Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ushauri wa Biblia Unaweza Kutumika Leo?

Je, Ushauri wa Biblia Unaweza Kutumika Leo?

BAADHI YA WATU HUSEMA HAPANA. Daktari mmoja alisema kwamba kutumia ushauri wa Biblia ni sawa na kutumia kitabu kilichotungwa miaka ya 1920 kufundishia somo la kemia. Mtu anayeidharau Biblia huenda hata akauliza, ‘Je, kweli inawezekana kurejelea kitabu cha mwongozo wa kutumia kompyuta ya kizamani kwa ajili ya kompyuta ya kisasa?’ Kwa maneno mengine, baadhi ya watu huiona Biblia kuwa imepitwa kabisa na wakati.

Kwa nini mtu atumie ushauri wa kitabu cha kale hivyo katika ulimwengu wa sasa uliosonga mbele kiteknolojia? Kwa kuongezea, kila siku maelfu ya tovuti na blogu mbalimbali hutoa ushauri na miongozo ya kisasa zaidi. Vipindi vya mahojiano huandaa ushauri kutoka kwa wanasaikolojia, waandishi wa vitabu, na wataalamu wa mambo mbalimbali maishani. Pia, maduka ya vitabu yamesheheni vitabu vya mashauri kuhusu nyanja mbalimbali za maisha, na uuzaji wa vitabu hivyo ni biashara iliyoshamiri sana leo.

Hivyo basi, kuna haja gani ya kutafuta ushauri wa Biblia, kitabu kilichokamilishwa miaka 2,000 hivi iliyopita, ilhali unaweza kupata ushauri unaotegemea habari za karibuni zaidi? Je, inawezekana kwamba wale wasioamini Biblia wako sahihi wanaposema kuwa kutegemea kitabu hicho cha kale ni sawa na kutumia kitabu cha mwongozo cha kompyuta ya kizamani au kitabu cha kemia kilichopitwa na wakati? Ukweli ni kwamba, njia hiyo ya kufikiri ina kasoro. Sayansi na teknolojia hubadilika haraka sana, lakini je, hali za asili za mwanadamu zimewahi kubadilika? Bado watu wanataka kuwa na maisha yaliyo na kusudi na vilevile kuwa na furaha na usalama, mahusiano mazuri ya familia, na marafiki wanaotegemeka.

Licha ya kuwa kitabu cha kale, Biblia huzungumzia mahitaji hayo na mengine mengi. Pia, inadai kwamba imeongozwa na roho ya Muumba wetu. Inasema inaweza kutuongoza katika kila nyanja ya maisha na kutusaidia kukabiliana na changamoto yoyote ile. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa kuongozea, inadai kuwa ushauri wake hauwezi kamwe kupitwa na wakati! Biblia yenyewe inasema: “Neno la Mungu liko hai.”—Waebrania 4:12.

Je, madai ya Biblia ni ya kweli? Je, imepitwa na wakati, au ni kitabu kilicho hai ambacho kina mashauri bora na yenye kutegemeka zaidi leo? Kusudi la toleo hili la Mnara wa Mlinzi, ambalo ni la kwanza katika mfululizo wa matoleo ya pekee, ni kukusaidia kupata majibu ya maswali hayo.