Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtegemee Yehova, “Mungu wa Faraja Yote”

Mtegemee Yehova, “Mungu wa Faraja Yote”

Mtegemee Yehova, “Mungu wa Faraja Yote”

“Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 KOR. 1:3.

1. Kila mwanadamu hata awe na umri gani anahitaji nini?

TANGU tunapozaliwa na kuendelea, tunahitaji faraja. Mtoto mchanga analia ili kutujulisha kwamba anahitaji kufarijiwa. Labda anataka abebwe au ana njaa. Hata tunapozeeka, mara nyingi tunahitaji kufarijiwa. Inakuwa hivyo hasa wakati tunapopatwa na hali ngumu.

2. Yehova anatoa uhakikisho gani kwamba atawafariji wale wanaomtegemea?

2 Mara nyingi, washiriki wa familia na marafiki wanaweza kutufariji kwa kadiri fulani. Hata hivyo, nyakati nyingine wanadamu hawana uwezo wa kukomesha hali zinazosababisha huzuni. Mungu tu ndiye anayeweza kutufariji hata tukipatwa na hali yoyote yenye kuhuzunisha. Neno lake linatuhakikishia hivi: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, . . . naye atakisikia kilio chao cha kuomba msaada.” (Zab. 145:18, 19) Ndiyo, “macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.” (Zab. 34:15) Lakini ikiwa tunataka Mungu atusaidie na kutufariji, ni lazima tumtegemee. Mtunga-zaburi Daudi alionyesha hilo wazi alipoimba hivi: “Yehova atakuwa kilele salama kwa ajili ya mtu yeyote aliyekandamizwa, kilele salama wakati wa taabu. Na wale wanaolijua jina lako watakutegemea, kwa maana hakika hutawaacha wale wanaokutafuta, Ee Yehova.”—Zab. 9:9, 10.

3. Yesu alitoa mfano gani unaoonyesha kwamba Yehova anawapenda watu Wake?

3 Waabudu wa Yehova ni wenye thamani machoni pake. Yesu alionyesha hilo wazi aliposema: “Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado hakuna hata mmoja wao husahaulika mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.” (Luka 12:6, 7) Kupitia nabii Yeremia, Yehova aliwaambia hivi watu Wake wa kale: “Nimekupenda wewe kwa upendo mpaka wakati usio na kipimo. Ndiyo sababu nimekuvuta kwa fadhili zenye upendo.”—Yer. 31:3.

4. Kwa nini tunaweza kuzitegemea ahadi za Yehova?

4 Kumtegemea Yehova na utimizo wa ahadi zake kunaweza kutufariji nyakati za huzuni. Kwa hiyo, tunapaswa pia kumtegemea Mungu kama alivyofanya Yoshua, ambaye alisema hivi: “Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.” (Yos. 23:14) Zaidi ya hayo, hata tukilemewa kwa muda na hali ngumu, tunaweza kuwa na hakika kwamba “Mungu ni mwaminifu” naye hatawaacha kamwe watumishi wake washikamanifu.—Soma 1 Wakorintho 10:13.

5. Kwa nini tunaweza kuwafariji wengine?

5 Mtume Paulo anamtaja Yehova kuwa “Mungu wa faraja yote.” “Kufariji” kunamaanisha kumtuliza mtu aliye na taabu au huzuni. Tunamfariji mtu wakati tunapompunguzia taabu au huzuni yake na hivyo kumletea kitulizo. Bila shaka, Yehova anafanya hivyo. (Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.) Hakuna kitu au mtu yeyote yule anayeweza kumzuia Baba yetu wa mbinguni asifanye jambo lolote, na kwa hiyo anaweza kutumia njia yoyote ile ili kuwafariji wale wanaompenda. Hivyo, tunaweza kuwafariji waamini wenzetu walio “katika namna yoyote ya dhiki.” Tunaweza kufanya hivyo “kupitia faraja ambayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.” Hilo linaonyesha vizuri kama nini kwamba Yehova ana uwezo usio na kifani wa kuwafariji wale wanaokata tamaa!

Kuvumilia Mambo Yanayosababisha Huzuni

6. Toa mifano ya mambo ambayo yanaweza kusababisha huzuni.

6 Tunahitaji faraja katika hali mbalimbali za maisha. Moja kati ya sababu kubwa zaidi zinazosababisha huzuni ni kifo cha mpendwa wetu, hasa kifo cha mwenzi wa ndoa mpendwa au mtoto. Mtu anaweza pia kuhitaji faraja anapobaguliwa. Mtu anaweza kuhitaji kufarijiwa kwa sababu ya afya mbaya, uzee, umaskini, matatizo ya ndoa, au hali za ulimwengu zenye kuhuzunisha.

7. (a) Katika hali zenye kuhuzunisha, tunahitaji faraja ya aina gani? (b) Yehova anaweza kufanya nini ili kuponya moyo “uliovunjika na kupondwa”?

7 Katika nyakati za huzuni, huenda tukahitaji faraja inayotuliza moyo, akili, hisia, na pia kuboresha afya yetu ya kimwili na ya kiroho. Kwa mfano, fikiria moyo. Neno la Mungu linasema kwamba moyo wetu unaweza ‘kuvunjika na kupondwa.’ (Zab. 51:17) Bila shaka, Yehova ana uwezo wa kuishughulikia hali hiyo, kwa sababu “anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.” (Zab. 147:3) Hata katika hali ngumu, Mungu anaweza kuutuliza moyo uliovunjika ikiwa tunasali kwake tukiwa na imani kamili na kushika amri zake.—Soma 1 Yohana 3:19-22; 5:14, 15.

8. Tunapokuwa na hangaiko la akilini, Yehova anaweza kutusaidia jinsi gani?

8 Mara nyingi akili yetu inahitaji kufarijiwa kwa sababu ya majaribu mbalimbali yanayosababishwa na hangaiko kubwa la akilini. Inaelekea kwamba hatuwezi kuvumilia majaribu hayo ya imani kwa nguvu zetu wenyewe. Hata hivyo, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Fikira zangu zinazofadhaisha zilipokuwa nyingi ndani yangu, faraja zako mwenyewe zilianza kuikumbatia nafsi yangu.” (Zab. 94:19) Zaidi ya hayo, Paulo aliandika hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Flp. 4:6, 7) Kusoma na kutafakari kuhusu Maandiko kunaweza kutusaidia sana kukabiliana na hangaiko la akilini.—2 Tim. 3:15-17.

9. Tunaweza kukabiliana jinsi gani na hangaiko la akilini?

9 Nyakati nyingine, tunaweza kuvunjika moyo sana hivi kwamba tunakuwa katika hatari ya kuwa na hisia zisizofaa. Labda tunahisi kwamba hatuwezi kutimiza daraka fulani la Kimaandiko au pendeleo fulani la utumishi. Katika hali hiyo pia, Yehova anaweza kutufariji na kutusaidia. Kwa mfano: Yoshua alipopewa daraka la kuwaongoza Waisraeli kupigana na mataifa adui yenye nguvu, Musa aliwaambia watu hivi: “Iweni hodari na wenye nguvu. Usiogope wala kushtuka mbele yao, kwa sababu Yehova Mungu wako ndiye anayepiga mwendo pamoja nawe. Hatakutupa wala kukuacha kabisa.” (Kum. 31:6) Kwa msaada wa Yehova, Yoshua aliweza kuwaongoza watu wa Mungu katika Nchi ya Ahadi na kuwashinda maadui wao wote. Mapema kwenye Bahari Nyekundu, Mungu alimsaidia Musa vivyo hivyo.—Kut. 14:13, 14, 29-31.

10. Ni msaada gani tunaoweza kupata ikiwa afya yetu ya kimwili inadhoofika kwa sababu ya huzuni?

10 Matukio yenye kuhuzunisha yanaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya afya yetu ya kimwili. Bila shaka, kula vizuri, kupumzika vya kutosha, kufanya mazoezi ya viungo, na kuwa safi kimwili kunaweza kutusaidia kuwa na afya nzuri. Pia, kutafakari juu ya mambo ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao, kunaweza kutusaidia kuwa na afya nzuri ya kimwili. Hivyo, tunapopambana na hali fulani yenye kuhuzunisha ni vizuri kukumbuka mambo ambayo Paulo alipitia maishani na maneno yake yafuatayo yenye kutia moyo: “Tunakazwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kuweza kusonga; tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa; tunateswa, lakini hatuachwi kabisa bila msaada; tunaangushwa chini, lakini hatuangamizwi.”—2 Kor. 4:8, 9.

11. Tunaweza kufanya nini tunapoona kwamba hali yetu ya kiroho inadhoofika?

11 Majaribu mengine yanaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya afya yetu ya kiroho. Katika hali hii pia, Yehova anaweza kutusaidia. Neno lake linatuhakikishia hivi: “Yehova anawategemeza wote wanaoanguka, naye anawainua wote ambao wameinama chini.” (Zab. 145:14) Tukiona kwamba afya yetu ya kiroho inadhoofika, tunapaswa kuwaomba wazee Wakristo watusaidie. (Yak. 5:14, 15) Na tukiendelea kukumbuka tumaini letu la Kimaandiko la uzima wa milele, tunaweza kuvumilia imani yetu inapojaribiwa.—Yoh. 17:3.

Mifano Inayoonyesha Jinsi Mungu Anavyotufariji

12. Yehova alimfariji Abrahamu jinsi gani?

12 Mtunga-zaburi mmoja aliyeongozwa na roho ya Mungu alisema hivi: “Ulikumbuke neno lako kwa mtumishi wako, ambalo [Yehova] umenifanya nilingojee. Hii ndiyo faraja yangu katika mateso yangu, kwa maana maneno yako mwenyewe yamenihifadhi hai.” (Zab. 119:49, 50) Leo, tuna Neno la Yehova lililoandikwa, ambalo lina mifano mingi inayoonyesha jinsi Mungu alivyowafariji watumishi wake. Kwa mfano, huenda Abrahamu alihuzunika alipojua kwamba Yehova angeharibu Sodoma na Gomora. Mzee huyo wa ukoo mwaminifu alimuuliza Mungu hivi: “Je, kweli utafagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu?” Yehova alimfariji Abrahamu kwa kumhakikishia kwamba ikiwa watu 50 tu waadilifu wangepatikana, Hangeharibu jiji la Sodoma. Hata hivyo, Abrahamu alimuuliza tena Yehova mara tano zaidi: Namna gani ikiwa kuna watu waadilifu 45? 40? 30? 20? 10 tu? Akiwa mwenye subira sana na mwenye fadhili, kila mara Yehova alimhakikishia Abrahamu kwamba jiji la Sodoma halingeharibiwa. Ingawa eneo hilo halikuwa hata na watu 10 waadilifu, Yehova alimlinda Loti na binti zake.—Mwa. 18:22-32; 19:15, 16, 26.

13. Hana alionyesha jinsi gani kwamba alimtegemea Yehova?

13 Hana, mke wa Elkana, alitamani sana kupata mtoto. Lakini alikuwa tasa, na jambo hilo lilimhuzunisha. Alisali kwa Yehova kuhusu hilo, na Kuhani Mkuu Eli akamwambia hivi: “Mungu wa Israeli akupe ombi lako.” Maneno hayo yalimfariji Hana, “na uso wake haukuonyesha tena kuhangaika.” (1 Sam. 1:8, 17, 18) Hana alimtegemea Yehova, na akiwa na uhakika aliacha mambo mikononi mwa Yehova. Ingawa hakujua angepata matokeo gani, Hana alipata amani ya moyoni. Baada ya muda, Yehova alijibu sala yake. Alipata mimba na kuzaa mwana, na akamwita jina lake Samweli.—1 Sam. 1:20.

14. Kwa nini Daudi alihitaji kufarijiwa, na alimgeukia nani ili kupata faraja?

14 Mfalme Daudi wa taifa la kale la Israeli ni mfano mwingine wa mtu aliyefarijiwa na Mungu. Kwa kuwa Yehova “huona jinsi moyo ulivyo,” alipomchagua Daudi kuwa mfalme wa wakati ujao wa Israeli, alijua kwamba Daudi alikuwa mnyoofu na alijitoa kabisa kwa ajili ya ibada ya kweli. (1 Sam. 16:7; 2 Sam. 5:10) Hata hivyo, baadaye, Daudi alifanya uzinzi na Bath-sheba na akajaribu kuficha dhambi hiyo kwa kupanga njama ili mume wa Bath-sheba auawe. Daudi alipotambua uzito wa dhambi yake, alisali hivi kwa Yehova: “Ufutilie mbali makosa yangu kulingana na wingi wa rehema zako. Unioshe kabisa kutokana na kosa langu, na kunitakasa kutokana na dhambi yangu. Kwa maana mimi mwenyewe nayajua makosa yangu, na dhambi yangu iko mbele yangu daima.” (Zab. 51:1-3) Daudi alitubu kikweli, na Yehova akamsamehe. Hata hivyo, Daudi alilazimika kukabiliana na matokeo mabaya ya kosa lake. (2 Sam. 12:9-12) Lakini, rehema za Yehova zilimfariji mtumishi wake huyo mnyenyekevu.

15. Ni msaada gani ambao Yehova alimpa Yesu kabla tu ya kifo chake?

15 Alipokuwa duniani, Yesu alipambana na hali nyingi ngumu. Mungu aliruhusu majaribu hayo ya imani, na Yesu alidumisha utimilifu wake akiwa mwanadamu mkamilifu na sikuzote alimtegemea Yehova na kutetea enzi Yake kuu. Alipokuwa karibu kusalitiwa na kuuawa, Yesu alisali hivi kwa Yehova: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” Kisha, malaika akamtokea Yesu na kumtia nguvu. (Luka 22:42, 43) Mungu alimfariji Yesu, akamtia nguvu, na kumpa msaada ambao alihitaji wakati huo.

16. Mungu anaweza kutusaidia jinsi gani uhai wetu ukiwa hatarini kwa sababu ya utimilifu wetu?

16 Yehova anaweza na atatusaidia kudumisha utimilifu wetu kwake hata ikiwa uhai wetu utakuwa hatarini kwa sababu ya msimamo wetu imara tukiwa Wakristo. Zaidi ya hayo, tumaini la ufufuo linatufariji. Na tunatazamia kwa hamu kama nini siku ambayo adui wa mwisho, kifo, ‘atakapoangamizwa’! (1 Kor. 15:26) Watumishi washikamanifu wa Mungu ambao wamekufa, na pia watu wengine, wako katika kumbukumbu kamilifu la Yehova na watafufuliwa. (Yoh. 5:28, 29; Mdo. 24:15) Kuwa na uhakika katika ahadi ya Yehova ya ufufuo kunatufariji na kutupatia tumaini hakika nyakati za mateso.

17. Yehova anaweza kutufariji jinsi gani mpendwa wetu anapokufa?

17 Inafariji kama nini kujua kwamba wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa ili waishi katika ulimwengu mpya na mzuri ajabu usio na mambo yote yenye kusababisha huzuni leo! Na litakuwa pendeleo kama nini kwa “umati mkubwa” wa watumishi wa Yehova ambao wataokoka mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo kuwakaribisha na kuwafundisha wale watakaofufuliwa ili waishi duniani!—Ufu. 7:9, 10.

Chini Kuna Mikono ya Milele ya Mungu

18, 19. Watumishi wa Mungu wamefarijiwa jinsi gani wakati wanapoteswa?

18 Kwa maneno yenye nguvu na yenye kugusa moyo ya wimbo mmoja, Musa aliwahakikishia watu wa Israeli hivi: “Mungu wa nyakati za kale ni mahali pa kujificha, na chini kuna mikono yenye kudumu mpaka wakati usio na kipimo.” (Kum. 33:27) Baadaye, nabii Samweli aliwaambia Waisraeli hivi: “Msigeuke kando mwache kumtumikia Yehova, nanyi lazima mmtumikie Yehova kwa moyo wenu wote. . . . Yehova hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.” (1 Sam. 12:20-22) Ikiwa tutaendelea kushikamana na Yehova katika ibada ya kweli, yeye hatatuacha kamwe. Sikuzote atatupatia msaada ambao tunahitaji.

19 Katika siku hizi za mwisho zilizo hatari, Mungu anawasaidia na kuwafariji kabisa watu wake. Kwa zaidi ya karne moja, maelfu ya waamini wenzetu ulimwenguni pote wameteswa na kufungwa gerezani kwa sababu tu wanamtumikia Yehova. Mambo ambayo wamekabiliana nayo maishani yanathibitisha kwamba katika nyakati za majaribu, Yehova kwa kweli anawafariji watumishi wake. Kwa mfano, mmoja wa ndugu zetu katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti alihukumiwa kifungo cha miaka 23 gerezani kwa sababu ya imani yake. Hata hivyo, akiwa gerezani, aliendelea kupokea chakula cha kiroho ambacho kilimtia nguvu na kumfariji. Alisema hivi: “Kwa miaka yote hiyo, nilijifunza kumtegemea Yehova na alinitia nguvu.”—Soma 1 Petro 5:6, 7.

20. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatatuacha?

20 Hata tukipatwa na mambo yoyote yale wakati ujao, itakuwa vizuri tukikumbuka maneno haya yenye kufariji ya mtunga-zaburi: “Yehova hatawaacha watu wake.” (Zab. 94:14) Ingawa sisi binafsi tunahitaji kufarijiwa, tuna pendeleo kubwa pia la kuwafariji wengine. Kama tutakavyoona katika habari inayofuata, tunaweza kuwafariji wale wanaoomboleza katika ulimwengu huu wenye msukosuko.

Ungesema Nini?

• Taja mambo fulani ambayo yanaweza kusababisha huzuni.

• Yehova anawafariji watumishi wake jinsi gani?

• Ni nini kinachoweza kutufariji tukikabiliana na kifo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

JINSI YA KUKABILIANA NA MAMBO AMBAYO YANAWEZA KUWA NA UVUTANO JUU YA . . .

moyo wetu Zab. 147:3; 1 Yoh. 3:19-22; 5:14, 15

akili yetu Zab. 94:19; Flp. 4:6, 7

hisia zetu Kut. 14:13, 14; Kum. 31:6

afya yetu ya kimwili 2 Kor. 4:8, 9

afya yetu ya kiroho Zab. 145:14; Yak. 5:14, 15