Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Yosefo Ndiye Aliyekiandika?

Je, Kweli Yosefo Ndiye Aliyekiandika?

Katika Kitabu chake cha 20 cha Jewish Antiquities, mwanahistoria wa karne ya kwanza Flavio Yosefo anataja kifo cha “Yakobo, ndugu ya Yesu aliyeitwa Kristo.” Wasomi wengi wanaona kwamba maneno hayo ni ya kweli. Hata hivyo, wengine wanatilia shaka ukweli wa maneno mengine kumhusu Yesu katika kitabu hicho. Fungu hilo la maneno linalojulikana kama Testimonium Flavianum linasema hivi:

“Sasa, wakati kama huu kulikuwa na Yesu, mwanadamu mwenye hekima, ikiwa ni halali kumwita mwanadamu, kwa kuwa alikuwa mtendaji wa kazi za ajabu—na wengi walifurahia kumsikiliza akifundisha kweli. Aliwavutia Wayahudi na watu wengi wa Mataifa. Alikuwa Kristo; naye Pilato kwa kufuata shauri la wanaume wazee miongoni mwetu, akamhukumu kifo juu ya msalaba, wale waliompenda tangu mwanzoni hawakumwacha, kwa kuwa aliwatokea siku ya tatu akiwa hai, kama manabii wa Mungu walivyokuwa wametabiri mambo hayo na mengine mazuri elfu kumi kumhusu; na Wakristo walioitwa kwa jina lake, wangalipo leo.”—Josephus—The Complete Works, kilichotafsiriwa na William Whiston.

Tangu mwisho wa karne ya 16, kumekuwa na bishano kali kati ya wale wanaoamini kwamba maelezo hayo ni sahihi na wale wenye shaka kwamba Yosefo ndiye aliyeyaandika. Mwanahistoria Mfaransa na mtaalamu wa fasihi ya zamani, Serge Bardet, alijaribu kutafuta suluhisho la bishano hilo ambalo limedumu kwa zaidi ya karne nne. Alichapisha utafiti wake katika kitabu kinachoitwa Le Testimonium Flavianum—Examen historique considérations historiographiques (Ushuhuda wa Flavio—Uchunguzi wa Kihistoria Unaotegemea Mambo ya Zamani).

Yosefo hakuwa mwandishi Mkristo. Alikuwa mwanahistoria Myahudi; kwa hiyo, mabishano mengi yanahusu kusema kwamba Yesu ni “Kristo.” Bardet alipochunguza suala hilo, alidai kwamba cheo hicho kinapatana “kikamili kabisa na jinsi majina [hususa] ya watu yalivyoandikwa katika Kigiriki.” Bardet aliongezea kwamba kwa maoni ya wale Wakristo Wayahudi, “si kwamba haiwezekani kutumia neno Christos lililotumiwa na Yosefo” lakini jambo hilo linadokeza kwamba “kwa ujumla, wachambuzi wamekosea sana kwa kulipuuza jina hilo.”

Je, inawezekana kwamba maneno hayo yalitiwa chumvi na mlaghai fulani aliyeiga mtindo wa Yosefo wa kuandika? Akitegemea maandishi na ushahidi wa kihistoria, Bardet alifikia mkataa kwamba kujaribu kuiga mtindo wa Yosefo ni jambo lisilowezekana. Hakuna anayeweza kufanya hivyo isipokuwa mlaghai mwenye “kipawa kisicho na kifani katika historia yote cha kuiga mtindo wa kuandika,” yaani, angehitaji kuwa “Yosefo mwenyewe.”

Basi, kwa nini kuna ubishi mwingi? Akitaja chanzo cha tatizo, Bardet alisema wazi kwamba “kuna shaka kuhusu Testimonium—tofauti kabisa na maandishi mengi ya kale—na sababu ni kwamba watu wana shaka kuihusu.” Anaendelea kusema kwamba kwa karne nyingi maoni ya watu yamechochewa na “nia mbaya” badala ya kutegemea utafiti wa maandishi hayo unaothibitisha kwamba yako sahihi.

Hatujui kama uchunguzi wa Bardet utabadili maoni ya wasomi kuhusu Testimonium Flavianum. Uchunguzi huo umemsadikisha Pierre Geoltrain, mtaalamu maarufu wa dini ya Wayahudi iliyotegemea utamaduni wa Wagiriki na dini ya kale ya Kikristo. Kwa muda mrefu aliona kwamba Testimonium imepotoshwa, hata aliwadhihaki wale walioamini kwamba ni sahihi. Lakini alibadili maoni yake. Amefikia mkataa kwamba kazi ya Bardet ndiyo iliyobadili maoni yake. Sasa Geoltrain ametangaza kwamba “kuanzia sasa, mtu yeyote asithubutu kusema kwamba maandishi ya Yosefo ni ya ‘kutiliwa shaka.’”

Bila shaka, Mashahidi wa Yehova wana sababu zenye kusadikisha zaidi za kukubali kwamba Yesu ni Kristo, zinazopatikana katika Biblia yenyewe.—2 Tim.3:16.