Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Epuka Mtego wa Kucheza Kamari

Epuka Mtego wa Kucheza Kamari

Epuka Mtego wa Kucheza Kamari

“Kucheza kamari hakukuathiri afya yangu, na sikuzote niliamua kimbele kiasi cha fedha ambacho nilitaka kutumia katika mchezo. Lakini kila nilipocheza kamari ya bahati nasibu, nilichagua nambari ambazo niliamini zilikuwa za bahati njema.”—Linda.

WACHEZAJI wengi wa kamari huamini kwamba watabahatika wakichagua nambari fulani au wakitumia hirizi mbalimbali. Huenda wasione desturi hizo za ushirikina kuwa za maana, lakini, bado wanasisitiza kuzifuata.

Wachezaji wengine wa kamari hata humwomba Mungu awasaidie kushinda mchezo waliochagua. Hata hivyo, katika Biblia, Mungu anawashutumu wale wanaosema kwamba wanamwabudu lakini ‘wanaandika meza kwa ajili ya [“mungu wa,” NW] Bahati.’ (Isaya 65:11) Ndiyo, Mungu huchukia mazoea yanayowatia watu moyo waamini ushirikina na bahati. Michezo ya kamari inawafanya watu wategemee bahati bila kutumia akili.

Pia, kamari huwachochea watu moja kwa moja wapende fedha. Watu wengi leo hawajali mambo ya kiroho, kwa hiyo, fedha imekuwa mungu wao na kucheza kamari ndiyo njia ya kuiabudu. Siku hizi watu huenda kwenye nyumba za fahari za kuchezea kamari badala ya kwenda kanisani, na humo wao hufundishwa kwamba pupa ni sifa nzuri. Watafiti wamegundua ya kwamba watu wengi hucheza kamari ili washinde “kiasi kikubwa sana cha fedha,” wala si kwa sababu ya tafrija au raha. Hata hivyo, Biblia inaonya hivi: “Kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:10.

Biblia inasema hivi waziwazi katika 1 Wakorintho 6:9, 10: “Msiongozwe vibaya. Wala . . . waabudu-sanamu . . . wala watu wenye pupa . . . hawatarithi ufalme wa Mungu.” Mbali na kuwa ugonjwa unaodhoofisha jamii, pupa ni ugonjwa wa kiroho wa kufisha, lakini huo ni ugonjwa unaoweza kutibiwa.

Walipata Nguvu ya Kufanya Mabadiliko

Kazushige, aliyetajwa katika makala ya kwanza, anasema hivi: “Nilijaribu mara nyingi kuacha kucheza kamari. Nilitambua kwamba kucheza kamari kwenye uwanja wa mbio za farasi kuliharibu familia yangu. Kila wakati nilipoteza fedha zote nilizoshinda. Hata nilipoteza fedha ambazo mke wangu alikuwa ameweka akibani alipokuwa akitarajia kujifungua mwana wetu wa pili, na hatimaye nilianza kutumia fedha za kampuni. Sikuweza kujiheshimu tena. Mke wangu alilia na kuniomba mara nyingi niache kucheza kamari, lakini sikuweza kuacha.”

Kisha Kazushige akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Nilipoendelea kusoma Biblia nilisadikishwa kwamba kuna Mungu na kwamba ningefaidika iwapo ningemsikiliza. Niliazimia kwamba ningeacha kucheza kamari kwa msaada wa Mungu. Jambo la kushangaza ni kwamba mbali na kuacha kucheza kamari, sasa nachukia sana zoea hilo. Mimi huhuzunika sana ninapokumbuka jinsi familia yangu ilivyoteseka kwa sababu ya zoea langu la kucheza kamari. Ninamshukuru sana Yehova Mungu kwa kunisaidia kuacha kucheza kamari na kwa kunisaidia kuishi maisha yenye kusudi.”—Waebrania 4:12.

John, aliyetajwa katika makala ya kwanza, alianza pia kujifunza Biblia. Anasema hivi: “Funzo langu la Biblia lilinisaidia kuchunguza maisha yangu. Kwa mara ya kwanza, niliona waziwazi jinsi zoea langu la kucheza kamari lilivyonidhuru mimi na familia yangu. Nilielewa kwamba kamari huendeleza ubinafsi na pupa, sifa ambazo humchukiza Yehova. Nilipoendelea kujifunza, upendo wangu kwa Yehova ulinipa nguvu ya kuacha kucheza kamari. Nilianza kucheza kamari kwa sababu nilitaka kupata maisha bora. Sasa, kwa sababu nimeacha kucheza kamari na ninamtumikia Yehova kwa furaha, matazamio yangu yametimizwa.”

Mke wa John, Linda, aliazimia pia kuacha kucheza kamari. Anasema hivi: “Haikuwa rahisi. Lakini mimi na mume wangu tulipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, nilianza kutanguliza mambo ya maana zaidi maishani. Nilianza kupenda mambo ambayo Mungu hupenda, na pia kuchukia mambo ambayo anachukia, kutia ndani aina zote za pupa. Mbali na kuwa na maisha yenye kusudi, nina pesa nyingi zaidi mkobani.”—Zaburi 97:10.

Ukisitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu utapata nguvu na hekima unayohitaji ili kuepuka mtego wa kucheza kamari. Ukifanya hivyo utaboresha hali yako ya kiuchumi, ya moyoni, na ya kiroho. Kisha utafurahia kujionea ukweli wa maneno ya Mithali 10:22: “Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Mbali na kuwa ugonjwa unaodhoofisha jamii, pupa ni ugonjwa wa kiroho wa kufisha

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Kucheza Kamari na Ushirikina

Katika ripoti moja iliyotumwa kwa Tume ya Kitaifa Inayochunguza Athari za Kamari, watafiti kwenye Chuo Kikuu cha Duke walionyesha jinsi matangazo ya michezo ya kamari yanavyowatia watu moyo kuamini ushirikina. Ripoti hiyo inasema hivi: “Matangazo mengi [ya mchezo wa bahati nasibu] huchochea moja kwa moja tamaa ya mali . . . Hata hivyo, hayo hayachochei tamaa ya kupata mali kwa kufanya kazi kwa bidii, bali huwatia watu moyo kutegemea majini na ushirikina, kwa kuamini matarajio, ndoto, na ushirikina. Na kila msimamizi wa mchezo wa bahati nasibu anajua kwamba wengi wa wateja wao wa kawaida hutegemea ushirikina, unajimu, waaguzi, na vitabu maarufu vya ndoto vinavyoonyesha uhusiano uliopo kati ya nambari fulani na majina, tarehe, na ndoto. Badala ya kukazia kwamba kila nambari ina uwezekano uleule wa kuchaguliwa na kwamba kuchagua nambari inayopendwa na wengi kunaweza kupunguza faida, mashirika ya mchezo wa bahati nasibu huwatia wachezaji moyo kuchagua (na kutumia kila wakati) nambari ambazo wanaamini zinaweza kushinda.”

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Upendo wangu kwa Yehova ulinipa nguvu ya kuacha kucheza kamari.”—John

“Mbali na kuwa na maisha yenye kusudi, nina pesa nyingi zaidi mkobani.”—Linda

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Jambo la kushangaza ni kwamba mbali na kuacha kucheza kamari, sasa nachukia sana zoea hilo.”—Kazushige