Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Daudi, mtumishi mwaminifu wa Yehova, aliruhusu mke wake Mikali aweke sanamu ya terafimu kama inavyoonyeshwa kwenye 1 Samweli 19:12, 13?

Kwanza, acheni tuchunguze kwa ufupi muktadha. Mke wa Daudi alichukua hatua mara moja alipopata habari kuhusu njama ya Mfalme Sauli ya kumuua mumewe. Biblia inasema: “Mikali akamteremsha Daudi kupitia dirishani, ili aende, akimbie na kuponyoka. Ndipo Mikali akachukua sanamu ya terafimu [ambayo yaonekana ilikuwa na ukubwa na umbo la mtu] na kuiweka kwenye kitanda, akaweka wavu wa manyoya ya mbuzi penye kichwa chake, kisha akaifunika kwa vazi.” Wajumbe wa Sauli walipokuja kumkamata Daudi, Mikali aliwaambia: “Ni mgonjwa.” Ujanja huo ulimpa Daudi wakati wa kutosha kutoroka.—1 Samweli 19:11-16.

Uvumbuzi wa akiolojia unaonyesha kwamba zamani, sanamu za terafimu ziliwekwa kwa sababu za kidini na pia za kisheria. Zamani, sanamu za terafimu zilitumika sawa na vile hati za kumiliki mali au wosia ulioandikwa unavyotumika leo kuonyesha mtu aliye na haki ya kurithi mali fulani. Yaonekana kwamba chini ya hali fulani, kuwa na terafimu kungempa mwana-mkwe haki ya kudai mali ya baba-mkwe wake aliyekufa. Hiyo huenda ndiyo sababu, katika tukio lingine la awali, Raheli alichukua sanamu za terafimu za babake, na pia ndiyo sababu babake alihangaika sana kuzipata. Wakati huo, Yakobo, mume wa Raheli hakujua mke wake alikuwa amefanya nini.—Mwanzo 31:14-34.

Waisraeli walipofanywa kuwa taifa, walipokea zile Amri Kumi, na ile ya pili hukataza waziwazi kutengeneza sanamu. (Kutoka 20:4, 5) Baadaye, nabii Samweli aligusia sheria hiyo alipozungumza na Mfalme Sauli. Alisema: “Uasi ni sawa na dhambi ya uaguzi, na kwenda kwa kimbelembele ni sawa na kutumia nguvu za uchawi na terafimu.” (1 Samweli 15:23) Kwa sababu hiyo, hailekei kwamba terafimu ilitumiwa katika mambo ya urithi huko Israeli. Hata hivyo, yaonekana familia fulani za Waisraeli ziliendelea kufuata ushirikina huo wa kale wa Kiyahudi. (Waamuzi 17:5, 6; 2 Wafalme 23:24) Kwa kuwa Mikali aliweka terafimu kati ya vitu vyake, hiyo inaonyesha kwamba moyo wake haukuwa kamili kumwelekea Yehova. Ama Daudi hakujua kuhusu sanamu hiyo ya terafimu ama aliivumilia tu kwa sababu Mikali alikuwa binti ya Mfalme Sauli.

Daudi anatoa maoni yake kuhusu kujitoa kikamili kwa Yehova anaposema hivi: “Yehova ni mkuu na wa kusifiwa sana, naye ni wa kuogopwa kuliko miungu mingine yote. Kwa maana miungu yote ya vikundi vya watu ni miungu isiyo na thamani. Lakini Yehova, alizifanya mbingu.”—1 Mambo ya Nyakati 16:25, 26.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Amri ya pili kati ya zile Amri Kumi ilikataza kutengeneza sanamu kama terafimu inayoonyeshwa hapa

[Hisani]

From the book The Holy Land, Vol. II, 1859