Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kuvuka na Kuingia Makedonia?

Je, Unaweza Kuvuka na Kuingia Makedonia?

Je, Unaweza Kuvuka na Kuingia Makedonia?

ALIPOKUWA kwenye jiji lenye bandari la Troa huko Asia Ndogo, mtume Paulo alipata maono. Mwanamume Mmakedonia alimsihi hivi: “Vuka uingie Makedonia utusaidie.” Mara tu Paulo alipoona maono hayo, yeye pamoja na wale aliokuwa akisafiri nao walikata ‘kauli kwamba Mungu alikuwa amewaita wawatangazie watu wa Makedonia habari njema.’ Walipata matokeo gani? Huko Filipi, mji mkuu wa Makedonia, Lidia pamoja na familia yake wakawa waamini. Watu wengine katika jimbo hilo la Roma la Makedonia walikuja kuwa waamini pia.—Mdo. 16:9-15.

Leo, Mashahidi wa Yehova wanaonyesha roho hiyohiyo ya bidii. Bila kulazimishwa na kwa gharama yao wenyewe, wengi wamehamia maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Kwa mfano, Lisa alitaka kukazia fikira zaidi huduma katika maisha yake. Alitoka Kanada na kuhamia Kenya. Trevor na Emily ambao pia wanatoka Kanada, walienda Malawi wakiwa na mradi wa kupanua utumishi wao. Paul na Maggie, kutoka Uingereza, waliona kwamba baada ya kustaafu walikuwa na nafasi nzuri sana ya kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova wakahamia Afrika Mashariki. Je, una roho ya kujidhabihu? Je, unaweza kufikiria kuhamia eneo lenye uhitaji? Ikiwa ndivyo, ni kanuni gani za Biblia na mapendekezo gani yanayofaa yanayoweza kukusaidia ufanikiwe?

Jichunguze

Jambo moja ambalo unapaswa kufikiria ni nia yako. Yesu alisema kwamba amri kuu ni: “Umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” Sababu ya kutumika katika nchi ya kigeni inapaswa kuwa upendo kwa Mungu na tamaa ya kutimiza agizo la kufanya wanafunzi. Yesu aliendelea kusema: “Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’” Tunaonyesha kwamba tunampenda jirani tunapotamani kusaidia kutoka moyoni. (Mt. 22:36-39; 28:19, 20) Kwa kawaida, ili mtu atumike katika nchi ya kigeni anahitaji kujidhabihu na kuwa tayari kufanya kazi nyingi. Si safari ya kusisimua tu. Ni lazima uchochewe na upendo. Remco na Suzanne kutoka Uholanzi, ambao sasa wanatumika huko Namibia, wanaeleza jambo hilo hivi: “Upendo ndio unaotufanya tuendelee kuwa huku.”

Willie ambaye ni mwangalizi wa mzunguko huko Namibia anasema hivi: “Wale ambao wamebaki katika eneo la kigeni hawakuja wakitazamia kwamba ndugu wenyeji watawatunza. Walikuja wakiwa na kusudi la kutumika pamoja na ndugu wenyeji, na kuwasaidia katika kazi ya kuhubiri.”

Baada ya kuchunguza nia yako, jiulize hivi: ‘Nina ujuzi gani ambao unaweza kufaa katika eneo la kigeni? Je, mimi ni mhudumu mwenye matokeo? Ninazungumza lugha gani mbalimbali? Je, niko tayari kujifunza lugha nyingine?’ Zungumzia jambo hilo kwa undani pamoja na watu wa familia yako. Zungumza na wazee katika kutaniko lenu. Na bila shaka usali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Kujichunguza kibinafsi kwa njia hiyo kunapaswa kukusaidia uone ikiwa kwa kweli unaweza na umeazimia kutumika katika eneo la kigeni.—Ona sanduku  “Jua Hali Zako.”

Mahali pa Kutumika

Paulo aliombwa aende Makedonia katika maono. Leo, Yehova hatumii uwezo unaopita nguvu za mwanadamu kutuongoza. Hata hivyo, kupitia gazeti hili na vichapo vingine, watu wa Mungu wametambua maeneo mengi yaliyo na uhitaji mkubwa. Hivyo, anza kwa kuandika orodha ya maeneo hayo. Ikiwa hutaki kujifunza lugha mpya au hutakaa katika nchi ya kigeni kwa muda mrefu, fikiria kutumika katika nchi ambayo inatumia lugha unayozungumza kwa sasa. Kisha chunguza mambo kama vile masharti ya kupata viza, usafiri, usalama, gharama za kawaida za maisha, na hali ya hewa. Huenda ukafaidika kwa kuzungumza na wale ambao tayari wamechukua hatua hiyo. Sali kuhusu mambo hayo. Kumbuka kwamba Paulo na wenzake walikuwa ‘wamekatazwa na roho takatifu wasiseme lile neno katika wilaya ya Asia.’ Ingawa walijaribu kuingia Bithinia, “roho ya Yesu haikuwaruhusu” kufanya hivyo. Vivyo hivyo, huenda ikachukua muda kuamua mahali ambapo unaweza kusaidia zaidi.—Mdo. 16:6-10.

Kufikia sasa, huenda umefikiria kuhusu maeneo fulani. Ikiwa unafikiria kutumika katika nchi ya kigeni, andikia ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova katika nchi ambazo ungependa kutumika. Eleza kuhusu hali yako ya kiroho na uulize pia maswali yoyote hususa ambayo huenda unayo, kama vile kuhusu gharama za maisha, mahali pa kuishi, huduma za afya ambazo zinapatikana, na nafasi za kupata kazi. Kisha peleka barua yako au barua zako kwa halmashauri ya utumishi ya kutaniko lenu. Wataambatanisha barua zako pamoja na barua yao ya kukupendekeza kisha watazituma moja kwa moja kwenye ofisi za tawi ulizoonyesha. Majibu ya barua hizo yatakusaidia kuamua mahali ambapo unaweza kutumika vizuri zaidi.

Willie, aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Kwa kawaida, wale ambao wamefanya vizuri walitembelea nchi hiyo kwanza na wakatafuta mahali ambapo kwa kweli wangeishi kwa furaha. Wenzi fulani wa ndoa waliona kwamba ingekuwa vigumu kwao kuishi katika eneo la mashambani. Hivyo, waliamua kuishi katika mji mmoja mdogo ambao ulikuwa na uhitaji lakini ambako wangeweza kuishi maisha ambayo yangewafanya wawe na furaha.”

Kukabiliana na Matatizo Mapya

Bila shaka, unapohama nyumbani na kwenda katika mazingira mapya kabisa utakabili matatizo fulani. Lisa, aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Inaweza kuwa vigumu sana kukabiliana na hisia za upweke.” Ni nini ambacho kinamsaidia? Ni kukaa karibu na kutaniko la eneo ambalo anaishi. Aliweka mradi wa kujua jina la kila mtu kutanikoni. Ili atimize mradi huo, alifika mapema mikutanoni na kubaki baada ya mikutano ili azungumze na ndugu na dada. Lisa alihubiri pamoja na wengine, akaalika wengi nyumbani kwake, naye akapata marafiki wapya. Anasema hivi: “Sijuti kamwe kwa sababu ya kujidhabihu. Kwa kweli, Yehova amenibariki.”

Baada ya kuwalea watoto wao, Paul na Maggie walihama kutoka nyumba ambayo walikuwa wameishi kwa miaka 30. Paul anasema hivi: “Ilikuwa rahisi kuacha vitu vya kimwili kuliko tulivyotarajia. Jambo gumu zaidi lilikuwa ni kuacha familia, ilikuwa vigumu zaidi ya vile tulivyotarajia. Tulilia sana tulipokuwa katika ndege. Ni rahisi kujiambia kwamba, ‘Hatuwezi kamwe kufaulu.’ Lakini tulimtegemea Yehova. Ukipata marafiki wapya unaazimia zaidi kusonga mbele.”

Greg na Crystal waliamua kuhama Kanada na kwenda Namibia kwa sababu walizungumza Kiingereza, lugha rasmi ya Namibia. Hata hivyo, baadaye waliona kwamba ingefaa sana kujifunza angalau lugha moja ya kienyeji. “Nyakati fulani, tulivunjika moyo. Ni baada ya kujifunza lugha ya kienyeji ndipo tulipoelewa utamaduni wa nchi hiyo. Kushirikiana kwa ukaribu na ndugu wenyeji kulitusaidia kuzoea mazingira yetu mapya.”

Mtazamo huo wa unyenyekevu na utayari wa kutumika unaweza kuwa na matokeo mazuri kwa ndugu wenyeji vilevile. Jenny, anafurahi anapokumbuka familia ambazo zilihamia Ireland, ambako alilelewa. Anasema hivi: “Walikuwa wakaribishaji-wageni. Kwa kweli walikuja kutumika, si kutumikiwa. Walikuwa na bidii sana na wenye furaha hivi kwamba mimi pia nikaamua kuhamia eneo lenye uhitaji.” Sasa, Jenny na mume wake wanatumika wakiwa Wamishonari huko Gambia.

Baraka ya Yehova “Hutajirisha”

Huduma ya Paulo huko Makedonia ilikuwa na matokeo mazuri sana! Karibu miaka kumi baadaye, aliwaandikia hivi ndugu wa Filipi: “Namshukuru Mungu wangu sikuzote kila mara ninapowakumbuka ninyi.”—Flp. 1:3.

Trevor na Emily, ambao walitumika huko Malawi kabla ya kualikwa kwenye Shule ya Gileadi wanahisi hivyo pia. “Nyakati nyingine tulijiuliza ikiwa tulikuwa tunafanya jambo linalofaa, lakini tulikuwa na furaha. Tulikuwa na uhusiano wa karibu kati yetu na tuliona baraka ya Yehova.” Greg na Crystal, ambao walitajwa mwanzoni, wanasema, “Hakuna jambo bora zaidi kuliko lile tunalofanya sasa.”

Kwa kweli, si kila mtu anaweza kutumika katika nchi ya kigeni. Huenda ikafaa wengine wahamie eneo lenye uhitaji zaidi katika nchi yao. Wengine wanaweza kujiwekea mradi wa kutumika katika makutaniko yaliyo karibu na eneo lao. Jambo la maana ni kufanya yote ambayo unaweza katika kumtumikia Yehova. (Kol. 3:23) Ukifanya hivyo, utaona ukweli wa maneno haya ambayo yameongozwa na roho ya Mungu: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Met. 10:22.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

 Jua Hali Zako

Ili ujichunguze na kutambua ikiwa unaweza kutumika katika eneo la kigeni, fikiria maswali yafuatayo na uchanganue kwa unyoofu na kupitia sala ikiwa kwa kweli unaweza kuhamia eneo lenye uhitaji. Habari zinazopatikana katika matoleo ya zamani ya Mnara wa Mlinzi zinaweza kukusaidia kufanya hivyo.

• Je, mimi ni mtu wa kiroho?—“Hatua Kuelekea Furaha” (Oktoba 15, 1997 [15/10/1997], ukurasa wa 6)

• Je, mimi ni mhudumu mwenye matokeo?—“Jinsi ya Kufaulu Katika Huduma ya Painia” (Mei 15, 1989 [15/5/1989], ukurasa wa 21)

• Je, ninaweza kuishi mbali na familia na marafiki?—“Kukabiliana na Tatizo la Kutamani Nyumbani Katika Utumishi wa Mungu” (Mei 15, 1994, ukurasa wa 28)

• Je, ninaweza kujifunza lugha mpya?—“Kutumika Katika Kutaniko la Lugha ya Kigeni” (Machi 15, 2006 [15/3/2006], ukurasa wa 17)

• Je, nina fedha za kunitegemeza katika eneo la kigeni?—“Je, Unaweza Kutumikia Katika Eneo la Kigeni?” (Oktoba 15, 1999, ukurasa wa 23)

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mtazamo wa unyenyekevu na utayari wa kutumika unaweza kuwa na matokeo mazuri kwa ndugu wenyeji

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wale wanaojitoa ili kutumika ndio wanaofanikiwa