Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Kifo Ndio Mwisho?

Je, Kweli Kifo Ndio Mwisho?

Je, Kweli Kifo Ndio Mwisho?

HUENDA hakuna jambo lingine ambalo limekuwa lenye kutatanisha na lenye kusumbua kama suala la kinachotupata baada ya kufa. Kwa maelfu ya miaka, watu wenye akili katika kila jamii wamejiuliza swali hilo. Lakini falsafa za wanadamu na utafiti wa kisayansi zimetokeza tu nadharia na hadithi nyingi.

Lakini namna gani mafundisho ya Biblia? Huenda wengine wakadai kwamba inapohusu suala la kifo na uhai baada ya kifo, Biblia pia ina majibu yenye kutatanisha. Hata hivyo, kusema kweli utata huo wote unasababishwa na dini nyingi ambazo huchafua mafundisho yaliyo wazi ya Biblia kwa uwongo na hadithi. Usipotilia maanani utamaduni na hadithi za watu na ushikamane na kile ambacho Biblia husema hasa, utatambua kwamba inatoa maelezo yanayopatana na akili na yanayotoa tumaini.

Ulikuwa Katika Hali Gani Kabla ya Kuzaliwa?

Kwa mfano, fikiria maandiko mawili ya Mfalme Sulemani yaliyonukuliwa katika makala iliyotangulia. Maandiko hayo yanaonyesha wazi kwamba wafu hawajui lolote kamwe, iwe ni wanadamu au wanyama. Hivyo, kulingana na Biblia, hakuna utendaji, ujuzi, hisia, au mawazo katika kifo.—Mhubiri 9:5, 6, 10.

Je, ni vigumu kuelewa jambo hilo? Hebu fikiria: Mtu alikuwa katika hali gani kabla ya kuwa hai? Ulikuwa wapi kabla ya chembe ndogo za wazazi wako kuungana na kutokeza mtu hai, yaani, wewe? Ikiwa mwanadamu ana kitu fulani kisichoonekana ambacho huendelea kuishi baada ya mtu kufa, kitu hicho huwa wapi kabla ya chembe hizo za wazazi wako kuungana? Ukweli ni kwamba, hukuwepo kabla ya kuwa mwanadamu kwa hiyo huna kumbukumbu lolote. Kabla mimba yako haijatungwa, hukuwepo. Huo ndio ukweli wa mambo.

Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba tunarudia hali ileile tuliyokuwa nayo kabla ya kuwa hai. Ni kama tu Mungu alivyomwambia Adamu baada ya kutenda dhambi: “Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:19) Wanadamu hawatofautiani na wanyama katika maana hiyo. Hali ya wafu iko kama vile tu Biblia inasema: “Mwanadamu si bora kuliko mnyama.”—Mhubiri 3:19, 20.

Je, hilo linamaanisha kwamba mwanadamu amekusudiwa aishi kwa miaka michache tu kisha atokomee milele? Au je, kuna tumaini kwa wafu? Fikiria yafuatayo.

Tamaa ya Asili ya Kuishi

Watu wengi hawapendi kuzungumza kuhusu kifo. Wengi hasa huepuka kuzungumzia au hata kufikiria kifo chao wenyewe. Kwa upande mwingine, wao huona watu wakifa kwa njia mbalimbali katika televisheni na sinema na pia vyombo vya habari huonyesha na kusimulia visa vya watu halisi wakifa.

Kwa sababu hiyo, vifo vya watu tusiowajua huonekana kuwa jambo la kawaida. Hata hivyo, kifo cha wapendwa wetu au chetu wenyewe si jambo la kawaida. Inakuwa hivyo kwa sababu wanadamu wana tamaa ya asili ya kuishi. Pia, tuna uwezo wa kutambua kupita kwa wakati na kufikiri kuhusu kuishi milele. Mfalme Sulemani aliandika kwamba Mungu “ameweka umilele katika mioyo ya wanadamu.” (Mhubiri 3:11, The Amplified Bible) Katika hali za kawaida sisi hutaka kuendelea kuishi mpaka wakati usiojulikana. Tunataka maisha yasiyo na kikomo. Hakuna uthibitisho wa kwamba wanyama wana tamaa kama hiyo. Wanaishi bila kutambua kwamba kuna wakati ujao.

Uwezo Mkubwa wa Mwanadamu

Wanadamu wana tamaa ya kuishi milele na pia uwezo wa kuwa na shughuli nyingi na kufanya maendeleo milele. Inaonekana kwamba uwezo wa mwanadamu wa kujifunza hauna kikomo. Inasemekana kwamba hakuna kitu chochote cha asili kilicho tata na chenye uwezo wa kujirekebisha upya kama ubongo wa mwanadamu. Tofauti na wanyama, sisi tuna akili ambayo inaweza kuelewa nadharia mbalimbali. Wanasayansi wana ujuzi wa kijuujuu tu kuhusu uwezo wa ubongo wa mwanadamu.

Utendaji mwingi wa ubongo huendelea hata tunapozeeka. Hivi karibuni, wanasayansi wa mfumo wa neva wamegundua kwamba utendaji mwingi wa ubongo hauathiriwi na uzee. Watafiti katika Taasisi ya Franklin ya Kujifunza Mbinu Mpya za Kisayansi wanaeleza hivi: “Ubongo wa mwanadamu una uwezo wa kubadilika na kufanyiza viunganishi vipya vya neva. Hata mtu anapozeeka, ubongo unaweza kutokeza chembe mpya za neva. Kwa kawaida kudhoofika sana kwa ubongo husababishwa na ugonjwa, ilhali kupoteza kumbukumbu au kushindwa kutumia misuli fulani ambako, mara nyingi kunahusianishwa na uzee, husababishwa hasa na kutofanya mazoezi ya mwili na akili.”

Kwa maneno mengine, tukiweza kuuzoeza ubongo wetu na kuukinga na magonjwa, unaweza kuendelea kufanya kazi milele. James Watson, mwanabiolojia wa molekuli ambaye alikuwa mmoja wa watu waliogundua muundo wa chembe za urithi, alisema hivi: ‘Ubongo, ndicho kitu tata zaidi ambacho tumepata kugundua katika ulimwengu wetu.’ Kitabu kilichoandikwa na Gerald Edelman, mwanasayansi wa mfumo wa neva kinaeleza kwamba sehemu ndogo ya ubongo inayolingana na kichwa cha kijiti cha kiberiti “ina miunganisho ya neva bilioni moja hivi ambayo inaweza kuungana katika njia ambazo zinaweza kufafanuliwa tu kuwa nyingi ajabu—nambari kumi ikifuatiwa na mamilioni ya sufuri.”

Je, ni jambo linalopatana na akili kufikiria kwamba wanadamu walio na uwezo huo walipaswa kuishi muda mfupi tu? Jambo hilo halipatani na akili kama vile tu si jambo linalopatana na akili kutumia gari la moshi lenye nguvu lililo na mabehewa mengi kusafirisha chembe ya mchanga kwa umbali wa sentimita chache tu! Kwa nini basi mwanadamu ana ubongo wenye uwezo mkubwa wa kubuni na kujifunza? Je, inawezekana kwamba tofauti na wanyama, wanadamu hawakupaswa kufa kamwe na kwamba waliumbwa waishi milele?

Tumaini Kutoka kwa Mwanzilishi wa Uhai

Kwa kuwa tumezaliwa tukiwa na tamaa ya kuishi na tuna uwezo mkubwa wa kujifunza, hilo linatufanya tufikie mkataa unaopatana na akili kwamba: Wanadamu waliumbwa waishi muda mrefu zaidi ya miaka 70 au 80 tu. Na hilo linatufanya tukate kauli kwamba: Lazima kuwe na Mbuni, Muumba, na Mungu. Sheria zisizobadilika za ulimwengu na kuwepo kwa viumbe wengi tata duniani kunaunga mkono imani ya kwamba kuna Muumba.

Ikiwa kwa kweli Mungu alituumba tukiwa na uwezo wa kuishi milele, kwa nini tunakufa? Ni nini hutukia baada ya kifo? Je, ni kusudi la Mungu kuwafufua wafu? Ni jambo linalopatana na akili kwamba Mungu mwenye hekima na nguvu angetupa majibu kwa maswali hayo, naye ametupa majibu hayo. Fikiria yafuatayo:

Kifo hakikuwa sehemu ya kusudi la Mungu la kwanza kwa mwanadamu. Andiko linalotaja kifo kwa mara ya kwanza linaonyesha kwamba mwanzoni Mungu hakukusudia wanadamu wafe. Simulizi la Biblia la Mwanzo linaeleza kwamba ili kuwapa wenzi wa ndoa wa kwanza, Adamu na Hawa, fursa ya kuonyesha upendo na ushikamanifu wao, Mungu aliwapa mtihani rahisi. Ulihusu kutokula matunda ya mti fulani. Mungu alisema: “Siku utakapokula, utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Adamu na Hawa wangekufa iwapo tu wangeasi, na hivyo kuanguka mtihani. Simulizi la Biblia linaonyesha kwamba hawakuwa washikamanifu kwa Mungu, na hivyo wakafa. Kwa njia hiyo, wanadamu wakarithi kutokamilika na kifo.

Biblia inalinganisha kifo na usingizi. Inazungumza kuhusu ‘kulala usingizi katika kifo.’ (Zaburi 13:3) Kabla ya kumfufua rafiki yake Lazaro, Yesu aliwaambia mitume wake hivi: “Lazaro rafiki yetu anapumzika, lakini ninafunga safari kwenda huko ili kumwamsha kutoka usingizini.” Na hivyo ndivyo Yesu alivyofanya! Biblia inasema kwamba alipomwita, “huyo mtu [Lazaro] aliyekuwa mfu akatoka” kwenye “kaburi” akiwa hai kabisa tena!—Yohana 11:11, 38-44.

Kwa nini Yesu alikilinganisha kifo na usingizi? Kwa sababu mtu anayelala hawezi kufanya lolote. Mtu akiwa amelala usingizi mzito hajui mahali alipo wala kupita kwa wakati. Hakuna maumivu au kuteseka. Vivyo hivyo, unapokufa huwezi kufanya au kufahamu chochote. Lakini kifo na usingizi vinafanana katika njia nyingine. Mtu anapolala anatarajia kuamka. Na hilo ndilo tumaini ambalo Biblia inatoa kwa ajili ya waliokufa.

Muumba mwenyewe anaahidi hivi: “Nitawakomboa wao kutoka katika mkono wa Kaburi; nitawaokoa wao kutoka kwenye kifo. Ee Kifo, iko wapi michomo yako? Ee Kaburi, yako wapi maangamizi yako?” (Hosea 13:14) Unabii mwingine wa Biblia unasema kwamba Mungu “kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isaya 25:8) Kitendo hicho cha kuwaleta kwenye uhai watu waliokufa kinaitwa ufufuo.

Wale watakaofufuliwa wataishi wapi? Kama ilivyozungumziwa awali, mwanadamu ana tamaa ya kuishi milele. Ungependa kuishi wapi milele? Je, ungefurahi kujua kwamba baada ya kufa ungeendelea kuishi ukiwa kama roho ama nguvu fulani inayoelea angani, kama dini fulani zinavyofundisha? Je, ungependa kuendelea kuishi ukiwa mtu mwingine, bila kuwa na kumbukumbu lolote la maisha yako kabla ya kifo chako? Je, ungefurahia kufufuliwa ukiwa mnyama au mti? Ikiwa ungepewa fursa ya kuchagua, je, ungependa kuishi katika ulimwengu ambao hauna mambo ambayo ulikuwa umezoea na kufurahia ulipokuwa mwanadamu duniani?

Kukiwa na hali nzuri, je, hungependa kuishi katika dunia paradiso? Hilo ndilo tumaini ambalo Biblia inatoa, kwamba watu wataishi milele hapa duniani. Mungu aliiumba dunia kwa kusudi hilo, ili ikaliwe na watu ambao watampenda na kumtumikia kwa furaha milele. Ndio maana Biblia inasema hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29; Isaya 45:18; 65:21-24.

Ufufuo utafanyika lini? Kwa kuwa kifo kinalinganishwa na usingizi, hilo linaonyesha kwamba kwa kawaida ufufuo hautokei mara tu mtu anapokufa. Kunakuwa na kipindi cha kulala “usingizi” mtu anapokufa hadi atakapofufuliwa. Katika Biblia, mtu fulani aitwaye Ayubu aliuliza swali hili: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Kisha akajibu: “Mimi nitangojea [katika kaburi], . . . mpaka kitulizo changu kije. Wewe [Mungu] utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.” (Ayubu 14:14, 15) Itakuwa shangwe iliyoje wafu watakapoungana tena na wapendwa wao!

Usiogope Sana Kifo

Ni kweli kwamba tumaini ambalo Biblia inatoa haliondoi hofu yote kuhusu kifo. Ni jambo la kawaida kuhofu maumivu na wasiwasi ambao nyakati nyingine hutokea kabla ya kifo. Inaeleweka kwamba huenda ukaogopa kumpoteza mpendwa wako. Na ikiwa unaogopa madhara yanayoweza kuwapata wapendwa wako ukifa, hilo ni jambo la kawaida pia.

Hata hivyo, kwa kufunua hali halisi ya wafu, Biblia inatusaidia kuepuka hofu kubwa ya kifo. Hakuna haja ya kuhofu kwamba baada ya kufa, utateswa na roho waovu katika moto wa mateso. Na hakuna haja ya kuhofia kuzimu ambako nafsi hutangatanga milele. Na pia huhitaji kuhofu hali ya kutokuwapo milele. Kwa nini? Kwa sababu Mungu ana kumbukumbu lisilo na mwisho naye anaahidi kuwafufua tena hapa duniani wafu wote walio katika kumbukumbu lake. Biblia inatuhakikishia hilo kwa maneno yafuatayo: “Kwetu, Mungu wa kweli ni Mungu wa matendo ya kuokoa; nazo njia za kutoka katika kifo ni za Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu.”—Zaburi 68:20.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”—Mwanzo 3:19

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“[Mungu] ameweka umilele katika mioyo ya wanadamu.”—Mhubiri 3:11, The Amplified Bible

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

MASWALI KUHUSU KIFO YAJIBIWA

Ni kweli kwamba kuna maswali kuhusu kifo na ufufuo ambayo hayakuzungumziwa katika makala hizi. Wengi wamepata majibu yenye kuridhisha kwa maswali hayo kwa kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Tunakutia moyo ufanye hivyo pia. Yafuatayo ni baadhi ya maswali ambayo utajibiwa:

▪ Maneno “moto wa mateso” na “ziwa la moto” ambayo yanapatikana katika Biblia yanamaanisha nini?

▪ Ikiwa hakuna moto wa mateso, watu wabaya wataadhibiwaje?

▪ Kulingana na Biblia, roho hutoka mwilini mtu anapokufa. Roho hiyo ni nini?

▪ Kwa nini kuna habari nyingi kuhusu watu ambao wamewasiliana na wafu?

▪ Neno “nafsi” linamaanisha nini katika Biblia?

▪ Ni lini watu watafufuliwa na kuishi kwenye paradiso?

▪ Je, wote wanaokufa watafufuliwa haidhuru mwenendo wao ulikuwaje walipokuwa hai?

Tafadhali soma ukurasa wa nyuma wa gazeti hili ili uone jinsi unavyoweza kupata jibu la wazi, linalotegemea Biblia la kila moja ya maswali haya.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu alisema ‘angemwamsha Lazaro kutoka usingizini’

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Wazia furaha itakayokuwepo wapendwa waliokufa watakapofufuliwa!