Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninashukuru Kwamba Nimemtumikia Yehova, Hata Chini ya Majaribu

Ninashukuru Kwamba Nimemtumikia Yehova, Hata Chini ya Majaribu

Ninashukuru Kwamba Nimemtumikia Yehova, Hata Chini ya Majaribu

Limesimuliwa na Maatje de Jonge-van den Heuvel

NINA umri wa miaka 98. Nimefurahia kumtumikia Yehova kwa miaka 70 kati ya miaka hiyo—lakini imani yangu imejaribiwa pia. Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, nilipelekwa katika kambi ya mateso, na nikiwa huko pindi moja nilivunjika moyo na nikafanya uamuzi ambao ulifanya nijute baadaye. Miaka michache baadaye, nilipata jaribu lingine lililoniumiza sana moyo. Hata hivyo, ninamshukuru Yehova kwa sababu nimepata pendeleo la kumtumikia, hata chini ya majaribu.

Maisha yangu yalibadilika Oktoba (Mwezi wa 10) 1940. Nilikuwa nikiishi huko Hilversum, mji ulio kilomita 24 hivi kusini-mashariki ya Amsterdam huko Uholanzi. Nchi yetu ilitawaliwa na Wanazi. Nilikuwa nimeolewa na mume mwenye kujali Jaap de Jonge, ambaye tulikuwa tumeishi pamoja kwa miaka mitano na tulikuwa na binti mpendwa mwenye umri wa miaka mitatu aliyeitwa Willy. Tuliishi karibu na familia maskini ambayo ilikuwa na matatizo ya kupata chakula cha kuwalisha watoto wanane. Ingawa hivyo, waliishi pia na mwanamume fulani kijana. Nilijiuliza, ‘Kwa nini walijiongezea mzigo huo wa ziada?’ Nilipowapelekea chakula, nilitambua kwamba mwanamume huyo kijana alikuwa painia. Aliniambia kuhusu Ufalme wa Mungu na baraka ambazo Ufalme huo utaleta. Niliguswa moyo sana na mambo niliyojifunza, na mara moja nikakubali kweli. Mwaka huohuo, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Mwaka mmoja baada ya kubatizwa, mume wangu pia alikubali kweli.

Ingawa sikuijua Biblia vizuri, nilielewa kikamili kwamba nikiwa Shahidi, nilikuwa mshiriki wa tengenezo ambalo lilikuwa limepigwa marufuku. Pia, nilijua kwamba tayari Mashahidi wengi walikuwa wamefungwa gerezani kwa sababu ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Ingawa hivyo, nilianza mara moja kuhubiri nyumba kwa nyumba, na mimi na mume wangu tuliwakaribisha mapainia na waangalizi wanaosafiri ili waishi katika nyumba yetu. Nyumba yetu ilikuwa pia mahali pa kuweka vichapo vya Biblia, ambavyo tulipokea kutoka kwa ndugu na dada kutoka Amsterdam. Baiskeli zao za kubeba mizigo mizito zilijaa vitabu ambavyo vilikuwa vimefunikwa kwa kitambaa kizito na kigumu. Ndugu na dada hao waliosafirisha vitabu walikuwa na upendo na ujasiri mwingi kama nini! Walihatarisha uhai wao kwa ajili ya ndugu zao.—1 Yoh. 3:16.

“Mama, Utarudi Haraka?”

Miezi sita hivi baada ya kubatizwa, polisi watatu walikuja kwenye mlango wetu. Waliingia ndani ya nyumba na kuipekua-pekua. Ingawa hawakuona kabati la nguo lililokuwa limejaa vitabu, walipata vitabu fulani vikiwa vimefichwa chini ya kitanda chetu. Papo hapo wakaniamuru niende nao mpaka kwenye kituo cha polisi huko Hilversum. Nilipomkumbatia binti yangu ili kumwambia kwaheri, Willy aliniuliza, “Mama, utarudi haraka?” Nikamwambia, “Ndiyo, binti yangu, Mama atarudi nyumbani baada ya muda mfupi.” Hata hivyo, miezi 18 migumu ingepita kabla sijambeba tena mikononi.

Polisi mmoja alinipeleka kwa gari-moshi mpaka Amsterdam ili nikahojiwe. Polisi waliokuwa wakinihoji walijaribu kuniambia niwaambie ikiwa ndugu watatu kutoka Hilversum walikuwa Mashahidi wa Yehova. Nikasema: “Siwajui, isipokuwa mmoja. Yeye ndiye anayetuuzia maziwa.” Na ilikuwa kweli; ndugu huyo alikuwa akiuza maziwa. Nikaongezea hivi: “Lakini ili mjue kama yeye ni Shahidi wa Yehova, muulizeni yeye, si mimi.” Nilipokataa kusema jambo lingine lolote, walinipiga usoni na kunifungia katika gereza, ambamo waliniacha kwa muda wa miezi miwili. Mume wangu alipotambua mahali nilipokuwa, aliniletea nguo na chakula. Kisha, Agosti (Mwezi wa 8) 1941, nikapelekwa Ravensbrück—kambi ya mateso ya wanawake iliyojulikana sana kwa uovu, kilomita 80 hivi upande wa kaskazini wa Berlin, Ujerumani.

“Changamka, Dada”

Tulipofika, tuliambiwa kwamba tungeenda nyumbani ikiwa tungetia sahihi hati ya kuonyesha kwamba tumekana imani yetu. Lakini bila shaka sikutia sahihi. Badala yake, nililazimika kuwapa vitu nilivyokuwa navyo na nikavua mavazi yangu yote ndani ya bafu, ambamo nilikutana na dada fulani Wakristo kutoka Uholanzi. Katika kambi, tulipewa nguo za kuvaa ambazo zilikuwa na alama ya pembetatu ya zambarau iliyokuwa imeshonwa juu yake, tukapewa pia sahani, kikombe, na kijiko. Usiku wa kwanza, tuliwekwa katika vyumba vya kuweka wafungwa kwa muda. Nikiwa humo, nililia machozi kwa mara ya kwanza tangu nilipokamatwa. Nililia nikijiuliza, “Ni nini kitakachotokea? Nitakaa humu kwa muda gani?” Kwa kweli, wakati huo uhusiano wangu pamoja na Yehova haukuwa na nguvu sana, kwa kuwa nilikuwa nimejua kweli kwa miezi michache tu. Bado nilikuwa na mengi ya kujifunza. Siku iliyofuata tulipokuwa tukiitwa majina, inaonekana kwamba dada mmoja kutoka Uholanzi aliona nilivyohuzunika. Akasema: “Changamka, dada, changamka! Ni nini kinachoweza kutudhuru?”

Baada ya kuitwa majina, tulipelekwa katika vyumba vingine, ambamo tulikaribishwa na mamia ya akina dada Wakristo kutoka Ujerumani na Uholanzi. Tayari akina dada fulani kutoka Ujerumani walikuwa wameishi katika vyumba hivyo kwa zaidi ya mwaka mmoja. Ushirika wao ulinitia nguvu—kwa kweli, ushirika huo ulinichangamsha. Pia, nilifurahi sana kwa kuwa vyumba ambamo dada zetu walikuwa wakiishi vilikuwa safi kuliko vyumba vingine katika kambi hiyo. Mbali na kuwa safi, vyumba vyetu vilijulikana kuwa mahali ambapo watu hawakuiba, kutukanana, au kupigana. Tofauti na hali mbaya sana tulizokabili katika kambi, vyumba vyetu vilikuwa kama kisiwa safi kilichozungukwa na bahari chafu.

Maisha ya Kila Siku Katika Kambi

Maisha kambini yalihusisha kufanya kazi nyingi na kula chakula kidogo sana. Tulikuwa tukiamka saa kumi na moja asubuhi, na muda mfupi baadaye tuliitwa majina. Walinzi walitulazimisha kusimama nje kwa karibu saa moja, iwe kulikuwa na mvua au jua. Saa kumi na moja jioni, baada ya kufanya kazi ngumu kwa siku nzima, tuliitwa tena majina. Kisha tulikula mkate na supu halafu tukalala—tukiwa tumechoka.

Kila siku isipokuwa Jumapili (Siku ya Yenga), nilifanya kazi katika mashamba, ambako nilivuna ngano kwa upanga wa kufyeka majani, na pia niliondoa takataka kwenye mifereji au mitaro na kusafisha nyumba za nguruwe. Ingawa kazi hiyo ilikuwa ngumu na chafu, niliifanya kila siku kwa sababu bado nilikuwa kijana na nilikuwa na nguvu. Pia, nilijitia nguvu kwa kuimba nyimbo zenye ujumbe wa Biblia nilipokuwa nikifanya kazi. Hata hivyo, kila siku nilitamani kumwona mume wangu na mtoto wangu.

Tulipewa chakula kidogo sana, lakini sisi dada wote tulijaribu kuweka kando kipande cha mkate kila siku ili tuwe na chakula cha ziada ambacho tungekula Jumapili, wakati ambapo tulipata nafasi ya kuwa pamoja ili kuzungumzia habari za Biblia. Hatukuwa na vichapo vya Biblia, lakini niliwasikiliza kwa makini dada Wajerumani wenye umri mkubwa waliokuwa waaminifu walipokuwa wakizungumzia mambo ya kiroho. Hata tuliadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

Kutaabika, Kujuta, na Kutiwa Moyo

Nyakati nyingine, tuliamuriwa kufanya kazi ambayo iliunga mkono moja kwa moja jitihada za kivita za Wanazi. Kwa sababu ya msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote katika vita, dada wote walikataa kufanya kazi hiyo, na nilifuata mfano wao wa ujasiri. Tuliadhibiwa kwa kunyimwa chakula kwa siku nyingi na tulilazimika kusimama kwa saa nyingi wakati wa kuitwa majina. Pindi moja, wakati wa majira ya baridi kali, tulifungiwa kwa siku 40 katika jumba ambalo halikuwa na mfumo wa kupasha joto.

Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuliambiwa tena na tena kwamba tungeachiliwa na kuruhusiwa kwenda nyumbani ikiwa tungetia sahihi hati ya kukana imani yetu. Baada ya kuishi Ravensbrück kwa zaidi ya mwaka mmoja, nilivunjika moyo sana. Tamaa ya kumwona mume wangu na binti yangu ikawa yenye nguvu sana hivi kwamba nilienda kwa walinzi, nikawaomba fomu ambayo ilisema kwamba mimi si Mwanafunzi wa Biblia tena, na nikaitia sahihi.

Akina dada walipotambua jambo nililokuwa nimefanya, wengine wao walianza kuniepuka. Ingawa hivyo, dada wawili Wajerumani wenye umri mkubwa, Hedwig na Gertrud walinitafuta na kunihakikishia tena kwamba wananipenda. Tulipokuwa tukifanya kazi pamoja katika nyumba za nguruwe, walinieleza kwa fadhili kwa nini ni jambo la maana kudumisha utimilifu kwa Yehova na jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunampenda kwa kutolegeza msimamo wetu. Niliguswa moyo sana kwa sababu walinijali na kunionyesha shauku nyororo kama ya mama. * Nilijua kwamba nilikuwa nimekosea, na nilitaka hati ile ifutiliwe mbali. Jioni moja nilimwambia dada fulani kuhusu uamuzi wangu wa kutaka hati ile ifutiliwe mbali. Inaonekana kwamba ofisa mmoja katika kambi ile alisikia mazungumzo yetu kwa kuwa jioni hiyohiyo, mara moja niliwekwa huru kutoka katika ile kambi na kurudishwa Uholanzi kwa gari-moshi. Mmoja wa wasimamizi, ambaye bado ninakumbuka sura yake, aliniambia hivi: “Bado wewe ni Bibelforscher (Mwanafunzi wa Biblia), na utaendelea kuwa hivyo.” Nikamjibu: “Ndiyo, nitaendelea, ikiwa ni mapenzi ya Yehova.” Lakini bado niliendelea kufikiria, ‘Ninaweza kubadilisha jinsi gani hati niliyokuwa nimetia sahihi?’

Sehemu moja katika hati ile ilisema hivi: “Kupitia hati hii ninatoa uhakikisho kwamba sitashirikiana tena kamwe na shirika la International Bible Students Society.” Nilijua jambo ambalo nilipaswa kufanya! Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 1943, mara tu baada ya kufika nyumbani, nilianza tena kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Bila shaka, ikiwa ningeshikwa mara ya pili na askari wa Nazi nikihubiri kuhusu Ufalme wa Mungu, ningeadhibiwa vikali zaidi.

Ili kumhakikishia zaidi Yehova kwamba nilitamani kutoka moyoni kuwa mtumishi mshikamanifu, mimi na mume wangu tulifanya tena nyumba yetu iwe mahali ambapo wasafirishaji wa vichapo na waangalizi wanaosafiri wangeishi. Nilithamini kama nini kupata nafasi nyingine ya kuthibitisha upendo wangu kwa Yehova na kwa watu wake!

Tukio Lililotutia Uchungu Mwingi Moyoni

Miezi michache kabla ya vita kwisha, mimi na mume wangu tulikabiliana na tukio lililotutia uchungu mwingi moyoni. Mnamo Oktoba 1944, kwa ghafula binti yetu alipata ugonjwa. Willy alikuwa na ugonjwa wa koo (diphtheria). Hali yake ilizidi kuwa mbaya haraka, na akafa siku tatu baadaye. Alikuwa na umri wa miaka saba tu.

Tulipata pigo kubwa kwa kumpoteza mtoto wetu wa pekee. Kwa kweli, majaribu niliyopitia huko Ravensbrück hayawezi kulinganishwa hata kidogo na uchungu mwingi ambao nilihisi mtoto wetu alipokufa. Hata hivyo, sikuzote tulipokuwa tumeshuka sana moyo, tulifarijiwa na maneno ya Zaburi 16:8: “Nimemweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa.” Mimi na mume wangu tulikuwa na uhakika kabisa katika ahadi ya Yehova ya ufufuo. Tulishikamana na kweli na sikuzote tulikuwa wahubiri wenye bidii wa habari njema. Mume wangu alinisaidia sana kumtumikia Yehova kwa shukrani mpaka alipokufa mwaka wa 1969.

Baraka na Shangwe

Katika makumi ya miaka ambayo imepita, sikuzote chanzo kimoja kikuu cha shangwe kimekuwa kushirikiana kwa ukaribu na watumishi wa wakati wote. Kama tu ilivyokuwa wakati wa vita, tuliwakaribisha sikuzote katika nyumba yetu waangalizi wanaosafiri pamoja na wake zao walipotembelea kutaniko letu. Mwangalizi mmoja wa mzunguko pamoja na mke wake, Maarten na Nel Kaptein, hata waliishi katika nyumba yetu kwa miaka 13! Nel alipopata ugonjwa usioweza kupona, nilikuwa na pendeleo la kumtunza katika nyumba yetu kwa miezi mitatu mpaka alipokufa. Kushirikiana pamoja nao na ndugu na dada katika kutaniko letu kumenisaidia kufurahia paradiso ya kiroho ambayo tunayo sasa.

Jambo moja kuu katika maisha yangu lilitokea mwaka wa 1995, nilipopata mwaliko wa kuhudhuria mwadhimisho huko Ravensbrück. Nikiwa huko nilikutana na dada ambao tulikuwa pamoja katika kambi hiyo na sikuwa nimewaona kwa miaka zaidi ya 50! Kuwa pamoja nao kulikuwa jambo lenye kugusa moyo sana na lisiloweza kusahaulika na ilikuwa nafasi nzuri ya kutiana moyo kuendelea kutazamia siku ambayo wapendwa wetu waliokufa wataishi tena.

Mtume Paulo anasema hivi katika Waroma 15:4: “Kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” Ninamshukuru Yehova kwa kutoa tumaini hilo, ambalo limeniwezesha kumtumikia kwa shukrani, hata chini ya majaribu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Wakati huo, kwa sababu hakukuwa na mawasiliano pamoja na makao makuu, ndugu walishughulikia mambo yaliyohusu kulegeza msimamo kwa kadiri walivyoweza. Kwa sababu hiyo, watu ambao walilegeza msimamo walitendewa kwa njia tofauti-tofauti.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nikiwa pamoja na Jaap, mwaka wa 1930

[Picha katika ukurasa wa 10]

Binti yetu, Willy, akiwa na umri wa miaka saba

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mwaka wa 1995, niliguswa moyo sana nilipokutana tena na marafiki wa zamani. Nimeketi kwenye safu ya mbele, wa pili kutoka kushoto