Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Epuka Usemi Unaoumiza

Epuka Usemi Unaoumiza

Maoni ya Biblia

Epuka Usemi Unaoumiza

“Kutoka katika kinywa kilekile huja kubariki na kulaani. Haifai, ndugu zangu, mambo haya kuendelea kutukia kwa njia hii.”—YAKOBO 3:10.

UWEZO wa kusema ni jambo ambalo hututofautisha na wanyama. Kwa kusikitisha, watu hutumia vibaya zawadi hiyo. Matusi, kuapa, kukufuru, mizaha michafu, na lugha chafu ni namna za usemi zinazoweza kuumiza hata kuliko majeraha ya mwili. Biblia inasema: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga.”—Mithali 12:18.

Watu wengi zaidi huapa kwa ukawaida. Shule zinaripoti visa vingi zaidi vya watoto wanaotumia usemi usiofaa. Watu wengine hudai eti kutumia usemi wenye kuumiza kunaweza kumsaidia mtu atulie kihisia. Mwanafunzi mmoja wa sayansi ya siasa aliandika hivi: “Kutumia lugha chafu ni njia yenye nguvu ya kuwasilisha hisia zetu za ndani, wakati usemi wa kawaida hauwezi kufanya hivyo.” Je, Wakristo wanapaswa kuwa na maoni kama hayo ya kizembe kuelekea usemi wenye kuumiza? Mungu analionaje jambo hilo?

Chukia Kabisa Mzaha Wenye Aibu

Kutumia lugha chafu si jambo la kisasa tu. Je, utashangaa kufahamu kwamba usemi wenye aibu ulitumiwa katika siku za mitume, karibu miaka 2,000 iliyopita? Kwa mfano, inaonekana watu fulani katika kutaniko la Kolosai walitumia mizaha walipokuwa na hasira. Huenda walitumia usemi huo kimakusudi kuwaumiza wengine, au labda kulipiza kisasi. Vivyo hivyo, watu wengi leo hutumia lugha chafu wanapokuwa na hasira nyingi. Kwa hiyo, barua ya mtume Paulo inafaa wakati wetu pia. Paulo aliandika hivi: “Yawekeni mbali nanyi hayo, hasira ya kisasi, hasira, ubaya, usemi wenye kuudhi, na maongezi yenye aibu kutoka katika kinywa chenu.” (Wakolosai 3:8) Ni wazi kwamba Wakristo wanahimizwa waepuke mifoko ya hasira na matusi ambayo hutumiwa wakati mtu amekasirika.

Kweli, watu wengi hutumia usemi mbaya bila kusudi la kuumiza wengine. Huenda wao huutumia tu bila kufikiri. Hatimaye, maneno machafu yanaweza kukolea katika lugha ya kila siku. Wengine hata huona vigumu kuongea bila kutumia matusi. Mara nyingi mizaha hutumiwa kuwachekesha watu. Lakini je, usemi usiofaa unapaswa kuonwa kuwa kosa dogo, linaloweza kupuuzwa? Fikiria mambo yafuatayo.

Mzaha wenye aibu ni usemi unaochukiza unaokusudiwa kuchekesha watu. Leo usemi wa aina hiyo huwa hasa juu ya ngono. Watu wengi ambao hudai kuwa wanaheshimika hufurahia sana lugha hiyo. (Waroma 1:28-32) Basi haishangazi kwamba ngono inayofaa na isiyofaa hutajwa-tajwa na wanasarakasi wengi. Mizaha yenye aibu hutumiwa katika sinema, kwenye vipindi vya televisheni na redio.

Biblia inatoa shauri kuhusu mizaha yenye aibu. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo huko Efeso: “Acheni uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa hata visitajwe hata miongoni mwenu, kama vile ifaavyo watu watakatifu; wala mwenendo wa aibu wala maongezi ya kipumbavu wala kufanya mzaha wenye aibu, mambo yasiyofaa.” (Waefeso 5:3, 4) Ni wazi kwamba usemi mchafu humchukiza Mungu, hata iwe yule anayeutumia ana nia gani. Ni usemi usiofaa na unaoumiza.

Maneno Makali Yanayomchukiza Mungu

Usemi unaoumiza hutia ndani mengi zaidi ya kufanya mizaha. Matusi, kejeli, dhihaka, na kuchambua watu vikali huumiza sana. Tunakubali kwamba sisi hujikwaa kwa ulimi, hasa kwa sababu tunazungukwa na ulimwengu uliojaa kejeli na masengenyo. (Yakobo 3:2) Wakristo wa kweli hawapaswi kuiona lugha chafu kuwa jambo la kawaida tu. Biblia inasema waziwazi kwamba Yehova Mungu huchukia usemi wote unaoumiza.

Kwa mfano, katika kitabu cha Wafalme wa Pili, tunajifunza kuhusu kundi la vijana ambao walimfanyia mzaha nabii Elisha. Simulizi hilo linasema kwamba ‘walimfanyia mzaha’ na ‘kumwambia, “Paa wewe mwenye upaa! Paa wewe mwenye upaa!”’ Yehova, ambaye alisoma mioyo ya vijana hao na kutambua nia yao mbaya, alikasirika sana. Simulizi hilo linasema kwamba Mungu aliwaua wavulana 42 kwa sababu ya usemi wao wenye kuumiza.—2 Wafalme 2:23, 24.

Waisraeli “waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.” (2 Mambo ya Nyakati 36:16) Hata ingawa hasira ya Mungu ilichochewa hasa na ibada ya sanamu na kutotii kwa watu wake, inafaa tuzingatie kwamba Biblia inataja waziwazi usemi wenye kuumiza ulioelekezwa kwa manabii wa Mungu. Hiyo inaonyesha Mungu anachukia kabisa mwenendo kama huo.

Vivyo hivyo, Biblia inawahimiza Wakristo hivi: “Usichambue mwanamume mzee kwa ukali.” (1 Timotheo 5:1) Kanuni hiyo inaweza kutumiwa tunaposhughulika na watu wote. Biblia inatutia moyo ‘tusiseme kwa ubaya juu ya yeyote, tusiwe wataka-vita, tuwe wenye kukubali sababu, tukionyesha wazi upole wote kuelekea watu wote.’—Tito 3:2.

Kuzuia Midomo Yetu

Wakati mwingine, si rahisi kuepuka kishawishi cha kuwashambulia wengine kwa maneno. Mtu akikosewa, anaweza kuhisi akiwa na haki ya kumwadhibu yule aliyemkosea kwa maneno makali, yenye kuumiza, iwe ni kwa kusema naye au kwa kumsengenya. Lakini, Wakristo hukinza mwelekeo huo. Andiko la Mithali 10:19 husema hivi: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.”

Malaika wa Mungu huweka mfano mzuri. Wao wanajua makosa yote ambayo wanadamu hufanya. Ingawa malaika wana uwezo na nguvu nyingi kuliko wanadamu, hawawashtaki wanadamu kwa matusi, “kwa sababu ya kumstahi Yehova.” (2 Petro 2:11) Kwa kuwa wanajua Mungu anajua makosa ya kila mtu na anaweza kurekebisha mambo, malaika huizuia midomo yao. Mikaeli, yule malaika mkuu, hakuthubutu kutumia matusi, hata dhidi ya Ibilisi.—Yuda 9.

Wakristo hujitahidi kuwaiga malaika. Wanafuata himizo hili la Biblia: “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote. Andaeni mambo bora mbele ya macho ya watu wote. Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa, asema Yehova.’”—Waroma 12:17-19.

Hata hali na kiasi cha sauti yetu kinaweza kuumiza. Waume na wake huumizana mara nyingi kwa kufokeana kwa sauti ya juu. Wazazi wengi huwafokea watoto wao. Hata hivyo, haifai kupiga makelele tunapoelezea hisia zetu. Biblia inatusihi hivi: “Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) Pia Biblia inasema kwamba “mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali ahitaji kuwa mwanana kuelekea wote.”—2 Timotheo 2:24.

Maneno Yanayoponya

Kwa kuwa usemi wenye kuumiza na mizaha imeenea sana leo, Wakristo wanapaswa kutafuta njia ya kujizuia wasiyatumie. Biblia inasema njia nzuri ni kumpenda jirani. (Mathayo 7:12; Luka 10:27) Tukiwajali na kuwapenda majirani, hiyo itatusaidia kutumia maneno yanayoponya kila siku. Biblia inasema hivi: “Msiache usemi uliooza utoke kinywani mwenu, bali usemi wowote ule ulio mwema kwa ajili ya kujenga kama vile kuwezavyo kuwa na uhitaji, ili huo upate kuwapa wasikiaji lililo la kupendeleka.”—Waefeso 4:29.

Pia, Neno la Mungu likipenya akilini mwetu, litatusaidia kuepuka usemi wenye kuumiza. Kusoma na kutafakari Maandiko Matakatifu kunaweza kutusaidia ‘kuweka mbali uchafuko wote.’ (Yakobo 1:21) Naam, Neno la Mungu linaweza kuponya akili zetu.