Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Niliacha Kuwa Mtumwa wa Kileo

Niliacha Kuwa Mtumwa wa Kileo

Niliacha Kuwa Mtumwa wa Kileo

Kutumia kileo kwa kiasi kunaweza kufanya mlo upendeze au kuchangia shangwe ya karamu. Hata hivyo, kwa watu fulani kutumia kileo kunaweza kusababisha matatizo makubwa. Fikiria hadithi ifuatayo ya mtu aliyeacha kutumia kileo vibaya.

BADO nina hisia za uchungu ninapoeleza hali ilivyokuwa nyumbani kwetu. Baba na Mama wangeanza kunywa kileo. Kisha Baba angempiga Mama. Mara nyingi makonde yake yangenipata. Walipoamua kutengana, nilikuwa na umri wa miaka minne tu. Ninakumbuka nikipelekwa kuishi kwa nyanya.

Nilihisi hakuna anayenipenda. Nilipokuwa na umri wa miaka saba, ningeingia kwenye chumba fulani na kunywa divai iliyotayarishwa nyumbani, ambayo ni kana kwamba ilipunguza huzuni yangu. Nilipokuwa na umri wa miaka 12, mama aligombana kwa ukali na nyanya yangu kwa sababu yangu. Mama alikasirika sana hivi kwamba akanitupia uma mkubwa. Niliweza kuukwepa bila kuguswa! Hiyo haikuwa pindi pekee ambapo uhai wangu ulihatarishwa. Ingawa nilikuwa na vidonda mwilini, havikuwa vimechimbika kama vidonda vya kihisia vilivyokuwa ndani yangu.

Nilipofikia umri wa miaka 14, nilikuwa nikinywa kila mara. Mwishowe, nilipokuwa na umri wa miaka 17 nilitoroka nyumbani. Kunywa kulinifanya nijihisi huru, nami nikawa mjeuri, na kusababisha matatizo kwenye mikahawa iliyokuwa karibu. Jambo lililonipendeza maishani ni kunywa kileo tu. Kwa siku moja, ningekunywa lita tano za divai, chupa kadhaa za bia, na vileo vikali zaidi.

Nilipooa, kunywa kileo kulimletea mke wangu matatizo makubwa sana. Chuki na kufungiana kinyongo kuliongezeka, nami nilimpiga pamoja na watoto, na hivyo kutokeza hali mbaya ambayo nilikuwa nimelelewa nayo. Karibu pesa zote nilizopata nilizitumia kununua kileo. Hatukuwa na vitu vya nyumbani hivyo mimi na mke wangu tulilala sakafuni. Sikuwa na sababu ya kuendelea kuishi na sikufanya jitihada yoyote ya kuboresha hali yangu.

Siku moja nilizungumza na Shahidi wa Yehova. Nilimuuliza kwa nini kulikuwa na kuteseka kwingi, na Shahidi huyo akanionyesha kwenye Biblia ahadi ya Mungu ya ulimwengu usio na matatizo. Jambo hilo lilinisadikisha kiasi cha kwamba nikaanza kujifunza Biblia na Mashahidi. Nilipofuata mafundisho ya Biblia na kupunguza kiasi nilichokunywa, maisha ya familia yetu yalianza kuwa mazuri. Hata hivyo, nilitambua kwamba ikiwa nilitaka kumtumikia Yehova Mungu kwa njia inayokubalika nilipaswa kushinda tatizo langu la kutumia kileo vibaya. Baada ya kujitahidi kwa miezi mitatu, nilifaulu kuishi bila kunywa kileo. Miezi sita baadaye niliweka maisha yangu wakfu kwa Mungu na kuonyesha hilo kwa kubatizwa.

Baada ya kutoka kwenye utumwa wa kileo, nilifaulu kulipa madeni yangu. Hatimaye, nilinunua nyumba na gari ambalo tunatumia kwenda kwenye mikutano ya Kikristo na kuhubiri nyumba kwa nyumba. Mwishowe, nikaanza kujiheshimu.

Mara nyingine mimi hualikwa kunywa kileo kwenye tafrija. Wengi hawajui jitihada kubwa ninayofanya na kwamba kunywa tu kiasi kidogo kunaweza kunifanya nirudie hali yangu ya zamani. Tamaa ya kunywa kileo ipo bado ndani yangu. Ninahitaji kusali sana na jitihada nyingi ili kukataa kileo. Ninapohisi kiu, mimi hunywa kinywaji chochote kisichokuwa na kileo kwa wingi. Sijanywa kileo hata kidogo kwa miaka kumi sasa.

Yehova anaweza kufanya kile ambacho mwanadamu hawezi. Amenisaidia kufurahia uhuru ambao sikuwahi kuamini ninaweza kuwa nao! Bado mimi huumia kwa sababu ya matatizo ya kihisia niliyopata nikiwa mtoto, na ninaendelea kukabiliana na mawazo ya kushuka moyo. Kwa upande mwingine, nimebarikiwa kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu, kutaniko lenye marafiki wa kweli, na familia nzuri inayoshiriki imani yangu. Mke na watoto wangu wananisaidia katika pigano langu dhidi ya kileo. Mke wangu anasema: “Zamani maisha yangu yalikuwa magumu. Leo, ninathamini sana kwamba Yehova ameniruhusu kufurahia maisha mazuri ya familia pamoja na mume wangu na watoto wetu wawili.”—Tumetumiwa makala hii.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Nilipofikia umri wa miaka 14, nilikuwa nikinywa kila mara

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Yehova anaweza kufanya kile ambacho mwanadamu hawezi

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

MAONI YA BIBLIA KUHUSU KILEO

▪ Biblia haishutumu kutumia kileo. Inafafanua “divai ambayo hufanya moyo wa mwanadamu anayeweza kufa ushangilie,” kuwa zawadi kutoka kwa Mungu kwa ajili ya wanadamu. (Zaburi 104:14, 15) Biblia pia inaonyesha mzabibu kuwa mfano wa utajiri na usalama. (Mika 4:4) Hata muujiza wa kwanza ambao Yesu Kristo alifanya ulikuwa kugeuza maji kuwa divai kwenye karamu ya arusi. (Yohana 2:7-9) Na wakati mtume Paulo alisikia kuhusu “ugonjwa [wa Timotheo] wa mara kwa mara” alipendekeza anywe “divai kidogo.”—1 Timotheo 5:23.

▪ Biblia inashutumu kunywa kileo kupita kiasi:

“Walevi . . . hawataurithi ufalme wa Mungu kamwe.” —1 Wakorintho 6:9-11, “The Jerusalem Bible.”

“Msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake.”—Waefeso 5:18.

“Ni nani aliye na ole? Ni nani aliye na wasiwasi? Ni nani aliye na ugomvi? Ni nani aliye na mahangaiko? Ni nani aliye na majeraha yasiyo na sababu? Ni nani aliye na macho mazito? Ni wale wanaokaa muda mrefu kwenye divai, wale wanaoenda kutafuta divai iliyochanganyika. Usiitazame divai inapotoa rangi nyekundu, inapochemka katika kikombe, inaposhuka taratibu. Mwisho wake inauma kama nyoka, nayo hutoa sumu kama nyoka. Macho yako mwenyewe yataona mambo mageni, nao moyo wako mwenyewe utasema mambo yaliyopotoka.”—Methali 23:29-33.

Kama ilivyotajwa kwenye makala kuu, wengine ambao wamewahi kuwa na tatizo la kileo wameamua kutoitumia hata kidogo.—Mathayo 5:29.