Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Walikuwa Watawa, Sasa Ni Dada Kiroho

Walikuwa Watawa, Sasa Ni Dada Kiroho

“USIZUNGUMZE nami. Sitaki kusikia jambo lingine lolote kuhusu dini yako. Inanichukiza sana. Sikupendi!” Mdogo wangu wa kike, Araceli, alisema maneno hayo kwa hasira. Ingawa sasa nina umri wa miaka 91, bado ninakumbuka jinsi maneno hayo yalivyoniumiza. Lakini Mhubiri 7:8 inasema kwamba “mwisho wa jambo ni bora kuliko mwanzo wake,” na ndivyo ilivyokuwa katika kisa chetu.—Felisa.

Felisa: Nilizaliwa kwenye familia iliyopenda sana dini. Kwa kweli, watu 13 wa familia yetu walikuwa makasisi au watu wenye vyeo mbalimbali katika dini ya Katoliki. Hata Papa John Paul II alipendekeza binamu ya mama yangu awe mtakatifu. Alikuwa kasisi na alifundisha katika shule moja ya Kikatoliki. Hata hivyo, familia yetu ilikuwa ya hali ya chini. Baba alikuwa mhunzi, na mama alifanya kazi shambani. Nilikuwa mtoto wa kwanza kati ya watoto nane.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Hispania vilianza. Baada ya vita, baba alifungwa gerezani kwa kuwa serikali ya kidikteta haikufurahishwa na maoni yake kuhusu uhuru. Haikuwa rahisi kwa Mama kutuandalia chakula, hivyo rafiki yake alipendekeza kwamba awapeleke wadogo zangu watatu wa kike—Araceli, Lauri, na Ramoni—kwenye makao ya watawa yaliyoko Bilbao, Hispania. Angalau hawangekosa chakula wakiwa huko.

Araceli: Wakati huo nilikuwa na miaka 14, Lauri alikuwa na miaka 12, na Ramoni miaka 10 tu. Hivyo haikuwa rahisi kuishi mbali na familia yetu. Huko Bilbao tulipewa kazi ya kufanya usafi. Miaka miwili baadaye, tulihamishiwa katika makao makubwa zaidi ya watawa huko Zaragoza ambayo yalitumika kuwatunza wazee. Tulipewa kazi ya kusafisha jiko, ambayo ilikuwa yenye kuchosha sana kwa vijana wadogo.

Felisa: Wadogo zangu walipopelekwa katika jiji la Zaragoza, mama na mjomba wangu, ambaye alikuwa kasisi wa eneo letu, waliamua kunipeleka pia nikafanye kazi katika makao hayo. Walifikiri kwamba kufanya hivyo kungenitenganisha na mvulana fulani aliyekuwa akivutiwa nami. Kwa kuwa nilipenda sana dini, nilifurahishwa na wazo la kuishi kwenye makao ya watawa kwa muda. Nilikuwa nikihudhuria Misa kila siku, na hata nilifikiria kuwa mmishonari kama binamu yangu aliyekuwa mtawa wa kiume katika nchi moja ya Afrika.

Makao ya watawa jijini Zaragoza, Hispania; (kushoto) Biblia tafsiri ya Nácar-Colunga (kulia)

Watawa hawakuchochea tamaa yangu ya kumtumikia Mungu katika nchi nyingine, na nilihisi kana kwamba nimefungwa gerezani nilipokuwa huko. Hivyo mwaka mmoja baadaye, niliamua kurudi nyumbani ili nimtunze mjomba wangu aliyekuwa kasisi. Nilifanya kazi za nyumbani lakini pia tulikariri Sala ya Rozari pamoja kila jioni. Nilipenda pia kupanga maua kanisani na kupamba sanamu za bikira na za “watakatifu.”

Araceli: Wakati huohuo, maisha yetu katika makao ya watawa yalibadilika. Baada ya kula viapo vya kwanza, watawa waliamua kututenganisha mimi na dada zangu. Ramoni alibaki Zaragoza, Lauri alipelekwa Valencia, nami nilipelekwa Madrid, na huko nilikula viapo vya pili. Makao ya Madrid yalikuwa na mahali pa kulala kwa ajili ya wanafunzi, wazee, na wageni wengine, hivyo kulikuwa na kazi nyingi sana. Nilifanya kazi kwenye chumba cha kuwatunzia wagonjwa.

Kusema kweli, nilitazamia maisha ya utawa yangekuwa yenye kuridhisha zaidi. Nilitazamia kwamba tungesoma Biblia na kuilewa. Lakini hakuna aliyezungumza kumhusu Mungu au Yesu, na hatukutumia Biblia. Nilijifunza tu Kilatini kidogo, maisha ya “watakatifu,” na kumwabudu Maria. Lakini mara nyingi tulifanya kazi ngumu.

Nilianza kuwa na mahangaiko, hivyo nilizungumza na mama mkuu wa makao hayo. Nilimwambia kwamba sioni haja ya kufanya kazi kwa bidii na kuwanufaisha watu wengine ilhali familia yangu ilihitaji msaada wangu. Alinifungia ndani ya chumba kidogo akitazamia kwamba nitabadili maoni yangu ya kutaka kuondoka.

Mara tatu, watawa waliniachilia huru, ili waone ikiwa bado nilitaka kuondoka. Kwa kuwa niliazimia kabisa kuondoka, waliniambia niandike hivi: “Ninaondoka kwa sababu ninachagua kumtumikia Shetani badala ya kumtumikia Mungu.” Jambo hilo lilinishtua sana, na ingawa niliazimia kuondoka, nisingeweza kamwe kuandika maneno hayo. Mwishowe, niliomba kuzungumza na padri muungamishaji, na nikamweleza kilichotokea. Alifanya mpango ili dayosisi inihamishie katika makao ya watawa niliyoishi zamani huko Zaragoza. Nilikaa huko kwa miezi michache, kisha niliruhusiwa kuondoka. Muda mfupi baadaye, Lauri na Ramoni waliondoka pia katika makao ya watawa.

KITABU “KILICHOKATAZWA” CHATUTENGANISHA

Felisa

Felisa: Baada ya muda, niliolewa na kuhamia Cantabria. Niliendelea kuhudhuria Misa kwa ukawaida, na Jumapili moja nilisikia tangazo lenye kushangaza kutoka jukwaani. Kasisi alisema hivi kwa hasira, “Tazama kitabu hiki!” na akaonyesha kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Kisha akasema, “Ikiwa umepewa kitabu hiki na mtu yeyote, kilete kwangu au ukitupe!”

Sikuwa na kitabu hicho, lakini nilitaka kukipata haraka iwezekanavyo. Kwa kushangaza, siku chache baadaye Mashahidi wawili walinitembelea na kunipa kitabu hicho “kilichokatazwa.” Usiku huohuo nilikisoma, na wanawake hao waliporudi, nilikubali kujifunza Biblia pamoja nao.

Kitabu “kilichokatazwa”

Baada ya muda mfupi kweli iligusa moyo wangu. Zamani nilipenda dini, lakini sasa nilianza kumpenda sana Yehova na kuwa na bidii katika huduma. Nilibatizwa mwaka wa 1973. Ingawa sikuwa na fursa nyingi za kuwahubiria watu wa familia yetu, nilijitahidi kadiri ya uwezo wangu. Na kama nilivyoeleza mwanzoni, washiriki wa familia, hasa mdogo wangu Araceli, walipinga sana imani yangu.

Araceli: Mambo mabaya niliyopitia kwenye makao ya watawa yalinifanya nichukie dini. Hata hivyo, niliendelea kuhudhuria Misa kila Jumapili, na kukariri Sala ya Rozari kila siku. Lakini bado nilikuwa na tamaa kubwa ya kuijua Biblia, na nilimwomba Mungu anisaidie. Dada yangu, Felisa, aliponieleza kuhusu imani yake mpya, alikuwa na shauku sana hivi kwamba nilihisi anashikilia mambo bila kufikiri. Sikukubaliana naye hata kidogo.

Araceli

Baada ya miaka michache, nilirudi Madrid kwenda kufanya kazi na nikaolewa. Pole kwa pole nilianza kuwa na mashaka kuhusu mambo fulani. Nilitambua kwamba watu ambao walihudhuria Misa kwa ukawaida hawakutumia mafundisho ya Injili maishani mwao. Hivyo niliacha kwenda kanisani. Sikuamini tena mafundisho kuhusu “watakatifu,” kuungama, au moto wa mateso. Hata nilitupa sanamu zangu zote. Sikujua kama nilikuwa nikifanya jambo linalofaa. Nilivunjika moyo, lakini niliendelea kusali hivi kwa Mungu: “Ninataka kukujua. Naomba unisaidie!” Nakumbuka kwamba Mashahidi wa Yehova walinitembelea mara kadhaa, lakini sikuwakaribisha. Sikuiamini dini yoyote.

Mwanzoni mwa miaka ya 1980, dada yangu Lauri, aliyeishi Ufaransa, na Ramoni, aliyeishi Hispania, walianza kujifunza Biblia na Mashahidi. Nilihisi kwamba walikuwa wamedanganywa kama Felisa. Baadaye, nilifahamiana na Angelines, aliyekuwa jirani na rafiki yangu wa karibu. Yeye pia alikuwa Shahidi wa Yehova. Mara kwa mara, Angelines na mume wake waliniomba nijifunze Biblia. Walitambua kwamba ingawa nilikuwa mwenye mashaka mengi, nilitamani kuijua Biblia. Mwishowe, niliwaambia hivi: “Sawa. Lakini nitakubali ikiwa tu nitatumia Biblia yangu,” yaani tafsiri ya Nácar-Colunga.

MWISHOWE BIBLIA YATUUNGANISHA

Felisa: Nilipobatizwa mwaka wa 1973, kulikuwa na Mashahidi 70 hivi huko Santander, jiji kuu la wilaya ya Cantabria, Hispania. Tulikuwa na eneo kubwa, hivyo tulisafiri kwa basi na baadaye kwa gari dogo ili tuhubiri katika wilaya yote. Tulienda kutoka kijiji kimoja kwenda kingine hadi tulipotembelea vijiji vyote katika eneo hilo.

Kwa miaka mingi, nimefurahia kuongoza mafunzo mengi ya Biblia, na 11 kati yao wamebatizwa. Wengi wao walikuwa Wakatoliki. Kwa kuwa zamani nilikuwa na imani kali, nilijua kwamba nilihitaji kuwa mwenye subira na mwenye kuelewa. Nilitambua kuwa walihitaji wakati ili kuachana na imani iliyotia mizizi na kwamba lazima Biblia na roho takatifu ya Yehova iguse mioyo yao ili iwasaidie wajue kweli. (Ebr. 4:12) Mume wangu Bienvenido, aliyekuwa askari, alibatizwa mwaka wa 1979, na mama yangu alianza kujifunza Biblia muda mfupi tu kabla hajafa.

Araceli: Nilikuwa na mashaka sana nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi. Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita nilitambua kwamba chuki yangu ya dini iliisha. Kilichonifurahisha zaidi kuwahusu Mashahidi ni kwamba walitenda kama walivyohubiri. Badala ya kuwa na mashaka, nilijenga imani na nikawa mwenye furaha zaidi. Hata baadhi ya majirani waliniambia hivi: “Araceli, endelea kufanya kile ulichoamua kufanya!”

Nakumbuka nilisali hivi: “Asante Yehova kwa kutokata tamaa ya kunisaidia na kunipa fursa nyingi za kupata nilichokuwa nikitafuta, yaani ujuzi wa kweli wa Biblia.” Nilimwomba msamaha dada yangu Felisa kwa sababu ya kumwambia maneno makali. Mabishano yetu yalibadilika na kuwa mazungumzo ya Biblia yenye kuchangamsha. Nilibatizwa mwaka wa 1989 nikiwa na umri wa miaka 61.

Felisa: Sasa mimi ni mjane mwenye umri wa miaka 91, na sina nguvu kama zamani. Lakini bado ninasoma Biblia kila siku, ninahudhuria mikutano afya yangu inaporuhusu, na ninafurahia kushiriki katika huduma kadiri niwezavyo.

Araceli: Ninapenda kuwahubiria makasisi na watawa wote ninaokutana nao katika huduma; huenda hiyo ni kwa sababu mimi pia nilikuwa mtawa. Nimewaachia machapisho mengi na nimekuwa na mazungumzo mazuri sana pamoja nao. Namkumbuka kasisi mmoja aliyeniambia hivi baada ya kumrudia mara kadhaa: “Araceli, ninakubaliana nawe kabisa, lakini nitaenda wapi nikiwa na umri huu? Waumini wangu na watu wa familia watasemaje?” Nilimjibu hivi: “Na Mungu atasemaje?” Alitikisa kichwa kwa huzuni, lakini wakati huo hakuwa na ujasiri wa kutosha kuendelea kutafuta kweli.

Siku ya pekee ninayokumbuka maishani mwangu ni ile ambayo mume wangu alisema kwa mara ya kwanza kwamba angependa kwenda pamoja nami mkutanoni. Ingawa alikuwa na zaidi ya miaka 80 wakati huo, hakukosa mkutano hata mmoja baada ya hapo. Alijifunza Biblia na akawa mhubiri ambaye hajabatizwa. Ninapata shangwe ninapokumbuka jinsi tulivyofurahia kuhubiri pamoja. Hata hivyo, alikufa miezi miwili kabla ya siku ya kubatizwa.

Felisa: Jambo moja linalonifurahisha sana maishani, ni kuona wadogo zangu wakiwa dada zangu kiroho, ingawa walinipinga sana mwanzoni. Tunafurahi sana kuwa pamoja tunapozungumza kumhusu Mungu wetu, Yehova, na Neno lake! Hatimaye, mimi na wadogo zangu tumeungana kiroho. *

^ fu. 29 Araceli mwenye umri wa miaka 87, Felisa mwenye miaka 91, na Ramoni mwenye miaka 83, wote wanaendelea kumtumikia Yehova kwa bidii mpaka sasa. Lauri alikufa mwaka wa 1990, akiwa mwaminifu kwa Yehova.