Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sisi Sote Ni Familia Moja

Sisi Sote Ni Familia Moja

Sisi Sote Ni Familia Moja

UNAWAONAJE watu wa rangi au kabila tofauti na lako? Je, unawaona wote kuwa sawa? Kwa kusikitisha, watu wengi huwaona watu wa rangi nyingine kuwa duni. Kamusi moja inafafanua “ubaguzi wa rangi” kuwa “imani ya kwamba jamii ya mtu ndiyo huamua tabia na uwezo wake utakuwaje na kwamba tofauti za rangi huwafanya watu wa jamii fulani wazaliwe wakiwa bora zaidi kuliko wengine.”

Imani hiyo imetokeza matatizo mengi sana. Kujiona kuwa watu bora zaidi “kumewafanya watu waone ni sawa kuwatawala na kuwafanya wengine kuwa watumwa,” akaandika Profesa Wen-Shing Tseng katika kitabu chake, Handbook of Cultural Psychiatry. Aliongeza kwamba watu wametumia rangi yao “kutetea ukosefu wa usawa wa kijamii, kiuchumi, na kisiasa.” Hata leo, ubaguzi wa rangi unaendelea katika nchi nyingi ulimwenguni. Lakini je, imani hiyo ni ya kweli? Sayansi na Biblia zinasema nini?

Sayansi Inasema Nini?

Uchunguzi wa chembe za urithi (DNA) umethibitisha uwongo wa kwamba watu wa jamii fulani wana chembe zinazowafanya wawe bora kuliko wengine. Watafiti waliowachunguza watu kutoka mabara tofauti waligundua kwamba tofauti zilizopo katika chembe za urithi za watu waliotoka sehemu yoyote ulimwenguni ilikuwa asilimia 0.5 hivi. * Na asilimia 86 hadi 90 ya tofauti hizo zilipatikana kati ya watu wa rangi ileile. Kwa hiyo, ni asilimia 14 tu ya tofauti hizo inayopatikana kati ya watu wa rangi tofauti.

Kwa kuwa “wanadamu wana muundo unaofanana wa chembe za urithi,” linasema jarida Nature, “elimu hiyo inapaswa kuwa muhimu ili kutatua tatizo la ubaguzi wa rangi.”

Mawazo kama hayo si mapya. Kuanzia mwaka wa 1950 Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi, na Utamaduni lilichapisha taarifa kadhaa zilizokusudiwa kukabiliana na ubaguzi wa rangi. Taarifa hizo ziliandikwa na wataalamu wanaochunguza desturi za wanadamu, wataalamu wa chembe za urithi, na wanasoshiolojia. Hata hivyo, ubaguzi wa rangi bado unaendelea. Kwa kweli, kujua tu mambo hakika hakutoshi. Lazima moyo wa mtu, au yule mtu wa ndani, pia aguswe. “Mawazo mabaya hutoka moyoni,” akasema Yesu Kristo.—Mathayo 15:19, 20.

Maoni ya Biblia

Biblia iliandikwa ili ichochee moyo. Kwa mfano, zaidi tu ya kutoa ukweli huu wa kisayansi kwamba “[Mungu] alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima,” Biblia inasema hivi pia: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35; 17:26) Je, hilo halifanyi umpende Mungu zaidi?—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Yehova Mungu anataka tuonyeshe kwamba tunampenda kwa kuwa kama yeye. “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo,” linasema andiko la Waefeso 5:1, 2. “Kutembea katika upendo” kunatia ndani kuwapenda watu kama Mungu anavyowapenda, haidhuru wao ni wa rangi au kabila gani.—Marko 12:31.

Mungu hawezi kuwakubali watu waliojaa ubaya moyoni, kutia ndani watu wenye chuki na ubaguzi wa rangi, wawe watumishi wake. (1 Yohana 3:15) Kwa kweli, hivi karibuni sana Mungu atawaondoa wanadamu wote waovu kutoka duniani. Ni wale tu wanaoiga sifa zake watakaobaki. Kisha wanadamu watakuwa familia moja tu kihalisi—kimwili na kiroho.—Zaburi 37:29, 34, 38.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Hata hivyo, tofauti hizo chache za chembe za urithi ni muhimu sana katika tiba kwa sababu magonjwa fulani huwaathiri watu wa jamii fulani tu.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

“Wanadamu wana muundo unaofanana wa chembe za urithi,” yaani, wao wote ni sawa