Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuvumilia Majaribu Kulitusaidia Kumtegemea Yehova Zaidi

Kuvumilia Majaribu Kulitusaidia Kumtegemea Yehova Zaidi

Kuvumilia Majaribu Kulitusaidia Kumtegemea Yehova Zaidi

Limesimuliwa na Ada Dello Stritto

Nilikuwa nimemaliza tu kuandika andiko la siku katika kijitabu changu. Nina umri wa miaka 36, lakini nilitumia muda wa saa mbili kuandika maneno hayo machache. Kwa nini nilitumia muda mrefu hivyo? Mama yangu ataeleza sababu.—Joel

MIMI na mume wangu tulibatizwa mwaka wa 1968 na kuwa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kujifungua watoto wawili wa kiume wenye afya nzuri, David na Marc, nilijifungua mwana wetu wa tatu, Joel. Alizaliwa mwaka wa 1973, kabla ya mimba kufika miezi tisa, kwenye hospitali moja katika mji wa Binche huko Ubelgiji, umbali wa kilomita 60 hivi upande wa kusini wa Brussels. Alikuwa na uzito wa kilogramu 1.7 tu. Nilipotoka hospitalini, Joel alibaki hospitalini ili uzito wake uongezeke.

Baada ya majuma machache hali ya mwana wetu haikuwa imebadilika, kwa hiyo, mimi na mume wangu, Luigi, tulimpeleka kwa daktari wa magonjwa ya watoto. Baada ya kumchunguza Joel, daktari huyo alisema hivi: “Poleni sana. Inaonekana kwamba Joel ana matatizo yote ambayo ndugu zake hawana.” Sisi sote tukanyamaza kwa muda mrefu. Wakati huo, nilitambua kwamba mwana wetu mdogo alikuwa na tatizo kubwa sana la kiafya. Halafu daktari akamwita mume wangu kando na kumwambia hivi: “Mtoto wenu ana ugonjwa wa trisomy 21 (au trisomie 21),” ambao pia unaitwa Down syndrome. *

Tulihuzunishwa sana na ripoti ya daktari huyo, tukaamua kumwona mtaalamu mwingine wa matibabu. Alimchunguza kwa uangalifu mtoto wetu Joel kwa karibu saa nzima bila kusema neno lolote. Mimi na Luigi tuliona muda huo kuwa mrefu kupita kiasi. Mwishowe, daktari huyo alitutazama na kusema, “Mtoto wenu atawategemea sana.” Kisha, akaongezea hivi kwa sauti yenye fadhili, “Lakini Joel atakuwa na furaha kwa sababu wazazi wake wanampenda!” Niliguswa moyo sana hivi kwamba nilimbeba Joel kwa uangalifu, tukarudi nyumbani. Wakati huo alikuwa na umri wa majuma manane.

Tulitiwa Nguvu na Huduma na Mikutano ya Kikristo

Uchunguzi wa madaktari ulionyesha kwamba Joel alikuwa pia na kasoro kubwa sana ya moyo na alikuwa na ugonjwa mbaya wa miguu (nyongea au matege). Kwa kuwa moyo wake ulikuwa mkubwa sana, ulifinya mapafu yake na hivyo alikabili hatari ya kuambukizwa magonjwa. Muda si muda, alipokuwa na umri wa miezi minne, Joel alipata ugonjwa wa nimonia na tukalazimika kumrudisha hospitalini ambamo alitengwa na wagonjwa wengine. Tuliumia sana kumwona akiteseka. Tulitamani kumbeba na kumpapasa, lakini kwa majuma kumi yenye kufadhaisha, hatukuruhusiwa kamwe kumgusa. Mimi na Luigi tulimtazama tu, tukakumbatiana, na kusali.

Wakati huo, tuliendelea kuhudhuria mikutano ya kutaniko pamoja na David, aliyekuwa na umri wa miaka 6 na Marc, ambaye alikuwa na umri wa miaka 3. Tulipokuwa kwenye Jumba la Ufalme tulihisi ni kana kwamba tulikuwa tumebebwa na mikono ya Yehova yenye kujali. Kila wakati tulipokuwa kwenye Jumba la Ufalme, tukiwa tumezungukwa na ndugu na dada zetu Wakristo, tulihisi kwamba tumemtupia Yehova mzigo wetu, na tulipata utulivu moyoni. (Zab. 55:22) Hata wauguzi waliomtunza Joel walisema kwamba waliona jinsi kuhudhuria mikutano ya Kikristo kulivyotusaidia kuwa na usawaziko.

Wakati huo, nilimsihi Yehova anipe pia nguvu za kwenda katika utumishi wa shambani. Badala ya kukaa nyumbani na kulia, nilitaka kuzungumza na wengine na kuwaambia kwa nini kutegemea ahadi ya Mungu ya kuleta ulimwengu usio na magonjwa kulinitia nguvu. Kila mara niliposhiriki katika huduma, nilihisi kwamba Yehova alijibu sala zangu.

“Hili Ni Jambo la Ajabu!”

Mwishowe, tulifurahi sana siku ambayo tuliruhusiwa kumpeleka Joel nyumbani! Lakini siku iliyofuata, shangwe yetu iligeuka na kuwa huzuni. Hali ya Joel ilibadilika mara moja na kuwa mbaya zaidi, tukalazimika kumpeleka haraka katika hospitali. Madaktari walituambia hivi baada ya kumchunguza: “Joel ataishi kwa miezi sita tu.” Baada ya miezi miwili, alipokuwa na umri wa miezi minane hivi, maneno ya madaktari yalionekana kuwa ya kweli kwa sababu hali ya Joel ilizidi kuwa mbaya. Daktari mmoja aliketi pamoja nasi na kutuambia hivi: “Ninasikitika sana. Hatuwezi kumsaidia kwa njia nyingine yoyote.” Kisha akaongezea hivi: “Kwa sasa, ni Yehova tu anayeweza kumsaidia.”

Nilirudi kwenye chumba cha hospitali ambamo Joel alikuwa amelazwa. Hata ingawa nilikuwa nimechoka sana kimwili na kufadhaika kihisia, niliazimia kutoondoka karibu na kitanda chake. Dada fulani Wakristo walikuwa na zamu ya kukaa pamoja na mimi huku Luigi akiwatunza wana wetu wawili wakubwa. Juma moja lilipita. Kisha kwa ghafula, Joel akapata mshtuko wa moyo. Wauguzi waliingia haraka kwenye chumba chake lakini hawangeweza kumwokoa. Baada ya dakika fulani kupita, mmoja wao alisema hivi kwa upole, “Mambo kwisha . . . ” Nilianza kulia na kuondoka katika chumba hicho huku nikiwa nimechoka kabisa. Nilijaribu kusali kwa Yehova, lakini nilishindwa kabisa kueleza uchungu wangu. Baada ya dakika 15 hivi kupita, muuguzi mmoja aliniambia hivi kwa sauti, “Joel anapata nafuu!” Akanishika mkono na kuniambia, “Njoo, unaweza kumwona sasa.” Nilipofika alipokuwa Joel, moyo wake ulikuwa umeanza kupiga tena! Habari hizo zilienea haraka sana. Wauguzi na madaktari walikuja kumwona, na wengi wao wakasema hivi kwa mshangao: “Hili ni jambo la ajabu!”

Apiga Hatua Kubwa Akiwa na Umri wa Miaka Minne

Katika miaka ya kwanza ya maisha ya Joel, daktari wa watoto alituambia tena na tena kwamba “Joel anahitaji upendo mwingi.” Kwa kuwa Yehova alikuwa amenitunza mimi na Luigi kwa upendo sana baada ya kujifungua Joel, tulitaka kumtunza kabisa mtoto wetu kwa upendo pia. Tulikuwa na nafasi nyingi za kufanya hivyo kwa sababu alihitaji msaada wetu katika kila jambo.

Kila mwaka kwa muda wa miaka saba ya kwanza ya maisha ya Joel, tulifuata utaratibu uleule. Kati ya Oktoba na Machi (Mwezi wa 3), alipata tatizo moja la afya baada ya lingine, na kila mara tulilazimika kumpeleka hospitalini. Wakati huohuo, nilijitahidi kadiri nilivyoweza kutumia wakati mwingi kuwatunza watoto wengine wetu David na Marc. Nao pia walishiriki sana kumsaidia Joel kufanya maendeleo, na matokeo yalikuwa mazuri ajabu. Kwa mfano, madaktari wengi walituambia kwamba Joel hangeweza kutembea kamwe. Lakini siku moja Joel alipokuwa na umri wa miaka minne, mwana wetu Marc alisema, “Njoo Joel, mwonyeshe Mama kwamba unaweza kutembea!” Nilishangaa sana kumwona Joel akianza kutembea! Tulifurahi sana, tukasali pamoja tukiwa familia na kumshukuru Yehova kutoka moyoni. Nyakati nyingine, hata Joel alipofanya maendeleo madogo sana katika mambo fulani, tulimpongeza sana.

Jitihada za Kumfundisha Joel Kumhusu Mungu Tangu Utotoni Zinafanikiwa

Tulienda na Joel kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme mara nyingi iwezekanavyo. Ili kumlinda asiambukizwe magonjwa kwa urahisi, tulimbeba ndani ya kigari cha pekee cha watoto ambacho kilikuwa kimefunikwa na karatasi ya plastiki. Hata hivyo, alifurahi kushirikiana na kutaniko ingawa aliketi ndani ya kigari hicho.

Ndugu na dada zetu Wakristo walitutia moyo sana, walituonyesha upendo na kutusaidia tulipohitaji msaada. Ndugu mmoja alitukumbusha mara nyingi maneno ya Isaya 59:1: “Tazama! Mkono wa Yehova haujawa mfupi mno kwamba usiweze kuokoa, wala sikio lake halijawa zito mno kwamba lisiweze kusikia.” Maneno hayo yenye kutia moyo yalitusaidia kumtegemea Yehova.

Joel alipoendelea kukua, tulijitahidi kumsaidia atangulize utumishi wa Yehova katika maisha yake. Katika kila nafasi, tulizungumza na Joel kumhusu Yehova na kumsaidia asitawishe uhusiano wenye upendo na Baba yake wa mbinguni. Tulimsihi Yehova abariki jitihada zetu za kumfundisha Joel njia ya Mungu.

Alipofikia miaka ya mapema ya ujana, tulifurahi sana kuona kwamba Joel alipenda kuzungumza na watu aliokutana nao kuhusu kweli za Biblia. Nilifurahi sana Joel aliponiuliza hivi alipokuwa akipata nafuu baada ya kufanyiwa upasuaji mkubwa akiwa na umri wa miaka 14: “Mama, ninaweza kumpa daktari-mpasuaji kitabu Kuishi Milele?” Baada ya miaka michache kupita, Joel alihitaji kufanyiwa upasuaji mwingine. Tulijua vizuri kwamba huenda angekufa. Kabla ya upasuaji, Joel aliwapa madaktari wake barua ambayo tulikuwa tumeandika tukiwa pamoja naye. Ilieleza msimamo wake kuhusu matumizi ya damu. Daktari-mpasuaji alimuuliza Joel, “Je, unakubaliana nayo?” Joel akamjibu kwa uthabiti, “Ndiyo, Daktari.” Tulifurahi sana kuona mwana wetu akimtegemea Muumba wake na kuona akiwa ameazimia kumpendeza. Wafanyakazi wa hospitali walitusaidia sana, na tulithamini kabisa msaada wao.

Maendeleo ya Kiroho ya Joel

Joel alibatizwa katika maji akiwa na umri wa miaka 17 ili kuonyesha wakfu wake kwa Mungu. Hatutasahau kamwe siku hiyo! Tunapata shangwe nyingi sana tunapoona maendeleo yake ya kiroho. Tangu wakati huo, hajapunguza upendo wake kwa Yehova na bidii yake kwa ajili ya kweli. Kwa kweli, Joel anapenda kumwambia hivi kila mtu anayekutana naye: “Kweli ni njia yangu ya maisha!”

Katika miaka ya mwisho ya ujana, Joel alijifunza kusoma na kuandika. Alijitahidi sana kufanya hivyo. Alipofaulu kuandika neno moja dogo tu, tuliona kuwa amepiga hatua kubwa sana. Tangu hapo, anaanza kila siku kwa kuchunguza andiko la siku akitumia kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Kisha, anaandika andiko hilo katika moja ya vijitabu vyake hata ingawa si rahisi kufanya hivyo. Anahifadhi habari hizo katika vitabu vyake vyenye kuvutia!

Siku za mikutano, Joel anahakikisha kwamba tunaenda kwenye Jumba la Ufalme mapema kwa sababu anataka kufika kwa wakati ili awakaribishe kwa uchangamfu wote wanaofika. Wakati wa mikutano, anafurahia kutoa maelezo na kushiriki katika maonyesho. Pia, anasaidia katika kushughulikia vikuza-sauti na kufanya kazi nyingine. Kila juma, afya yake inaporuhusu, anaenda kuhubiri pamoja nasi. Mwaka wa 2007, kutaniko lilitangaziwa kwamba Joel amewekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma. Tulitokwa na machozi ya shangwe. Hiyo ni baraka yenye upendo kama nini kutoka kwa Yehova!

Tunaona Jinsi Yehova Anavyotusaidia

Tulipata jaribu lingine mwaka wa 1999. Gari letu liligongwa na gari lingine lililokuwa likiendeshwa vibaya, na Luigi akaumia sana. Mguu wake mmoja ulihitaji kukatwa, na akafanyiwa upasuaji mkubwa wa uti wa mgongo mara kadhaa. Kwa mara nyingine tena, tulimtegemea Yehova tukapata nguvu ambazo anawapa watumishi wake. (Flp. 4:13) Ingawa Luigi angali mlemavu, tunajitahidi kukazia fikira baraka zetu. Kwa kuwa hawezi kufanya kazi, ana wakati mwingi zaidi wa kumtunza Joel. Hilo linaniruhusu niwe na wakati zaidi wa kufanya mambo ya kiroho. Luigi pia anapata wakati zaidi wa kushughulikia mahitaji ya kiroho ya familia yetu na ya kutaniko, ambamo anaendelea kutumika akiwa mratibu wa baraza la wazee.

Kwa sababu ya hali zetu za pekee, tunakuwa na wakati mwingi zaidi wa kuwa pamoja tukiwa familia. Kadiri ambavyo wakati umepita, tumejifunza kuwa na usawaziko na kutotazamia kutimiza mambo mengi zaidi kuliko tunayoweza. Siku ambazo tumevunjika moyo, tunasali na kumweleza Yehova hisia zetu. Inahuzunisha kwamba wakati wana wetu David na Marc walipokuwa watu wazima na kuondoka nyumbani, baadaye waliacha kumtumikia Yehova. Tunatumaini kwamba siku moja watamrudia Yehova.—Luka 15:17-24.

Katika miaka mingi ambayo imepita, tumeona Yehova akitutegemeza na tumejifunza kumtegemea katika kila tatizo tunalokabili. Tunathamini sana maneno ya Isaya 41:13: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’” Kujua kwamba Yehova ameushika kwa nguvu mkono wetu kunatufariji. Kwa kweli, tunaweza kusema kwa hakika kwamba kukabiliana na majaribu kulitufanya tumtegemee zaidi Baba yetu wa mbinguni, Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Trisomy 21 ni ugonjwa ambao mtu anazaliwa nao na unasababisha mtu kuwa na akili punguani. Kwa kawaida chembe za kromosomu zinakuwa mbili-mbili au pea, lakini watoto wanaozaliwa na ugonjwa huo wana kromosomu ya ziada kwenye pea moja. Ugonjwa huo unavuruga kromosomu ya 21.

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Joel akiwa na mama yake, Ada

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ada, Joel, na Luigi

[Picha katika ukurasa wa 19]

Joel anafurahia kuwakaribisha akina ndugu na dada kwenye Jumba la Ufalme