Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uwe Tayari!

Uwe Tayari!

Uwe Tayari!

“Iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.”—MT. 24:44.

1, 2. (a) Ni matukio gani yaliyotabiriwa na unabii wa Biblia yanayoweza kulinganishwa na shambulizi la simbamarara? (b) Shambulizi linalokuja linakuhusu namna gani?

KWA miaka mingi, mwanamichezo fulani aliwafurahisha watu kwa kucheza kwa utulivu na simbamarara wake wa Bengal. Alisema hivi: “Mnyama anapokuamini, unahisi ni kana kwamba umepewa zawadi maridadi zaidi katika ulimwengu.” Lakini mnamo Oktoba 3, 2003 (3/10/2003), hali hiyo ya kuaminiana ilikwisha. Bila sababu yoyote, mmoja kati ya wanyama wake, simbamarara mweupe mwenye uzito wa kilogramu 172 alimshambulia mtu huyo. Mtu huyo aliyewazoeza wanyama alishambuliwa kwa ghafula. Hakuwa tayari.

2 Ni vizuri kukumbuka kwamba Biblia inatabiri shambulizi fulani la “mnyama-mwitu,” na tunahitaji kuwa tayari. (Soma Ufunuo 17:15-18.) Mnyama huyo anamshambulia nani? Katika badiliko la ghafula lenye kushangaza la matukio, ulimwengu wa Ibilisi unagawanyika na kushambulia sehemu zake nyingine. Yule mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu anafananisha shirika la Umoja wa Mataifa, na zile “pembe kumi” zinafananisha mamlaka zote za kisiasa. Mnyama huyo na hizo pembe kumi zitamgeukia huyo kahaba wa mfano Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, na kumharibu kwa hasira. Jambo hilo litatokea wakati gani? Hatujui siku wala saa. (Mt. 24:36) Tunajua tu kwamba uharibifu huo utatokea katika saa tusiyotazamia na tunajua kwamba wakati uliobaki kabla ya shambulizi hilo umepungua. (Mt. 24:44; 1 Kor. 7:29) Basi, ni jambo la maana tujitayarishe wenyewe kiroho ili shambulizi hilo litakapotokea na Kristo atakapokuja akiwa Mtekelezaji wa Hukumu, atakuwa pia Mkombozi wetu! (Luka 21:28) Ili kuwa tayari kiroho, tunaweza kujifunza kutokana na watumishi waaminifu wa Mungu ambao walikuwa tayari na hivyo wakajionea wenyewe ahadi za Mungu zikitimizwa. Je, tutachukua kwa uzito masimulizi hayo ya kweli?

Uwe Tayari Kama Noa

3. Ni hali gani zilizofanya iwe vigumu kwa Noa kumtumikia Mungu kwa uaminifu?

3 Hata ingawa hali zenye kuchukiza zilikuwa zimeenea duniani wakati wa maisha ya Noa, yeye alikuwa tayari kuona ahadi ya Mungu ikitimia. Wazia matatizo ambayo Noa alilazimika kupambana nayo wakati malaika waasi walipovaa miili ya kibinadamu na kufanya ngono na wanawake warembo! Mahusiano hayo yasiyo ya asili yalitokeza watoto wenye nguvu zinazopita za kibinadamu, “watu wenye nguvu” ambao walitumia nguvu zao nyingi kuwatesa wengine. (Mwa. 6:4) Fikiria jeuri na uharibifu mkubwa uliosababishwa na majitu hayo kila mahali yalipoenda. Matokeo ni kwamba uovu ulienea na fikira na tabia za wanadamu zikapotoka kabisa. Kisha, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova akatangaza wakati wa kuuharibu ulimwengu huo usiomwogopa Mungu.—Soma Mwanzo 6:3, 5, 11, 12. *

4, 5. Hali katika siku zetu zinalingana jinsi gani na hali katika siku za Noa?

4 Yesu alitabiri kwamba katika siku zetu hali zingekuwa kama zilivyokuwa katika siku za Noa. (Mt. 24:37) Kwa mfano, sisi pia tunashuhudia uvutano wa roho waovu. (Ufu. 12:7-9, 12) Malaika hao ambao ni roho waovu walivaa miili ya kibinadamu katika siku za Noa. Ingawa sasa wamezuiwa kuvaa miili ya kibinadamu, wanajitahidi kuwaongoza vijana na pia watu wazima. Bila kuonekana, malaika hao ambao wana maadili mapotovu ya kingono wanafurahia matendo maovu na machafu sana yanayofanywa na watu ambao wanakubali kupotoshwa na malaika hao duniani.—Efe. 6:11, 12.

5 Neno la Mungu linaeleza kwamba Ibilisi ni “muuaji” na linasema kwamba ana “uwezo wa kusababisha kifo.” (Yoh. 8:44; Ebr. 2:14) Nguvu zake za kusababisha kifo moja kwa moja zina mipaka. Hata hivyo, roho huyo mkatili anawachochea watu akitumia udanganyifu na ushawishi. Anapanda ndani ya akili na mioyo ya watu mielekeo ya kuua. Kwa mfano, mtoto 1 kati ya kila watoto 142 ambao wanazaliwa huko Marekani atauawa. Huku jeuri ya kipumbavu ikiwa imeenea sana, je, unafikiri kwamba Yehova haoni jeuri hiyo leo kama alivyoiona katika siku za Noa? Je, atakosa kuchukua hatua?

6, 7. Noa na familia yake walionyesha jinsi gani kwamba walikuwa na imani na kwamba walimwogopa Mungu?

6 Baadaye, Noa alijulishwa uamuzi wa Mungu wa kuleta gharika ya maji juu ya dunia, na kuwaharibu wote wenye mwili. (Mwa. 6:13, 17) Yehova alimwagiza Noa ajenge safina inayofanana na sanduku kubwa. Noa na familia yake walianza kazi hiyo. Ni nini kilichowasaidia kutii na kuwa tayari wakati hukumu ya Mungu ilipofika?

7 Imani yenye nguvu sana na kumwogopa Mungu kulimchochea Noa na familia yake kufanya kama Mungu alivyoamuru. (Mwa. 6:22; Ebr. 11:7) Akiwa kichwa cha familia, Noa alikaa macho kiroho na kuepuka uchafu wa ulimwengu huo wa zamani. (Mwa. 6:9) Alijua kwamba familia yake ilihitaji kujilinda ili isiige matendo ya kijeuri na mtazamo wa ukaidi wa watu waliowazunguka. Lilikuwa jambo la maana kwao kutojishughulisha kupita kiasi na mambo ya kila siku ya maisha. Mungu alikuwa na kazi ambayo alitaka wafanye, na lilikuwa jambo la maana kwa familia nzima kutanguliza kazi hiyo katika maisha yao.—Soma Mwanzo 6:14, 18.

Noa na Familia Yake Walikuwa Tayari

8. Ni nini kinachoonyesha kwamba washiriki wa familia ya Noa walizoea ujitoaji-kimungu?

8 Masimulizi ya Biblia yanamkazia uangalifu Noa, kichwa cha familia, lakini mke na wana wa Noa pamoja na wake zao walikuwa pia waabudu wa Yehova. Nabii Ezekieli alithibitisha hilo. Alisema kwamba ikiwa Noa angeishi katika siku za Ezekieli, watoto wake hawangeokolewa kwa sababu ya uadilifu wa baba yao. Walikuwa watu wazima na wangeweza kutii au kutotii. Kwa hiyo, kila mmoja wao alikuwa ameonyesha kwamba anampenda Mungu na njia zake. (Eze. 14:19, 20) Washiriki wa familia ya Noa walikubali maagizo yake, wakawa na imani kama yake, na hawakuruhusu uvutano wa wengine uwazuie kufanya kazi waliyopewa na Mungu.

9. Tunaweza kutaja mifano ya watu gani leo ambao wana imani kama ya Noa?

9 Inatia moyo kama nini leo kuona katika undugu wetu wa ulimwenguni pote vichwa vya familia ambao wanafanya yote wanayoweza ili kumwiga Noa! Wanatambua kwamba haitoshi tu kuandalia familia zao chakula, mavazi, makao, na elimu. Ni lazima pia watimize mahitaji ya kiroho ya familia zao. Wanapofanya hivyo, wanaonyesha kwamba wako tayari kwa ajili ya yale ambayo Yehova atafanya hivi karibuni.

10, 11. (a) Bila shaka Noa na familia yake walihisi namna gani walipokuwa ndani ya safina? (b) Ni swali au ulizo gani ambalo tunapaswa kujiuliza?

10 Huenda Noa, mke wake, watoto wake wa kiume, na wake zao walijenga safina kwa miaka 50 hivi. Bila shaka, walipokuwa wakijenga safina, waliingia na kutoka ndani yake mara nyingi sana. Waliifunika kwa lami ili maji yasiingie ndani, wakaweka vyakula na kuingiza wanyama ndani yake. Hebu wazia jinsi hali ilivyokuwa. Mwishowe ile siku kubwa waliyongojea inafika. Ni siku ya 17 ya mwezi wa pili mwaka wa 2370 K.W.K., wanaingia ndani ya safina. Yehova anafunga mlango, kisha mvua inaanza kunyesha. Hii si mvua ya kawaida tu ya mafuriko. Kilindi kikubwa cha maji ambayo yako juu ya anga au bahari ya mbinguni, kinafunguka na mvua kubwa sana inaanza kuipiga safina. (Mwa. 7:11, 16) Watu walio nje ya safina wanakufa lakini wale walio ndani wanaokolewa. Huenda Noa na familia yake walihisi namna gani? Bila shaka, walimshukuru sana Mungu. Lakini hapana shaka kwamba walifikiria hivi: ‘Tunafurahi kama nini kwamba tulitembea pamoja na Mungu wa kweli na tulikuwa tayari!’ (Mwa. 6:9) Je, unaweza kujiwazia ukiwa umeokoka Har-Magedoni, moyo wako ukiwa umejaa uthamini kama huo?

11 Hakuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Mweza-Yote asitimize ahadi yake ya kuuharibu mfumo huu wa mambo wa kishetani. Jiulize hivi: ‘Je, nina hakika kabisa kwamba hakuna ahadi yoyote ya Mungu itakayokosa kutimia hata katika jambo dogo na kwamba ahadi zote zitatimizwa kwa wakati alioweka?’ Ikiwa ndivyo, uwe tayari kwa kuendelea kuiweka karibu akilini ‘siku hiyo ya Yehova’ inayokuja haraka.—2 Pet. 3:12.

Musa Aliendelea Kukaa Macho

12. Ni nini ambacho kingeweza kumpofusha Musa kiroho?

12 Acheni tuzungumzie mfano mwingine. Kwa maoni ya kibinadamu, Musa alionekana kuwa na nafasi nzuri sana ya kufanikiwa katika nchi ya Misri. Kwa kuwa binti ya Farao alimchukua na kumlea kama mwana wake, inaelekea kwamba Musa aliheshimiwa sana na alifurahia vyakula bora kabisa, mavazi mazuri kabisa, na mazingira yenye kustarehesha kabisa. Alielimishwa sana. (Soma Matendo 7:20-22.) Huenda angepokea urithi mkubwa sana.

13. Musa aliendelea jinsi gani kukazia macho ahadi za Mungu?

13 Inaonekana kwamba mazoezi ambayo Musa alipata kutoka kwa wazazi wake alipokuwa mtoto mchanga yalimwezesha kutambua upumbavu wa ibada ya sanamu ya Wamisri. (Kut. 32:8) Elimu ya Misri na utajiri wa nyumba ya mfalme haukumfanya Musa aache ibada ya kweli. Bila shaka, alitafakari sana kuhusu ahadi ambazo Mungu aliwapa mababu zake naye alitamani sana kuonyesha kwamba alikuwa tayari kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa kweli, Musa aliwaambia hivi wana wa Israeli: “Yehova . . . Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu.”—Soma Kutoka 3:15-17.

14. Imani na ujasiri wa Musa ulijaribiwa jinsi gani?

14 Tofauti na sanamu zote zilizowakilisha miungu isiyo hai ya Misri, Mungu wa kweli, Yehova, alikuwa halisi kwa Musa. Musa aliishi kana kwamba alikuwa akimwona “Yeye asiyeonekana.” Musa alikuwa na imani kwamba watu wa Mungu wangewekwa huru, lakini hakujua hilo lingetukia wakati gani. (Ebr. 11:24, 25, 27) Tamaa yake yenye nguvu ya kuona Waebrania wakiwekwa huru ilionekana wakati alipomtetea mtumwa Mwisraeli aliyekuwa akiteswa. (Kut. 2:11, 12) Hata hivyo, wakati wa Yehova wa kufanya hivyo haukuwa umefika, kwa hiyo Musa alilazimika kuishi akiwa mkimbizi katika nchi ya mbali. Bila shaka, ilikuwa vigumu kwake kuacha mazingira yenye starehe katika makao ya mfalme wa Misri na kuishi jangwani. Hata hivyo, Musa alionyesha kwamba alikuwa tayari kwa kuwa macho na kufuata kila agizo ambalo Yehova alimpa. Hivyo, baada ya Musa kukaa Midiani kwa miaka 40, Mungu angeweza kumtumia kuwaletea ndugu zake kitulizo. Musa alitii mwongozo wa Mungu na kurudi Misri. Wakati ulikuwa umefika wa Musa kutimiza mgawo aliopewa na Mungu na kufanya kazi ya Mungu kwa njia ya Mungu. (Kut. 3:2, 7, 8, 10) Aliporudi Misri, Musa, ‘aliyekuwa mpole zaidi kuliko watu wote,’ alihitaji imani na ujasiri ili kufika mbele ya Farao. (Hes. 12:3) Alifanya hivyo, si mara moja tu, bali tena na tena kadiri mapigo yalivyotolewa, na baada ya kila pigo hakujua angerudi mbele ya Farao mara ngapi zaidi.

15. Hata ingawa Musa alipata vipingamizi, ni nini kilichomchochea kutumia kila nafasi aliyopata kumheshimu Baba yake wa mbinguni?

15 Katika muda wa miaka 40 iliyofuata, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. mpaka 1473 K.W.K., Musa alipatwa na mambo yenye kuvunja moyo. Hata hivyo, alitumia kila nafasi aliyopata kumheshimu Yehova na kwa moyo wote aliwatia moyo Waisraeli wenzake wafanye hivyo. (Kum. 31:1-8) Kwa nini? Kwa sababu alilipenda jina na enzi kuu ya Yehova kuliko jina lake mwenyewe. (Kut. 32:10-13; Hes. 14:11-16) Hata tukipata vipingamizi au hali zenye kuvunja moyo, sisi pia ni lazima tuendelee kuunga mkono utawala wa Mungu, tukiwa na hakika kwamba njia yake ya kufanya mambo ni yenye hekima zaidi, ya uadilifu zaidi, na bora zaidi kuliko njia nyingine yoyote. (Isa. 55:8-11; Yer. 10:23) Je, hivyo ndivyo unavyohisi?

Endelea Kukesha!

16, 17. Kwa nini andiko la Marko 13:35-37 ni la maana sana kwako?

16 “Endeleeni kutazama, endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni gani.” (Marko 13:33) Yesu alitoa onyo hilo alipokuwa akizungumza kuhusu ishara ya umalizio wa mfumo huu mwovu wa mambo. Fikiria maneno ya mwisho ya unabii mkubwa wa Yesu ulioandikwa katika kitabu cha Marko: “Endeleeni kukesha, kwa maana hamjui bwana wa nyumba anakuja wakati gani, kama ni wakati wa jioni au katikati ya usiku au anapowika jogoo au asubuhi na mapema; ili anapofika kwa ghafula, asiwakute mkiwa mmelala usingizi. Lakini lile ninalowaambia ninyi ninawaambia wote, Endeleeni kukesha.”—Marko 13:35-37.

17 Himizo la Yesu linachochea fikira. Alitaja vipindi vinne tofauti vya kukesha wakati wa usiku. Kipindi cha mwisho ndicho kingekuwa kipindi kigumu zaidi cha kukesha kwa sababu kilianza saa tisa ya usiku mpaka jua linapochomoza asubuhi. Wataalamu wa kupanga vita waliona kipindi hicho kuwa kipindi kizuri zaidi cha kushambulia maadui, kwa kuwa ilikuwa nafasi bora zaidi ya kuwakuta wakiwa ‘wamelala usingizi.’ Vivyo hivyo leo, wakati ambapo ulimwengu unalala usingizi mzito wa kiroho, huenda tukahitaji kujikaza zaidi ili tuendelee kukesha. Je, tuna shaka yoyote kwamba tunahitaji ‘kuendelea kukesha’ na ‘kuendelea kutazama’ kwa sababu ya mwisho uliotabiriwa na pia ukombozi wetu?

18. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuna pendeleo gani lisilo na kifani?

18 Yule mtu aliyekuwa akiwazoeza wanyama, ambaye alitajwa mwanzoni, aliokoka shambulizi la yule simbamarara wa Bengal. Lakini unabii wa Biblia unaonyesha bila kukosea kwamba dini ya uwongo na hata sehemu inayobaki ya mfumo huu mwovu haitaokoka mwisho unaokuja. (Ufu. 18:4-8) Watumishi wote wa Mungu, wadogo kwa wakubwa, na waone umuhimu wa kufanya yote wanayoweza ili kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova kama Noa na familia yake. Tunaishi katika ulimwengu ambao haumheshimu Mungu na ambamo walimu wa dini ya uwongo, na pia watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu na wale wanaoamini kwamba mambo yake hayawezi kujulikana, wanamdhihaki Muumba kwa maneno yao. Lakini hatuwezi kupuuza hatari ya kupotoshwa. Acheni tutie moyoni mifano ambayo tumezungumzia na kuendelea kutumia nafasi tunazopata kumtetea na kumheshimu Yehova akiwa “Mungu wa miungu,” ndiyo, “Mungu mkuu, mwenye nguvu na mwenye kuogopesha.”—Kum. 10:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kuhusu “miaka 120” inayotajwa katika Mwanzo 6:3, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 2010 (15/12/2010), ukurasa wa 30.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Noa alihitaji kutanguliza mahitaji ya kiroho ya familia yake?

• Nyakati zetu zinalingana sana jinsi gani na nyakati za Noa?

• Kwa nini Musa alikazia macho ahadi za Yehova hata ingawa alipatwa na mambo yenye kuvunja moyo?

• Ni unabii gani mbalimbali wa Biblia unaokuchochea kuendelea kukesha kiroho?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Noa na familia yake walikazia fikira kazi ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ahadi hakika za Mungu zilimsaidia Musa kuendelea kukaa macho