Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaamini Kwamba Ibilisi Yuko?

Je, Unaamini Kwamba Ibilisi Yuko?

Je, Unaamini Kwamba Ibilisi Yuko?

MAANDIKO yanaonyesha kwamba Ibilisi ni mtu halisi. Wanadamu hawawezi kumwona Ibilisi kama vile wasivyoweza kumwona Mungu. Biblia inasema kwamba “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Ibilisi ni kiumbe wa roho. Hata hivyo, tofauti na Muumba, Ibilisi ana mwanzo.

Mapema kabla ya kuwaumba wanadamu, Yehova Mungu aliumba viumbe wengi wa roho. (Ayubu 38:4, 7) Biblia huwaita roho hao malaika. (Waebrania 1:13, 14) Mungu aliwaumba wote wakiwa wakamilifu—hakuna aliyekuwa ibilisi au aliyekuwa na sifa mbaya. Basi, Ibilisi alitoka wapi? Neno “ibilisi” linamaanisha “mchongezi” nalo linarejelea mtu anayesema uwongo mwovu kuhusu watu wengine. Neno “Shetani” linamaanisha “Mshindani,” au mpinzani. Kama vile mtu aliyekuwa mnyoofu hapo awali anavyojifanya mwenyewe kuwa mwizi kwa kuiba, ndivyo na mmoja wa wana wakamilifu wa roho wa Mungu alivyositawisha tamaa mbaya na kujifanya mwenyewe kuwa Shetani Ibilisi. Biblia inaeleza kwa njia ifuatayo hatua zinazoongoza kwenye upotovu: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.”—Yakobo 1:14, 15.

Yaonekana hivyo ndivyo mambo yalivyotukia. Yehova Mungu alipowaumba wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, malaika huyo ambaye alikuwa karibu kumwasi Mungu alikuwa akichunguza hilo kwa makini. Alijua kwamba Yehova aliwaamuru Adamu na Hawa waijaze dunia na wanadamu waadilifu ambao wangemwabudu Muumba. (Mwanzo 1:28) Malaika huyo alitambua kwamba ingewezekana yeye kupata heshima na umashuhuri huo. Akichochewa na pupa, alitamani sana kupata kile ambacho ni haki ya Muumba pekee, yaani, ibada kutoka kwa wanadamu. Badala ya kutupilia mbali tamaa hiyo isiyofaa, malaika huyo aliisitawisha hadi ikazaa uwongo na baadaye ikamwongoza kuasi. Ona yale aliyofanya.

Malaika huyo mwasi alitumia nyoka kuzungumza na mwanamke wa kwanza, Hawa. Nyoka huyo alimuuliza Hawa hivi: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Hawa alipotaja amri ya Mungu na adhabu ambayo ingetokana na kutoitii, nyoka alisema hivi: “Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda [ya ule mti ulio katikati ya bustani] macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:1-5) Alidai kwamba Mungu hakuwaambia Adamu na Hawa ukweli. Alidai kwamba ikiwa Hawa angekula matunda ya mti huo, angekuwa kama Mungu, akiwa na haki ya kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya. Huo ndio uliokuwa uwongo wa kwanza kabisa. Uwongo huo ulimfanya malaika huyo awe mchongezi, na akawa pia mpinzani wa Mungu. Hivyo, Biblia inamtambulisha adui huyo wa Mungu kuwa “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani.”—Ufunuo 12:9.

“Iweni Wenye Kulinda”

Uwongo ambao Ibilisi alimwambia Hawa ulifanikiwa tu kama alivyokusudia. Biblia inasema hivi: “Basi mwanamke akaona kwamba mti huo ulikuwa mzuri kwa chakula na kwamba ulikuwa kitu cha kutamanika kwa macho, ndiyo, mti huo ulikuwa wenye kupendeza kuutazama. Kwa hiyo akaanza kuchukua kati ya matunda yake akala. Baadaye akampa mume wake pia alipokuwa pamoja naye, naye akaanza kula.” (Mwanzo 3:6) Hawa alimwamini Shetani na akamwasi Mungu. Hawa aliweza kumshawishi Adamu avunje pia sheria ya Mungu. Hivyo, Ibilisi akafaulu kuwafanya wanadamu wa kwanza wamwasi Mungu. Tangu wakati huo, Shetani amekuwa na uvutano juu ya wanadamu bila kuonekana. Ana kusudi gani? Kusudi lake ni kuwafanya watu wasimwabudu Mungu wa kweli na kuwafanya wamwabudu yeye. (Mathayo 4:8, 9) Ni kwa sababu hiyo Maandiko yanatuonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.”—1 Petro 5:8.

Hivyo, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Ibilisi ni kiumbe halisi wa roho, yaani, malaika ambaye alipotoka na aliye hatari! Hatua ya kwanza kabisa ya kutusaidia kuwa wenye kulinda ni kutambua kwamba Ibilisi yuko. Hata hivyo, kutunza akili zetu na kuwa wenye kulinda kunahusisha mambo mengi zaidi. Ni muhimu pia kujua “mbinu” na njia ambazo Shetani hutumia ili kuwadanganya watu. (2 Wakorintho 2:11) Mbinu zake ni zipi? Nasi tunaweza kuzipingaje?

Ibilisi Hulenga Uhitaji wa Kiasili wa Mwanadamu

Ibilisi amewachunguza wanadamu tangu walipoumbwa. Anajua jinsi walivyo, yaani, mahitaji yao, mapendezi yao, na tamaa zao. Shetani anajua vema kwamba mwanadamu aliumbwa akiwa na uhitaji wa kiroho, na Ibilisi ametumia kwa werevu uhitaji huo. Jinsi gani? Kwa kuwafundisha wanadamu uwongo wa kidini. (Yohana 8:44) Mafundisho mengi ya kidini kumhusu Mungu yanapingana na ni yenye kuvuruga. Unafikiri yanatimiza kusudi la nani? Mafundisho yanayopingana hayawezi kuwa ya kweli. Basi, je, inawezekana kwamba mafundisho ya kidini yanakusudiwa na kutumiwa na Shetani hasa ili kuwadanganya watu? Kwa kweli, Biblia inamtaja Shetani kuwa “mungu wa mfumo huu wa mambo,” ambaye amepofusha akili za watu.—2 Wakorintho 4:4.

Mafundisho ya kweli humlinda mtu kutokana na uwongo wa kidini. Biblia hufananisha kweli ya Neno la Mungu na mshipi ambao askari-jeshi wa zamani alivaa ili kulinda kiuno chake. (Waefeso 6:14) Ukipata ujuzi wa Biblia na kuishi kulingana nao, kana kwamba unajifunga ujuzi huo kama mshipi, Neno la Mungu litakulinda ili usipotoshwe na uwongo na makosa ya kidini.

Tamaa ya wanadamu ya kuabudu imewafanya wachunguze mambo yasiyojulikana. Hilo limewafanya wanaswe na mbinu nyingine yenye udanganyifu ya Shetani. Akitumia tamaa ya mwanadamu ya kupenda kujua mambo yasiyo ya kawaida na ya mafumbo, Shetani amewatawala watu wengi kwa kuwafanya wawasiliane na pepo. Kama vile mwindaji hutumia chambo ili kunasa windo lake, Shetani hutumia mbinu kama kubashiri, unajimu, kupumbaza akili, uchawi, usomaji wa viganja, na mizungu ili kuwavuta na kuwanasa watu kotekote ulimwenguni.—Mambo ya Walawi 19:31; Zaburi 119:110.

Unaweza kujilindaje ili usinaswe katika mtego wa kuwasiliana na pepo? Andiko la Kumbukumbu la Torati 18:10-12 linasema hivi: “Asipatikane ndani yako yeyote anayempitisha mwana wake au binti yake katikati ya moto, yeyote anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi, au anayefunga wengine kwa kuwatakia maovu au yeyote anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au mjuzi wa kubashiri matukio au yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova, na kwa sababu ya machukizo hayo, Yehova Mungu wako anawafukuza kutoka mbele yako.”

Shauri la Kimaandiko liko wazi: Kataa kabisa kuwasiliana na pepo. Namna gani ikiwa umewahi kujihusisha katika aina yoyote ya kuwasiliana na pepo na sasa unataka kuacha zoea hilo? Unaweza kufuata mfano wa Wakristo wa mapema wa jiji la Efeso. Walipolikubali “neno la Yehova,” Biblia inasema kwamba ‘hesabu kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa uchawi walileta pamoja vitabu vyao wakaviteketeza mbele ya kila mtu.’ Vitabu hivyo vilikuwa vya bei ghali. Vilikuwa na thamani ya vipande 50,000 vya fedha. (Matendo 19:19, 20) Hata hivyo, Wakristo huko Efeso hawakusita kuviharibu.

Shetani Hutumia Udhaifu wa Wanadamu

Malaika mkamilifu aligeuka kuwa Shetani Ibilisi kwa sababu alijiruhusu ashindwe na tamaa ya kujitukuza. Pia, alimfanya Hawa awe na kiburi na ubinafsi ambao ulimfanya atamani kuwa kama Mungu. Leo, Shetani anatawala watu wengi kwa kuwafanya wawe na kiburi. Kwa mfano, watu wengine huhisi kwamba jamii yao, kabila lao, au taifa lao ni bora kuliko la wengine. Hiyo ni kinyume kabisa na mafundisho ya Biblia! (Matendo 10:34, 35) Biblia inasema waziwazi hivi: “[Mungu] alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.”—Matendo 17:26.

Kuwa mnyenyekevu ni njia bora ya kupinga jitihada za Shetani za kuwafanya watu wawe na kiburi. Biblia inatushauri ‘tusijifikirie wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’ (Waroma 12:3) Inasema hivi: “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.” (Yakobo 4:6) Njia bora ya kupinga jitihada za Shetani ni kuwa mnyenyekevu na kuonyesha sifa nyingine ambazo zinakubaliwa na Mungu.

Ibilisi anafurahia pia kutumia udhaifu mwingine wa wanadamu, yaani, kujiruhusu tushindwe na tamaa zisizofaa za mwili. Yehova Mungu alikusudia wanadamu wafurahie maisha. Tamaa zinapotoshelezwa kupatana na mapenzi ya Mungu, hilo huleta furaha ya kweli. Lakini Shetani huwachochea wanadamu kutosheleza tamaa zao katika njia zilizopotoka kiadili. (1 Wakorintho 6:9, 10) Ni vizuri zaidi kufikiria mambo mema na yaliyo safi kiadili. (Wafilipi 4:8) Hilo litakusaidia kuyadhibiti mawazo na hisia zako.

Endelea Kumpinga Ibilisi

Je, unaweza kumpinga Ibilisi? Ndiyo, unaweza. Biblia inatupa uhakikisho huu: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Yakobo 4:7) Hata ukimpinga Shetani, hataacha kukusumbua mara moja bali ataendelea kukuzuia usijifunze juu ya Mungu. Ibilisi atajaribu tena “wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Hata hivyo, hupaswi kumwogopa Ibilisi. Ukiendelea kumpinga, hataweza kukugeuza mbali na Mungu wa kweli.

Hivyo, ili kumpinga Ibilisi unahitaji kumjua na kujua jinsi anavyowadanganya watu na pia hatua unazohitaji kuchukua ili kujilinda na mbinu zake. Neno la Mungu, Biblia, ndicho chanzo sahihi tu cha ujuzi huo. Hivyo, uwe thabiti katika azimio lako la kujifunza Maandiko yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu, na utumie maishani mwako mambo unayojifunza. Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia bila malipo kujifunza Biblia kwa wakati unaokufaa. Tafadhali usisite kukutana nao au kuwaandikia wachapishaji wa gazeti hili.

Unapoanza kujifunza Biblia, unahitaji kujua kwamba Shetani anaweza kutumia upinzani au mateso ili kukufanya uache kujifunza kweli kutoka katika Neno la Mungu. Huenda baadhi ya wapendwa wako watakasirika kwa sababu unajifunza Biblia. Huenda wakafanya hivyo kwa sababu hawajui kweli za ajabu zilizomo katika Biblia. Huenda hata wengine wakakudhihaki. Lakini je, Mungu atafurahi ukishindwa na mikazo hiyo? Ibilisi anataka kukuvunja moyo ili uache kujifunza juu ya Mungu wa kweli. Usimruhusu Shetani ashinde. (Mathayo 10:34-39) Huna deni lake. Una deni kwa Yehova kwa sababu amekupa uhai. Hivyo basi, azimia kumpinga Ibilisi na ‘kuufanya moyo wa Yehova ushangilie.’—Methali 27:11.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Wale waliogeuka kuwa Wakristo waliteketeza vitabu vyao vya kuwasiliana na pepo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Fanya uamuzi thabiti wa kujifunza Biblia