro 3:7) Je, mtu yeyote, awe mwanamke au mwanamume, ambaye kwa kawaida hutazama picha zinazoonyesha waziwazi ngono za watu wengine, kwa kweli anajiendesha kwa adabu? Na je, mtu huyo anaonyesha staha na heshima? Ponografia huendeleza tamaa yenye ubinafsi ya kujitanguliza, badala ya upendo.

Bado kuna jambo jingine. Kama ilivyo kawaida na aina nyingine za tamaa zisizofaa, jambo ambalo wakati mmoja linaamsha mtu kingono huanza kukosa kusisimua. Mwandishi mmoja anasema hivi: “Hatimaye, wale [wanaotazama ponografia] huhitaji picha chafu na zilizopotoka zaidi . . . Wanaweza kuwashurutisha wenzi wao wafanye ngono zinazopotoka zaidi . . . , huku wakizidi kushindwa kuonyesha upendo wa kweli.” Je, kweli hiyo ni raha isiyodhuru? Hata hivyo kuna sababu nyingine ya kutufanya tuepuke ponografia.

Biblia na Tamaa

Ingawa watu wengi hawaoni kosa lolote au hatari ya kutazama ponografia, Biblia haiungi mkono maoni hayo. Inasema waziwazi kwamba matendo yetu yanaongozwa sana na mambo tunayojaza akilini mwetu. Mwanafunzi Mkristo Yakobo anaonyesha kwamba “kila mmoja hujaribiwa kwa kuvutwa na kutongozwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetungika mimba, huzaa dhambi.” (Yakobo 1:14, 15) Yesu alisema: “Kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:28.

Kama vile Yakobo na Yesu wanavyoonyesha, wanadamu husukumwa na tamaa iliyo ndani yao. Hatimaye, tamaa hiyo inapositawishwa, inaweza kuwa na nguvu sana. Ni vigumu sana kuuzuia msukumo huo na baada ya muda unaweza kumfanya mtu atende mambo anayotazama. Kwa hiyo, yale tunayoweka akilini yana nguvu nyingi na yanaathiri matendo yetu hatimaye.

Kufikiria mambo ya kingono isivyofaa kunaweza kuathiri ibada yetu kwa Mungu. Hiyo ndiyo sababu Paulo aliandika hivi: “Kwa hiyo, fisheni viungo vya mwili wenu . . . kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kuumiza, na tamaa, ambako ni ibada ya sanamu.”—Wakolosai 3:5.

Katika andiko hilo Paulo alionyesha kwamba hamu ya ngono inahusiana na tamaa, ambayo ni kutaka sana kuvipata vitu usivyokuwa navyo. * Tamaa ni namna ya ibada ya sanamu. Kwa nini? Kwa sababu yule anayetamani huweka kitu anachotamani mbele ya mambo mengine yote, hata Mungu. Ponografia huamsha tamaa kwa ajili ya kitu ambacho mtu hana. “Unatamani maisha ya kingono ya mtu. . . . Huwezi kuwa na jambo jingine akilini ila tu kutamani kile ambacho huna. . . . Kile tunachotamani, tunakiabudu,” akasema mwandishi mmoja wa mambo ya kidini.

Ponografia Hufisidi

Biblia inatuhimiza hivi: “Mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yaliyo ya kusemwa vema, wema wa adili wowote ulioko . . . endeleeni kufikiria mambo haya.” (Wafilipi 4:8) Mtu anayetazama ponografia na kuijaza akilini mwake analikataa himizo la Paulo. Ponografia haina kiasi kwa sababu inafunulia watu wote mambo ya siri na ya faragha. Ni tendo la kipumbavu kwa sababu linamshusha mhusika na kushusha heshima. Hilo si tendo la upendo kwa kuwa halichangii hali ya kuwajali wengine. Hilo hukazia tu tamaa ya mtu binafsi.

Kwa kuonyesha matendo yasiyo ya kiadili na yaliyopotoka kingono, ponografia hudhoofisha na kuharibu jitihada ya Mkristo ya ‘kuchukia mabaya.’ (Amosi 5:15) Ponografia huwatia watu moyo kufanya dhambi na ni kinyume kabisa cha himizo la Paulo kwa Waefeso la kuacha ‘uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa hata visitajwe hata miongoni mwao, kama vile ifaavyo watu watakatifu; wala mwenendo wa aibu wala kufanya mzaha wenye aibu, mambo yasiyofaa.’—Waefeso 5:3, 4.

Kwa kweli ponografia haikosi kuleta madhara. Hiyo hutumikisha na kufisidi. Inaweza kuharibu mahusiano mazuri, na kupotosha njia ya kiasili ya kuonyesha ukaribu wa kingono kuwa uraibu wa kutazama picha za kiponografia. Hiyo huharibu akili na hali ya kiroho ya mraibu. Hiyo hukuza ubinafsi, pupa na kumfanya mtu kuwaona wengine kama vyombo tu vya kutosheleza tamaa zao. Hiyo huharibu jitihada ya mtu ya kufanya mema na kuwa na dhamiri safi. Jambo baya hata zaidi, ponografia inaweza kuathiri vibaya au hata kuharibu kabisa uhusiano wa mtu wa kiroho pamoja na Mungu. (Waefeso 4:17-19) Kwa kweli, ponografia ni janga linalopasa kuepukwa.—Mithali 4:14, 15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Hapa Paulo hakuwa akizungumza kuhusu hamu ya kawaida ya ngono—ile tamaa ambayo mtu huwa nayo ya kutaka kufanya ngono na mwenzi wake wa ndoa.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ponografia hupotosha maoni yetu kuhusu watu wa jinsia tofauti