Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nyumba Iliyogawanyika—Jinsi Talaka Inavyowaathiri Vijana

Nyumba Iliyogawanyika—Jinsi Talaka Inavyowaathiri Vijana

Nyumba Iliyogawanyika—Jinsi Talaka Inavyowaathiri Vijana

WATAALAMU walifikiri wanajua mashauri yanayofaa zaidi. Waliwaaambia wazazi walio katika ndoa zenye matatizo kwamba ‘Unapaswa kukazia fikira furaha yako,’ na wakaongezea hivi: ‘Usijali kuhusu watoto. Wao wanaweza kubadilikana kulingana na hali. Ni rahisi kwao kukabiliana na talaka kuliko kuishi na wazazi wawili ambao wanazozana kila wakati!’

Hata hivyo, washauri fulani ambao hapo awali walipendekeza talaka sasa wamebadili maoni yao. Sasa wanasema, ‘Talaka ni kama vita. Kila mtu hujeruhiwa; kutia ndani watoto.’

Uwongo Kuhusu Talaka

Hadithi hii yenye vichekesho inaweza kuwa yenye kusisimua kwenye televisheni. Baba na Mama wanatalikiana. Mama anapata kibali cha kuwalea watoto, kisha anaolewa na mwanamume aliyefiwa na mke wake ambaye pia ana watoto. Kila juma, familia hiyo inakabiliana na tatizo moja baada ya lingine, lakini kila tatizo linasuluhishwa kwa ucheshi mwingi katika muda wa dakika 30 tu.

Huenda hadithi hiyo ikawa yenye kusisimua kwenye televisheni. Lakini talaka halisi si hadithi yenye vichekesho. Talaka huumiza sana. “Talaka huhusisha kuchukua hatua za kisheria,” anaandika M. Gary Neuman katika kitabu chake Emotional Infidelity. “Mzazi mmoja anamshtaki yule mwingine. Punde tu unapoamua kumtaliki mwenzi wako, unapoteza udhibiti juu ya watoto wako. Pia unaacha kuwa na udhibiti juu ya pesa zako na huenda hata mahali utakapoishi. Huenda mkatatua matatizo yenu kortini lakini huenda pia msiyatatue. Jambo kuu ni kwamba mtu usiyemjua anayeitwa hakimu ndiye atakayeamua utawaona watoto wako mara ngapi na utabaki na kiasi gani cha pesa. Jambo la kusikitisha ni kwamba hakimu huyo haoni mambo kama wewe unavyoyaona.”

Mara nyingi, talaka husuluhisha matatizo fulani na kutokeza mengine. Kwa kweli, kila kitu kitabadilika iwe ni maisha yako au hali yako ya kiuchumi, na huenda yasiwe mabadiliko mazuri. Kisha kuna madhara ya talaka kwa watoto.

Jinsi Talaka Inavyowaathiri Vijana

Talaka inaweza kuwaumiza sana watoto, haidhuru wana umri gani. Wengine hudai kwamba vijana wanaobalehe hawaumizwi sana. Kwani watu wengine wanadhani kwamba, vijana hao wamekomaa zaidi na wanafikia hatua ya kujitenga na wazazi wao. Hata hivyo, watafiti wanaona madhara ya talaka. Wamegundua kwamba kwa sababu hizohizo, talaka inaweza kuwaathiri sana vijana wanaobalehe. * Fikiria mambo yafuatayo:

▪ Vijana wanapopitia kipindi cha kubalehe, wanakuwa na wasiwasi mwingi labda hata kuliko ule waliokuwa nao walipokuwa watoto. Usidanganywe na wazo la kwamba wanataka uhuru zaidi, wakati huo ndipo wanapohitaji mwongozo wa familia imara kuliko wakati mwingine wowote.

▪ Wakati ambapo vijana hao wanajifunza kuanzisha urafiki na watu waliokomaa, talaka inawafundisha wawe na shaka kuhusu viwango kama vile uaminifu, ushikamanifu, na upendo. Baadaye, watakapokuwa watu wazima, huenda wakaepuka kabisa kuwa na mahusiano ya karibu.

▪ Ingawa ni kawaida kwa watoto wa miaka yote kuonyesha kwamba wanaumia, vijana wanaobalehe wanaweza kufanya hivyo kwa njia hatari, kama vile kuvunja sheria, kutumia kileo vibaya, na kutumia dawa za kulevya.

Hilo halimaanishi kwamba vijana wanaobalehe ambao wazazi wao wanatalikiana hawawezi kabisa kuwa na uhusiano mzuri na watu wengine au kufanikiwa maishani. Wanaweza kufanikiwa, hasa ikiwa wana uhusiano na wazazi wote wawili. * Hata hivyo, si jambo linalopatana na akili kufikiria kama watu fulani wanavyofikiri kwamba talaka ‘itawafaidi watoto’ au kwamba itaondoa mizozano kati ya wenzi wa ndoa. Kwa kweli, wengine wameona kwamba wanahitaji kushirikiana zaidi na mwenzi wao “asiyeweza kuvumilika” baada ya talaka kuliko walivyofanya kabla na wanahitaji kuzungumzia masuala yanayoweza kusababisha ugomvi kama vile, utegemezo wa kifedha au nani atakayewalea watoto. Katika visa kama hivyo, talaka haisuluhishi matatizo ya familia, inayahamisha tu kwenye uwanja mwingine.

Suluhisho Lingine

Vipi ikiwa uko katika ndoa yenye matatizo na umefikiria kuhusu talaka? Makala hii imetoa sababu zenye kusadikisha kwa nini unapaswa kufikiria tena uamuzi wako. Talaka haisuluhishi matatizo yote ya ndoa.

Lakini usielewe jambo hili kimakosa: Suluhisho si kuvumilia katika ndoa yenye matatizo. Kuna suluhisho lingine—Ikiwa ndoa yako ina matatizo, mbona usijitahidi kuiboresha? Usikate kauli upesi kwamba haiwezekani kutatua matatizo ya ndoa yako. Jiulize maswali haya:

▪ ‘Ni sifa zipi ambazo zilinifanya nivutiwe na mwenzi wangu? Je, bado ana sifa hizo kwa kadiri fulani?’—Methali 31:10, 29.

▪ ‘Je, hisia nilizokuwa nazo kabla ya kufunga ndoa zinaweza kuchochewa tena?’—Wimbo wa Sulemani 2:2; 4:7.

▪ ‘Licha ya mambo ambayo mwenzi wangu anafanya, je, mimi ninaweza kutumia mapendekezo yaliyo kwenye ukurasa wa 3 hadi 9 wa gazeti hili?’—Waroma 12:18.

▪ ‘Je, ninaweza kumweleza mwenzi wangu (moja kwa moja au kwa kumwandikia) jinsi ninavyotaka kuboresha uhusiano wetu?’—Ayubu 10:1.

▪ ‘Je, tunaweza kuzungumza na rafiki mkomavu anayeweza kutusaidia kuweka miradi itakayoboresha ndoa yetu?’—Methali 27:17.

Biblia inasema hivi: “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” (Methali 14:15) Kanuni hiyo inatumika mtu anapochagua mwenzi na pia anapofikiria jinsi ya kutatua matatizo katika ndoa. Kwa kweli, kama iliyotajwa katika ukurasa wa 9 wa gazeti hili, familia zilizofanikiwa huwa pia na matatizo, tofauti ni jinsi zinavyoyatatua matatizo hayo.

Kwa mfano: Hebu wazia unasafiri mbali kwa gari. Bila shaka, utakabili matatizo njiani, iwe ni hali mbaya ya hewa, msongamano wa magari, au vizuizi njiani. Nyakati nyingine, huenda hata ukapotea njia. Utafanya nini? Je, utarudi nyumbani au utatafuta njia ya kukabiliana na tatizo lako na kusonga mbele? Siku ulipofunga ndoa, ulianza safari ambayo bila shaka ingekuletea matatizo, kwa kuwa Biblia inasema kwamba ‘wale wanaooa watakuwa na dhiki katika mwili wao.’ (1 Wakorintho 7:28) Jambo kuu si iwapo utapatwa na matatizo bali ni jinsi utakavyoyashughulikia yanapotokea. Je, unaweza kupata njia ya kukabiliana na tatizo na kusonga mbele? Hata ikiwa unahisi kwamba ndoa yako haiwezi kurekebishwa, je, utajaribu kutafuta msaada?—Yakobo 5:14.

Mungu Ndiye Aliyeanzisha Ndoa

Ndoa ilianzishwa na Mungu na inapaswa kuchukuliwa kwa uzito. (Mwanzo 2:24) Unapoona ni kana kwamba hupati suluhisho la matatizo yako, kumbuka mambo yaliyozungumziwa katika makala hii.

1. Jaribu kuchochea tena upendo ulio kuwa nao mwanzoni.—Wimbo wa Sulemani 8:6.

2. Amua ni jambo gani ambalo wewe unaweza kufanya ili kuboresha ndoa yako, na ulifanye.—Yakobo 1:22.

3. Kwa njia ya waziwazi lakini kwa heshima mwambie mwenzi wako—iwe ni moja kwa moja au kwa kumwandikia—ni mambo gani ambayo unaona yanahitaji kufanywa ili kuboresha ndoa yenu.—Ayubu 7:11.

4. Tafuta msaada. Si lazima ujaribu kuokoa ndoa yako ukiwa peke yako!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Makala hii inakazia fikira vijana wanaobalehe, lakini talaka huwaathiri watoto wadogo vilevile. Kwa habari zaidi, ona magazeti ya Amkeni! ya Desemba 8, 1997 (8/12/1997), ukurasa wa 3-12, na Aprili 22, 1991 (22/4/1991), ukurasa wa 3-11.

^ fu. 13 Kwa kweli, huenda isiwe rahisi nyakati zote kuwa na uhusiano na wazazi wote wawili, hasa ikiwa mzazi mmoja aliiacha familia au anakataa kuwapa mahitaji yao au hata anahatarisha uhai wao.—1 Timotheo 5:8.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

‘PINDI HII NDOA YANGU ITAFANIKIWA’

Uchunguzi unaonyesha kwamba mtu anapofunga ndoa mara ya pili, kuna uwezekano mkubwa wa ndoa hiyo kuvunjika, na hali ni mbaya hata zaidi unapofunga ndoa mara ya tatu. Katika kitabu chake Emotional Infidelity, M. Gary Neuman anaeleza sababu moja: “Ikiwa una matatizo katika ndoa yako ya kwanza,” anaandika, “si kwa sababu ulichagua mwenzi asiyefaa. Wewe ndiye mwenye tatizo. Ulimpenda mtu huyo. Vitu mlivyo navyo mmevipata pamoja na vile ambavyo hamna ni ninyi wawili ambao mmeshindwa kuvipata.” Neuman alifikia mkataa gani? “Ni afadhali kusuluhisha tatizo na kubaki na mwenzi wako kuliko kumwacha mwenzi wako na kubaki na tatizo.”

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

NDOA INAPOVUNJIKA

Biblia inaonyesha wazi kwamba wenzi wa ndoa wanapopitia hali fulani wasizoweza kuvumilia wanaweza kutalikiana. * Familia yako inapopatwa na hali kama hiyo, utawasaidia watoto wako jinsi gani kukabiliana na hali hiyo?

Mwambie kijana wako kinachotendeka. Ikiwezekana, wazazi wote wawili wanapaswa kufanya hivyo. Wote wanapaswa kumjulisha kwamba uamuzi wao wa kutalikiana hautabadilika. Wanapaswa kumhakikishia kwamba si yeye aliyesababisha watalikiane na kwamba wazazi wote wawili wataendelea kumpenda.

Acheni kupigana, vita vimekwisha. Wazazi fulani huendelea kuzozana muda mrefu baada ya kutalikiana. Mtaalamu mmoja alisema kwamba wanakuwa “wametalikiana kisheria lakini bado ni wapiganaji waliounganishwa kihisia ambao hawajafaulu kufanya mapatano ya amani.” Hilo haliwanyimi tu vijana nafasi ya kuwa na wazazi wao—kwa kuwa kila wakati Baba na Mama huwa wanazozana—lakini pia linawatia moyo wawagonganishe wazazi ili wapate wanachotaka. Kwa mfano, mtoto anaweza kumwambia mama yake: “Baba hajali hata nikirudi nyumbani saa ngapi. Kwa nini wewe unanizuia?” Kwa kuwa hataki mtoto huyo aegemee upande wa baba, mama humwacha afanye anachotaka.

Mruhusu kijana atoe maoni yake. Huenda vijana wakawa na maoni haya, ‘Ikiwa wazazi wangu waliacha kupendana basi huenda wakaacha kunipenda,’ au ‘Ikiwa wazazi wangu walivunja sheria, mbona mimi nisizivunje?’ Ili kupunguza wasiwasi wa kijana wako na kurekebisha maoni yake yasiyofaa, mruhusu atoe maoni yake. Lakini tahadhari: Usitafute utegemezo wa kihisia kutoka kwa mtoto wako. Huyo ni mtoto wako, si msiri wako.

Mtie moyo kijana wako awe na uhusiano mzuri na mwenzi wako mliyetalikiana. Mtu uliyemtaliki si mwenzi wako tena, lakini bado yeye ni mzazi wa mtoto wako. Kusema mambo mabaya kumhusu kutaleta madhara. Kitabu Teens in Turmoil—A Path to Change for Parents, Adolescents, and Their Families kinasema hivi: “Ikiwa wazazi wanapotalikiana watawatumia watoto wao kama silaha, lazima watarajie kuvuna walichopanda.”

Jitunze. Nyakati nyingine, huenda ukahisi umelemewa sana. Lakini usikate tamaa. Jipangie ratiba nzuri. Ikiwa wewe ni Mkristo, jihusishe katika utendaji wa kiroho. Kufanya hivyo kutakusaidia wewe na kijana wako muwe na usawaziko.—Zaburi 18:2; Mathayo 28:19, 20; Waebrania 10:24, 25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 38 Kulingana na Biblia, msingi pekee wa talaka kukiwa na uwezekano wa kufunga ndoa tena ni ngono nje ndoa. (Mathayo 19:9) Mwenzi mmoja anapokosa kuwa mwaminifu, mwenzi asiye na hatia—si watu wa familia au wengine—ndiye atakayeamua ikiwa atamtaliki.—Wagalatia 6:5.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Jitahidi sana kutimiza nadhiri ulizoweka siku ya arusi yako

[Picha katika ukurasa wa 21]

Ikiwa nyote mna kibali cha kuwalea watoto wenu, mtie moyo kijana wako awe na uhusiano mzuri na mwenzi wako mliyetalikiana