Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Je, Ndoa Inaweza Kustahimili Msukosuko? (Julai 2006) Mimi husoma Amkeni! kwa ukawaida. Ingawa mimi ni Mkatoliki, nimegundua kwamba magazeti yenu yanavutia na yanaelimisha. Hata hivyo, sikubaliani na maelezo yenu yafuatayo: “Mnamo 1983 kanisa hilo lililegeza sheria zake kuhusu ndoa na kufanya iwe rahisi zaidi kwa Wakatoliki kuvunja ndoa.”

G.V.M., Zambia

“Amkeni!” lajibu: Tulikuwa tunarejezea mabadiliko yaliyofanywa katika Orodha ya Kanuni za Kanisa ya mwaka wa 1983. Matokeo ya mabadiliko hayo yamekuwa makubwa, hasa nchini Marekani. Kulingana na Askofu wa Kanisa Katoliki Mark A. Pivarunas, ni ndoa 338 tu zilizovunjwa mnamo 1968 nchini Marekani. Lakini kufikia mwaka wa 1990, idadi ya ndoa zilizovunjwa iliongezeka kufikia 62,824. Kwa nini kulikuwa na ongezeko kubwa hivyo?

Mwanasheria wa kanuni za kanisa Edward Peters, anasema hivi: “Mabadiliko makubwa katika orodha ya kanuni za kanisa yamefanywa katika kipindi cha miaka 30 iliyopita, mabadiliko hayo yamefanya iwe rahisi kwa watu kuomba ndoa zao kuvunjwa na kuongeza uwezekano wa maombi yao kukubaliwa.” Baada ya kuonyesha baadhi ya mabadiliko yaliyofanywa katika kanuni hizo, Peters aliongeza hivi: “Kila moja ya mabadiliko yaliyofanywa na Vatican kwenye orodha ya kanuni za kanisa yamechangia sana kuongezeka kwa idadi ya ndoa zinazovunjwa.” Bila kujali lengo lao lilikuwa nini, matokeo ya kubadilishwa kwa kanuni hizo yameonekana wazi huko Marekani kama gazeti la “Amkeni!” lilivyoeleza: “[Kanisa] lilifanya iwe rahisi kwa Wakatoliki kuvunja ndoa zao.”

Je, Kuna Muumba? (Septemba 2006) Toleo hilo la pekee la Amkeni! liliandikwa kwa ustadi mkubwa sana. Hoja zilizotolewa zilieleweka kwa urahisi, zilikuwa zenye nguvu, na zinazopatana na akili. Nilipendezwa sana na mpangilio wa gazeti lenyewe kwani gazeti zima lilizungumzia kichwa kimoja kwa maoni tofauti-tofauti.

A. B., Hispania

Asanteni sana kwa gazeti hilo lililoandikwa kwa umakini na lenye kuvutia sana. Hoja na picha nyingi zinamletea Yehova heshima. Anastahili kutukuzwa kwa njia hiyo.

R. B., Uswisi

Nilisadikishwa kutokana na uthibitisho rahisi wa kwamba vitu viliumbwa. Fundisho la mageuzi lilifunuliwa waziwazi kuwa la uwongo kupitia hoja sahihi zinazopatana na sayansi bila kuibua hisia za chuki.

L. G., Ufaransa

Waromani—Miaka Elfu ya Shangwe na Majonzi (Oktoba 2006) Sikuzote nimewapenda Waromani. Inasikitisha kwamba bado wanaendelea kubaguliwa. Nina hakika kwamba makala hiyo itawasaidia wengi kuwa na mtazamo tofauti. Jinsi inavyotia moyo kujua kwamba Yehova hana ubaguzi na kwamba Waromani ni miongoni mwa waabudu wake!

B. B., Ufaransa

Sisi ni Waromani. Baba yangu bado si Shahidi wa Yehova, na hafurahii sana kusoma. Hata hivyo, alitaka sana gazeti hilo, na sasa liko juu ya meza yake!

A. G., Finland