Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kujitahidi Zaidi Kuwaonya Wengine?

Je, Unaweza Kujitahidi Zaidi Kuwaonya Wengine?

Sinema isiyo na sauti inayoitwa A Trip Down Market Street (Matembezi Sokoni) inawasisimua watazamaji kwa sababu inaonyesha shughuli za maisha mwanzoni mwa karne ya 20 huko San Francisco, Marekani. Watengenezaji wa sinema hiyo walifunga kamera ndogo upande wa mbele wa kigari kilichoning’inia kwenye nyaya na kupiga picha soko hilo lenye shughuli nyingi. Sinema hiyo inaonyesha magari ya kukokotwa na farasi, magari ya zamani, watu wakinunua bidhaa, na wengine wakiuza magazeti.

Inasikitisha kwamba huenda sinema hiyo ilitengenezwa Aprili 1906, muda mfupi tu kabla ya tetemeko la ardhi na moto uliozuka na kusababisha vifo vya maelfu ya watu na kuharibu sehemu kubwa ya jiji hilo. Inaonekana kwamba baadhi ya watu wenye uchangamfu walio katika sinema hiyo walikufa siku chache baadaye. Scott Miles, aliyekuwa na uhusiano wa kifamilia na mtengenezaji mmoja wa sinema hiyo anasema hivi: “Ninapowatazama watu hawa, hawajui msiba utakaowapata. Ninawasikitikia tu.”

Kwa ghafla, tetemeko la ardhi la mwaka wa 1906 na moto uliozuka uliharibu sehemu kubwa ya jiji la San Francisco

Tunaweza kuona uzito wa hali hiyo tunapoilinganisha na hali yetu leo. Sisi pia tunawasikitikia sana jirani zetu. Wanaendelea na shughuli zao bila kujua kwamba kuna msiba unaokuja, yaani, mitindo ya watu ya maisha na mfumo huu wa mambo utaharibiwa hivi karibuni. Tofauti na tetemeko la ardhi lisilotabirika, tuna muda mfupi wa kuwaonya jirani zetu kuhusu siku ya Yehova ya hukumu. Inaelekea kwamba unatumia muda fulani kila juma kuhubiri nyumba kwa nyumba. Lakini je, unaweza kujitahidi zaidi kuwaonya wengine?

YESU ALITUMIA KILA FURSA ALIYOPATA

Yesu alituwekea mfano bora kwa sababu alitumia kila fursa aliyopata kumhubiria kila mtu aliyekutana naye. Alimhubiria mkusanya-kodi barabarani na hata mwanamke aliyemkuta Yesu akipumzika mchana kwenye kisima. (Luka 19:1-5; Yoh. 4:5-10, 21-24) Hata alipokuwa akipumzika, Yesu alibadili mipango yake na kuwafundisha wengine kwa hiari. Huruma ilimchochea kuwahubiria jirani zake kwa bidii. (Marko 6:30-34) Wakristo huigaje mfano wa Yesu katika kuwaonya watu wanaokabili hatari leo?

WANATUMIA KILA FURSA WANAYOPATA

Melika anaishi katika jengo lenye ulinzi mkali. Wengi wa jirani zake ni wanafunzi kutoka nchi  nyingine lakini majina na namba zao za simu hazijaandikwa katika orodha ya wapangaji. Anatumia fursa ya pekee anayopata ili kuzungumza na wapangaji wenzake kuhusu Biblia katika chumba cha wageni na kwenye lifti. Anasema hivi: “Ninaliona hili kuwa eneo langu.” Melika hubeba machapisho ya lugha nyingi, na wengi hukubali trakti na magazeti. Anawahimiza pia wachunguze Tovuti yetu ya jw.org. Ameanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia.

Sonia pia hujitahidi kumhubiria mtu yeyote yule. Ameajiriwa kwenye kliniki, na alijiwekea mradi wa kuwahubiria wafanyakazi wenzake. Kwanza, alijitahidi kujua mahitaji na mapendezi ya kila mmoja wao. Kisha, akatumia kipindi cha mapumziko ya mchana kuzungumza na kila mmoja wao kuhusu Biblia. Sonia alifaulu kuanzisha mafunzo mawili ya Biblia. Sasa anapanga kutumia wakati wake wa mapumziko kuongea na wagonjwa wanaosubiri kumwona daktari.

TUMIA KILA FURSA UNAYOPATA

Mtu aliyeokoka tetemeko la ardhi la mwaka wa 1906 alisema kwamba “hakuna jimbo au jiji lolote lililowahi kupatwa na msiba mbaya kama huo.” Hata hivyo, hakuna msiba wowote unaoweza kulinganishwa na siku ya kisasi inayokuja juu ya “wale wasiomjua Mungu.” (2 The. 1:8) Yehova anataka sana watu wabadili akili na mioyo yao na kutii onyo linalotolewa na Mashahidi wake.2 Pet. 3:9; Ufu. 14:6, 7.

Je, unaweza kutumia kila fursa unayopata kuhubiri unapokuwa katika shughuli zako za kila siku?

Una pendeleo la kufungua watu macho ili waone kwamba tunaishi katika nyakati za hatari na kuwasaidia wamtafute Yehova badala ya kufuatilia mapendezi yao ya kichoyo. (Sef. 2:2, 3) Je, unaweza kutumia kila fursa unayopata kuwahubiria wafanyakazi wenzako, jirani zako, na watu unaokutana nao kila siku? Je, unaweza kujitahidi zaidi kuwaonya wengine?