Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walimngoja Masihi

Walimngoja Masihi

Walimngoja Masihi

“Watu walikuwa wakingoja, na wote walikuwa wakiwaza mioyoni mwao juu ya Yohana, kama ndiye aliyekuwa Masihi.” —LUKA 3:15, THE EMPHATIC DIAGLOTT.

1. Wachungaji fulani walisikia tangazo gani lililotolewa na malaika?

USIKU umeingia. Wachungaji wako nje, wakichunga mifugo yao. Wanashtuka malaika wa Yehova anaposimama kando yao na utukufu wa Mungu unapowaangazia pande zote! Sikiliza! Malaika huyo anatoa tangazo hili la pekee: ‘Msiogope, kwa maana, tazama! ninawatangazia ninyi habari njema ya shangwe kubwa ambayo watu wote watakuwa nayo, kwa sababu leo, Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu,’ yule ambaye atakuwa Masihi. Wachungaji watamkuta mtoto huyo akiwa amelazwa ndani ya hori katika mji wa karibu. Kwa ghafula, “umati wa jeshi la mbingu” unaanza kumsifu Yehova ukisema: “Utukufu katika vilele vilivyo juu kwa Mungu, na juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.”—Luka 2:8-14.

2. Neno “Masihi” linamaanisha nini, na anaweza kutambuliwa jinsi gani?

2 Bila shaka, wachungaji hao Wayahudi wanajua kwamba neno “Masihi,” au “Kristo,” linamaanisha “Mtiwa-Mafuta” wa Mungu. (Kut. 29:5-7) Lakini watafanya nini ili wajifunze na wawasadikishe wengine kwamba mtoto ambaye ametajwa na malaika atakuwa Masihi aliyechaguliwa na Yehova? Ni kwa kuchunguza unabii unaopatikana katika Maandiko ya Kiebrania na kuulinganisha na utendaji na maisha ya mtoto huyo.

Kwa Nini Watu Walikuwa Wakimngoja Masihi?

3, 4. Tunaelewa jinsi gani andiko la Danieli 9:24, 25?

3 Miaka mingi baadaye, Yohana Mbatizaji alianza kazi ya kuhubiri. Watu fulani waliposikia mambo aliyosema na kufanya walifikiri kwamba Masihi alikuwa amefika. (Soma Luka 3:15.) Inawezekana kwamba wengine walielewa kwa usahihi unabii wa Kimasihi unaohusu “majuma 70.” Ikiwa ndivyo, wangeweza kukadiria wakati ambapo Masihi angetokea. Kwa sehemu, unabii huo ulisema hivi: “Tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.” (Dan. 9:24, 25) Wasomi mbalimbali wanakubali kwamba hayo ni majuma ya miaka. Kwa mfano, tafsiri moja ya Biblia (Revised Standard Version) inasema hivi: “Majuma 70 ya miaka yameamuriwa.”

4 Leo, watumishi wa Yehova wanajua kwamba yale majuma 69, au miaka 483, ya Danieli 9:25 yalianza mwaka wa 455 K.W.K. wakati Mfalme Artashasta wa Uajemi alipomwamuru Nehemia arudishe na kujenga upya Yerusalemu. (Neh. 2:1-8) Majuma hayo yalimalizika miaka 483 baadaye, katika mwaka wa 29 W.K., wakati Yesu wa Nazareti alipobatizwa na kutiwa-mafuta kwa roho takatifu, na hivyo akawa Masihi.—Mt. 3:13-17. *

5. Kwa sasa tutachunguza unabii gani mbalimbali?

5 Acheni sasa tuchunguze unabii fulani kati ya unabii mwingi unaomhusu Masihi ambao ulitimia kuhusiana na kuzaliwa kwa Yesu, maisha yake ya utotoni, na huduma yake. Bila shaka, kufanya hivyo kutatia nguvu imani yetu katika neno la Mungu la kinabii. Na hilo litatusaidia kuona wazi kwamba Yesu alikuwa kwa kweli yule Masihi aliyengojewa kwa muda mrefu.

Maisha Yake ya Utotoni Yalitabiriwa

6. Eleza jinsi andiko la Mwanzo 49:10 lilivyotimia.

6 Masihi angezaliwa Israeli katika kabila la Yuda. Mzee wa ukoo Yakobo aliwabariki watoto wake wa kiume kabla ya kifo chake na kutabiri hivi: “Fimbo ya enzi haitageuka kando kutoka kwa Yuda, wala fimbo ya kiongozi kutoka katikati ya miguu yake, mpaka Shilo aje; na vikundi vya watu vitamtii yeye.” (Mwa. 49:10) Wasomi wengi wa kale Wayahudi walisema kwamba maneno hayo yalimhusu Masihi. Kuanzia utawala wa Mfalme Daudi wa Yuda, fimbo (enzi ya kifalme) na fimbo ya uongozi (mamlaka ya kuongoza) ilikuwa katika kabila la Yuda. Neno “Shilo” linamaanisha “Yeye Ambaye Ni Yake; Yeye Ambaye Ni Mali Yake.” Ukoo wa kifalme wa Yuda ungefikia mwisho wake wakati ambapo “Shilo” angekuwa Mrithi wa kifalme wa kudumu, kwa sababu Mungu alimwambia Sedekia, mfalme wa mwisho wa Yuda, kwamba yule aliye na haki ya kisheria ndiye angepewa utawala huo. (Eze. 21:26, 27) Baada ya Sedekia, Yesu ndiye mzao pekee wa Daudi ambaye aliahidiwa ufalme. Kabla Yesu hajazaliwa, malaika Gabrieli alimwambia Maria hivi: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Ni lazima Shilo awe ni Yesu Kristo, ambaye alikuwa mzao wa Yuda na Daudi.—Mt. 1:1-3, 6; Luka 3:23, 31-34.

7. Masihi alizaliwa wapi, na kwa nini hilo ni jambo la pekee?

7 Masihi angezaliwa Bethlehemu. Nabii Mika aliandika hivi: “Nawe, Ee Bethlehemu Efratha, wewe uliye mdogo sana kuwa kati ya maelfu ya Yuda, kutoka kwako atanijia yeye atakayekuwa mtawala katika Israeli, ambaye asili yake ni kutoka nyakati za kale, kutoka siku za wakati usio na kipimo.” (Mika 5:2) Masihi angezaliwa katika mji wa Bethlehemu huko Yuda, na inaonekana kwamba zamani mji huo uliitwa Efratha. Ingawa Maria mama ya Yesu, na baba yake mlezi, Yosefu, waliishi huko Nazareti, mtawala wa Roma aliamuru watu wajiandikishe na hivyo wakarudi Bethlehemu, ambako Yesu alizaliwa mwaka wa 2 K.W.K. (Mt. 2:1, 5, 6) Kwa kweli, unabii kuhusu kuzaliwa kwa Yesu ulitimia kama ilivyotabiriwa!

8, 9. Ni nini kilichotabiriwa kuhusu kuzaliwa kwa Masihi na matukio yaliyofuata?

8 Masihi angezaliwa na bikira. (Soma Isaya 7:14.) Neno la Kiebrania bethu·lahʹ linamaanisha “bikira,” lakini neno lingine (ʽal·mahʹ) linapatikana katika Isaya 7:14. Katika andiko hilo, ilitabiriwa kwamba “mwanamwali [ha·ʽal·mahʹ]” angezaa mwana. Neno ʽal·mahʹ linatumiwa kumhusu mwanamwali Rebeka kabla ya kuolewa. (Mwa. 24:16, 43) Chini ya mwongozo wa roho ya Mungu, Mathayo alitumia neno la Kigiriki (par·theʹnos) linalomaanisha “bikira” alipoonyesha kwamba andiko la Isaya 7:14 lilitimia kuhusiana na kuzaliwa kwa Yesu. Waandikaji wa Injili, Mathayo na Luka, wanasema kwamba Maria alikuwa bikira aliyepata mimba kupitia nguvu za roho ya Mungu.—Mt. 1:18-25; Luka 1:26-35.

9 Watoto wachanga wangeuawa baada ya kuzaliwa kwa Masihi. Jambo fulani linalofanana na hilo lilitukia karne nyingi mapema wakati Farao wa Misri alipoamuru kwamba watoto wa kiume Waebrania watupwe ndani ya Mto Nile. (Kut. 1:22) Lakini jambo kuu hasa linapatikana katika andiko la Yeremia 31:15, 16, ambalo linasema kwamba Raheli anawalilia wanawe ambao walipelekwa katika “nchi ya adui.” Maombolezo au kilio chake kilisikika mbali huko Rama, katika eneo la Benyamini upande wa kaskazini wa Yerusalemu. Mathayo anaonyesha kwamba maneno ya Yeremia yalitimia wakati Mfalme Herode alipoamuru watoto wote wachanga wa kiume wachinjwe huko Bethlehemu na katika maeneo ya karibu. (Soma Mathayo 2:16-18.) Fikiria huzuni ya watu katika eneo hilo!

10. Eleza jinsi andiko la Hosea 11:1 lilivyotimia kumhusu Yesu.

10 Kama Waisraeli, Masihi angeitwa kutoka Misri. (Hos. 11:1) Kabla Herode hajaamuru watoto wa kiume wauawe, malaika aliwaagiza Yosefu, Maria, na Yesu waende Misri. Walikaa huko “mpaka kufa kwa Herode, ili litimizwe lile lililosemwa na Yehova kupitia nabii [Hosea], akisema: ‘Kutoka Misri nilimwita mwanangu.’” (Mt. 2:13-15) Bila shaka, Yesu hangeweza kuongoza kwa ujanja mambo yaliyotabiriwa kuhusiana na kuzaliwa kwake na maisha yake ya utotoni.

Masihi Anaanza Kutenda!

11. Mtiwa-Mafuta wa Yehova alitayarishiwa njia jinsi gani?

11 Njia ilipaswa kutayarishwa mbele ya Mtiwa-Mafuta wa Mungu. Malaki alitabiri kwamba “nabii Eliya” angefanya kazi hiyo ya kutayarisha mioyo ya watu kwa ajili ya kuja kwa Masihi. (Soma Malaki 4:5, 6.) Yesu mwenyewe alisema kwamba Yohana Mbatizaji ndiye aliyekuwa “Eliya.” (Mt. 11:12-14) Naye Marko alionyesha kwamba huduma ya Yohana ilitimiza unabii wa Isaya. (Isa. 40:3; Marko 1:1-4) Yesu hakumwambia Yohana afanye kazi kama ya Eliya ya kumtayarishia njia. Kazi ya huyo “Eliya” aliyetabiriwa ilifanywa kupatana na mapenzi ya Mungu ili kuwasaidia watu wamtambue Masihi.

12. Ni kazi gani inayomtambulisha Masihi?

12 Kazi aliyopewa na Mungu inamtambulisha Masihi. Katika sinagogi la Nazareti, mji ambako alilelewa, Yesu alisoma kitabu cha kukunjwa cha Isaya na kusema kwamba maneno yafuatayo yalimhusu: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema, alinituma kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka na kupata kuona tena kwa vipofu, kuacha waliopondeka waende zao wakiwa wameachiliwa huru, kuhubiri mwaka wa Yehova wenye kukubalika.” Na kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa Masihi, kwa kufaa Yesu alisema hivi: “Leo andiko hili ambalo mmesikia sasa hivi limetimizwa.”—Luka 4:16-21.

13. Huduma ya hadharani ya Yesu huko Galilaya ilitabiriwa jinsi gani?

13 Huduma ya hadharani ya Masihi huko Galilaya ilitabiriwa. Kuhusu “nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali . . . Galilaya ya mataifa,” Isaya aliandika hivi: “Watu waliokuwa wakitembea katika giza wameona nuru kuu. Kwa habari ya wale wanaokaa katika nchi yenye kivuli kizito, nuru imewaangazia.” (Isa. 9:1, 2) Yesu alianza huduma yake ya hadharani huko Galilaya, naye aliishi Kapernaumu, ambako wakaaji wengi wa Zabuloni na Naftali walifaidika na nuru ya kiroho ambayo aliwaletea. (Mt. 4:12-16) Huko Galilaya, Yesu alitoa Mahubiri yake ya Mlimani yenye kuchochea sana, aliwachagua mitume wake, alifanya muujiza wake wa kwanza, na inaelekea kwamba aliwatokea wanafunzi 500 hivi baada ya kufufuliwa. (Mt. 5:1–7:27; 28:16-20; Marko 3:13, 14; Yoh. 2:8-11; 1 Kor. 15:6) Hivyo, alitimiza unabii wa Isaya kwa kuhubiri katika “nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali.” Bila shaka, Yesu aliendelea kuhubiri ujumbe wa Ufalme katika maeneo mengine ya Israeli.

Utendaji Mwingine wa Masihi Ulitabiriwa

14. Yesu alitimiza unabii wa Zaburi 78:2 kwa njia gani?

14 Masihi angesema kwa kutumia mifano. Mtunga-zaburi Asafu aliimba hivi: “Katika neno la kimethali nitakifungua kinywa changu.” (Zab. 78:2) Tunajua jinsi gani kwamba unabii huo ulimhusu Yesu? Mathayo anatueleza jambo hilo. Baada ya kueleza mifano ya Yesu ambayo ilifananisha Ufalme na chachu na pia mbegu ya haradali inayokua, Mathayo anasema hivi: “[Yesu] hakuwa akisema nao bila mfano; ili litimizwe lililosemwa kupitia nabii aliyesema: ‘Nitakifungua kinywa changu kwa mifano, nitatangaza mambo yaliyofichwa tangu kuwekwa msingi.’” (Mt. 13:31-35) Maneno ya kimethali au mifano, ni moja kati ya njia zenye matokeo ambazo Yesu alitumia kufundisha.

15. Eleza jinsi unabii wa Isaya 53:4 ulivyotimia.

15 Masihi angebeba udhaifu wetu. Isaya alitabiri hivi: “Kwa kweli yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu; na kwa habari ya maumivu yetu, yeye aliyabeba.” (Isa. 53:4) Mathayo alisema kwamba baada ya kumponya mama-mkwe wa Petro, Yesu aliwaponya wengine ili “litimizwe lile lililosemwa kupitia nabii Isaya, akisema: ‘Yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu na kuyachukua maradhi yetu.’” (Mt. 8:14-17) Na hilo ni simulizi moja tu kati ya masimulizi mengi yanayoonyesha kwamba Yesu aliwaponya wagonjwa.

16. Mtume Yohana alionyesha jinsi gani kwamba Yesu alitimiza unabii wa Isaya 53:1?

16 Watu wengi hawangemwamini Masihi hata ingawa angefanya mambo mengi mazuri. (Soma Isaya 53:1.) Akionyesha kwamba unabii huo ulitimia, mtume Yohana aliandika hivi: “Ijapokuwa [Yesu] alikuwa amefanya ishara nyingi sana mbele yao, hawakuwa wanamwamini, hata kwamba neno la nabii Isaya likatimizwa ambalo alisema: ‘Yehova, ni nani aliyeliamini jambo ambalo tumesikia? Na kwa habari ya mkono wa Yehova, umefunuliwa kwa nani?’” (Yoh. 12:37, 38) Hata wakati wa huduma ya mtume Paulo, ni watu wachache sana ambao waliamini habari njema ya kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi.—Rom. 10:16, 17.

17. Yohana alisema unabii wa Zaburi 69:4 ulitimia jinsi gani?

17 Masihi angechukiwa bila sababu. (Zab. 69:4) Mtume Yohana anataja maneno haya ya Yesu: “Kama singefanya kati [ya watu] kazi ambazo hakuna mwingine aliyezifanya, hawangekuwa na dhambi; lakini sasa wameniona na pia wamenichukia mimi na vilevile Baba yangu. Lakini ni ili neno lililoandikwa katika Sheria yao lipate kutimizwa, ‘Walinichukia bila sababu.’” (Yoh. 15:24, 25) Mara nyingi neno “Sheria” linamaanisha Maandiko yote kwa ujumla. (Yoh. 10:34; 12:34) Masimulizi ya Injili yanathibitisha kwamba Yesu alichukiwa, hasa na viongozi wa dini ya Kiyahudi. Zaidi ya hayo, Kristo alisema hivi: “Ulimwengu hauna sababu ya kuwachukia ninyi, lakini huo unanichukia mimi, kwa sababu ninatoa ushahidi juu yake kwamba kazi zake ni mbovu.”—Yoh. 7:7.

18. Ni habari gani zaidi ambayo itatusaidia kusadiki kabisa kwamba Yesu ndiye Masihi?

18 Wafuasi wa Yesu katika karne ya kwanza walikuwa na hakika kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi, kwa sababu kwa kweli alitimiza unabii mbalimbali kumhusu Masihi unaopatikana katika Maandiko ya Kiebrania. (Mt. 16:16) Kama tulivyoona, unabii fulani ulitimia wakati Yesu wa Nazareti alipokuwa mtoto na wakati wa huduma yake. Unabii mwingine kumhusu Masihi utazungumziwa katika habari inayofuata. Bila shaka, tukisali na kutafakari kuhusu unabii huo, tutasadiki kabisa kwamba kwa kweli Yesu Kristo ndiye Masihi aliyewekwa rasmi na Baba yetu wa mbinguni, Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa mazungumzo zaidi kuhusu yale “majuma 70,” ona sura ya 11 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

Ungesema Nini?

• Ni unabii gani mbalimbali uliotimizwa wakati wa kuzaliwa kwa Yesu?

• Masihi alitayarishiwa njia jinsi gani?

• Ni maneno gani ya unabii wa Isaya sura ya 53 yaliyotimia kuhusiana na Yesu?

[Maswali ya Funzo]