Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kudumisha Roho ya Kujidhabihu

Jinsi ya Kudumisha Roho ya Kujidhabihu

Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe.”​MT. 16:24.

1. Yesu aliwekaje mfano bora katika kujidhabihu?

YESU alipokuwa duniani aliweka mfano bora kabisa katika kujidhabihu. Alitanguliza mapenzi ya Mungu badala ya tamaa na mapendezi yake mwenyewe. (Yoh. 5:30) Kwa kuendelea kuwa mwaminifu mpaka alipokufa juu ya mti wa mateso, alithibitisha kwamba alikuwa tayari kujidhabihu mpaka mwisho.—Flp. 2:8.

2. Tunawezaje kuonyesha roho ya kujidhabihu, na kwa nini tuonyeshe roho hiyo?

2 Tukiwa wafuasi wa Yesu, tunahitaji pia kuonyesha roho ya kujidhabihu. Kuwa na roho ya kujidhabihu kunamaanisha nini? Kwa ufupi, ni kuacha kwa hiari mapendezi yako ili uwasaidie wengine. Kwa njia fulani, ni kinyume cha kuwa na ubinafsi. (Soma Mathayo 16:24.) Roho isiyo ya ubinafsi inaweza kutusaidia kutanguliza mapendezi na hisia za wengine badala ya hisia au mapendezi yetu. (Flp. 2:3, 4) Kwa kweli, Yesu alifundisha kwamba roho isiyo ya ubinafsi ni muhimu sana katika ibada yetu. Jinsi gani? Upendo wa Kikristo ni kati ya mambo yanayotuchochea kujidhabihu. Upendo ndiyo sifa kuu inayowatambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu. (Yoh. 13:34, 35) Hebu wazia baraka tunazofurahia kwa sababu ya kuwa sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote unaoonyesha roho ya kujidhabihu!

3. Ni nini kinachoweza kudhoofisha roho yetu ya kujidhabihu?

 3 Hata hivyo, tunakabili adui anayeweza kudhoofisha kwa hila roho yetu ya kujidhabihu. Adui huyo ni mwelekeo wetu wa kuwa na ubinafsi. Kumbuka jinsi Adamu na Hawa walivyoonyesha ubinafsi. Hawa alitenda kwa ubinafsi alipotamani kuwa kama Mungu. Naye Adamu alitamani kwa ubinafsi kumpendeza mke wake. (Mwa. 3:5, 6) Baada ya kuwashawishi Adamu na Hawa kuacha ibada ya kweli, Ibilisi aliendelea kuwashawishi watu kuwa na ubinafsi. Hata alijaribu kutumia njia hiyo kumshawishi Yesu. (Mt. 4:1-9) Leo, Shetani amefanikiwa kuwapotosha watu wengi na kuwachochea waonyeshe ubinafsi kwa njia nyingi. Tunahitaji kuwa waangalifu kwa kuwa roho ya ubinafsi imeenea sana leo na inaweza kutuathiri.—Efe. 2:2.

4. (a) Je, tunaweza kuondoa mielekeo ya ubinafsi? Eleza. (b) Tutachunguza maswali gani?

4 Ubinafsi unaweza kulinganishwa na kutu. Chuma kinaweza kuanza kuliwa na kutu katika mazingira yenye unyevunyevu. Ni hatari sana kupuuza kutu kwa sababu inaweza kuharibu kabisa chuma. Vivyo hivyo, ingawa hatuwezi kuondoa hali yetu ya kutokamilika na mielekeo ya ubinafsi, ni lazima tuwe macho ili kuona hatari na kuendelea kupambana na mielekeo hiyo. (1 Kor. 9:26, 27) Tutajuaje ikiwa tumeanza kuwa na ubinafsi? Na tunawezaje kusitawisha kwa kadiri kubwa roho ya kujidhabihu?

TUMIA BIBLIA KUCHUNGUZA IKIWA UNA UBINAFSI

5. (a) Biblia ni kama kioo katika maana gani? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 7.) (b) Ni lazima tuepuke nini tunapojichunguza ili kuona ikiwa tuna ubinafsi?

5 Kama vile tunavyoweza kutumia kioo kutazama sura yetu, ndivyo tunavyoweza kutumia Biblia kuchunguza utu wetu wa ndani na kurekebisha kasoro yoyote. (Soma Yakobo 1:22-25.) Hata hivyo, kioo kinaweza tu kutusaidia tukikitumia kwa njia inayofaa. Kwa mfano, tukijitazama haraka-haraka katika kioo huenda tusione kasoro ndogo tulizo nazo ambazo ni mbaya sana. Na tukisimama mahali pasipofaa tunapojitazama huenda tukamwona mtu mwingine katika kioo. Vivyo hivyo, ili tutumie Biblia kuona kasoro yoyote, kama vile ubinafsi, hatupaswi kuisoma kijuu-juu tu au kuitumia kuona makosa ya mtu mwingine.

6. ‘Tunadumu’ katika sheria kamilifu jinsi gani?

6 Kwa mfano, tunaweza kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida, au hata kila siku, na bado tusitambue kwamba tumeanza kuwa na ubinafsi. Inawezekanaje? Fikiria hili: Si kwamba mtu anayetajwa na Yakobo hakujitazama kwa makini katika kioo. Yakobo aliandika kwamba mtu huyo “hujitazama.” Yakobo alitumia neno la Kigiriki linalomaanisha kujichunguza kwa undani au kwa makini. Basi mtu huyo alikuwa na tatizo gani? Yakobo aliendelea kusema hivi: “Huenda zake na kusahau mara moja yeye ni mtu wa namna gani.” Ndiyo, mtu huyo huenda zake baada ya kujitazama katika kioo lakini harekebishi kasoro anayoona. Hata hivyo, mtu mwenye furaha ‘hachunguzi tu ndani ya sheria kamilifu’ bali pia “hudumu katika hiyo.” Badala ya kuiacha sheria kamilifu ya Neno la Mungu, mtu huyo hudumu katika sheria hiyo kwa kuendelea kufuata mafundisho yake. Yesu alitaja jambo kama hilo aliposema hivi: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.”​—Yoh. 8:31.

7. Tunaweza kuitumiaje Biblia kuchunguza ikiwa tuna mwelekeo wa ubinafsi?

7 Kwa hiyo, ili ufanikiwe kupambana na mwelekeo wowote wa ubinafsi, ni lazima usome kwanza Neno la Mungu kwa makini.  Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kutambua mambo unayohitaji kurekebisha. Lakini unahitaji kufanya jambo lingine. Chimba zaidi kwa kufanya utafiti. Baada ya kuelewa kikamili simulizi la Biblia, jiweke katika hali hiyo kwa kujiuliza maswali kama haya: ‘Ningetendaje katika hali hii? Je, kweli ningetenda kwa njia inayofaa?’ Baada ya kutafakari ulichosoma, ni muhimu zaidi kujitahidi kutumia habari hiyo. (Mt. 7:24, 25) Acheni tuchunguze jinsi masimulizi kuhusu Mfalme Sauli na mtume Petro yanavyoweza kutusaidia kudumisha roho ya kujidhabihu.

JIFUNZE KUTOKANA NA MFANO MBAYA WA MFALME SAULI

8. Sauli alikuwa na mtazamo gani alipoanza kutawala? Alionyeshaje mtazamo huo?

8 Mfalme Sauli wa Israeli ni mfano mbaya wenye onyo unaoonyesha jinsi ubinafsi unavyoweza kuharibu roho yetu ya kujidhabihu. Sauli alipoanza kutawala alikuwa mwenye kiasi na mnyenyekevu. (1 Sam. 9:21) Hakuwaadhibu Waisraeli waliopinga ufalme wake ijapokuwa angeweza kufanya hivyo ili kutetea cheo alichopewa na Mungu. (1 Sam. 10:27) Mfalme Sauli alikubali mwongozo wa roho ya Mungu alipowaongoza Waisraeli kushinda vita dhidi ya Waamoni. Baada ya kushinda vita hivyo, kwa unyenyekevu alimsifu Yehova.—1 Sam. 11:6, 11-13.

9. Sauli alianzaje kusitawisha mawazo ya ubinafsi?

9 Baadaye, Sauli aliruhusu mawazo ya ubinafsi na kiburi yamwathiri kama kutu inavyoathiri chuma. Alipowashinda Waamaleki vitani, alitanguliza tamaa yake badala ya kumtii Yehova. Akichochewa na pupa, Sauli alichukua nyara badala ya kuziharibu kama Mungu alivyomwagiza. Na kwa kiburi Sauli akajijengea mnara wa ukumbusho. (1 Sam. 15:3, 9, 12) Nabii Samweli alipomwambia kwamba Yehova hakupendezwa na jambo hilo, Sauli alijaribu kujitetea kwa kutaja sehemu ya amri ya Mungu aliyotii na kuwalaumu wengine kwa sababu ya makosa yake. (1 Sam. 15:16-21) Pia, kiburi kilimfanya Sauli ahangaikie zaidi kuheshimiwa na watu badala ya kumpendeza Mungu. (1 Sam. 15:30) Tunawezaje kutumia simulizi hilo kumhusu Sauli kama kioo cha kutusaidia kudumisha roho ya kujidhabihu?

10, 11. (a) Kisa cha Sauli kinatufundisha nini kuhusu kudumisha roho ya kujidhabihu? (b) Tunawezaje kuepuka kuiga mfano mbaya wa Sauli?

10 Kwanza, kisa cha Sauli kinaonyesha kwamba hatupaswi kuwa na mtazamo wa kutojali na kufikiri kwamba kwa kuwa zamani tulionyesha roho ya kujidhabihu, basi tutaendelea kuwa nayo. (1 Tim. 4:10) Kumbuka kwamba Sauli alitenda kwa njia inayofaa mwanzoni na kumpendeza Mungu, hata hivyo, hakung’oa mielekeo ya ubinafsi iliyoanza kutia mizizi moyoni mwake. Mwishowe, Yehova alimkataa Sauli kwa sababu ya kutotii.

11 Pili, tunapaswa kuwa waangalifu kutokazia fikira mambo mazuri tunayofanya na kupuuza mambo tunayohitaji kurekebisha. Kufanya hivyo ni kama kujitazama kwenye kioo na kufurahia mavazi yetu mapya na kukosa kuona uchafu ulio usoni. Hata ikiwa hatuna kiburi au ubinafsi kama Sauli, tunapaswa kujitahidi kuepuka mwelekeo wowote utakaotufanya tuige mfano wake mbaya. Tunaposhauriwa, tunapaswa kuepuka kutetea mwenendo wetu usiofaa, kupunguza uzito wa tatizo, au kuwalaumu wengine. Badala ya kuwa kama Sauli, itafaa zaidi tukikubali shauri.—Soma Zaburi 141:5.

12. Roho ya kujidhabihu itatusaidiaje tukitenda dhambi nzito?

12 Hata hivyo, namna gani ikiwa tumetenda dhambi nzito? Sauli hakupona kiroho kwa kuwa alitaka watu waendelee  kumheshimu. Hata hivyo, roho ya kujidhabihu inaweza kutusaidia kushinda aibu na kutafuta msaada tunaohitaji. (Met. 28:13; Yak. 5:14-16) Kwa mfano, ndugu mmoja alianza kutazama ponografia alipokuwa na umri wa miaka 12 na aliendelea kufanya hivyo kisiri kwa zaidi ya miaka kumi. Anasema hivi: “Ilikuwa vigumu sana kumwambia mke wangu na wazee wa kutaniko jambo nililokuwa nikifanya. Lakini sasa, baada ya kuwaambia ninahisi kwamba mzigo mzito umeondolewa kutoka kwenye mabega yangu. Baadhi ya marafiki wangu walivunjika moyo nilipoondolewa kuwa mtumishi wa huduma. Hata hivyo, ninajua kwamba Yehova anapendezwa zaidi na utumishi wangu sasa kuliko nilipokuwa nikitazama ponografia. Jambo muhimu zaidi ni jinsi Yehova anavyoniona.”

PETRO ASHINDA UBINAFSI

13, 14. Petro alionyeshaje mielekeo ya ubinafsi?

13 Mtume Petro alionyesha roho ya kujidhabihu alipozoezwa na Yesu. (Luka 5:3-11) Hata hivyo, alihitaji kupambana na mielekeo ya ubinafsi. Kwa mfano, alikasirika sana mtume Yakobo na Yohana walipopanga njama ya kupata vyeo vikubwa kando ya Yesu katika Ufalme wa Mungu. Huenda Petro alifikiri kwamba alistahili cheo kikubwa kwa kuwa tayari Yesu alisema kwamba Petro angekuwa na mgawo wa pekee. (Mt. 16:18, 19) Kwa vyovyote vile, Yesu aliwaonya Yakobo na Yohana, na pia Petro na mitume wengine kwamba hawapaswi kuonyesha ubinafsi kwa ‘kupiga ubwana juu ya’ ndugu zao.​—Marko 10:35-45.

14 Hata baada ya Yesu kujitahidi kurekebisha maoni ya Petro, bado Petro aliendelea kujiona kuwa bora. Yesu alipowaambia mitume kwamba wangemwacha kwa kipindi fulani, Petro aliwadharau wengine na kujikweza kwa kudai kwamba yeye peke yake ndiye angebaki mwaminifu. (Mt. 26:31-33) Hata hivyo, mtazamo wake wa kujiamini haukufaa kwa sababu usiku huo alishindwa kuonyesha roho ya kujidhabihu. Petro alipojaribu kujilinda, alimkana Yesu mara tatu.—Mt. 26:69-75.

15. Kwa ujumla, kwa nini mfano wa Petro unatutia moyo?

15 Petro anatutia moyo licha ya kwamba  alipambana na hata kushindwa na mielekeo ya ubinafsi. Kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, Petro alijitahidi na kufanikiwa kushinda mielekeo yake isiyofaa na hivyo kuonyesha roho ya kujizuia na upendo wa kujidhabihu. (Gal. 5:22, 23) Alivumilia majaribu ambayo huenda yalikuwa makali zaidi kuliko yale yaliyomfanya ajikwae mwanzoni. Itikio la Petro aliposhauriwa hadharani na mtume Paulo linaonyesha kwamba alikuwa mnyenyekevu. (Gal. 2:11-14) Hata baada ya kushauriwa, Petro hakuwa na kinyongo moyoni na kuhisi kwamba Paulo alimdharau. Petro aliendelea kumpenda Paulo. (2 Pet. 3:15) Mfano wa Petro unaweza kutusaidia kusitawisha roho ya kujidhabihu.

Petro aliitikiaje aliposhauriwa? Je, tungeitikia vivyo hivyo?(Tazama fungu la 15)

16. Tunawezaje kuonyesha roho ya kujidhabihu tunapokabili hali ngumu?

16 Fikiria jinsi unavyotenda unapokabili hali ngumu. Petro na mitume wengine walipofungwa gerezani na kupigwa viboko kwa sababu ya kuhubiri, walishangilia “kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake [Yesu].” (Mdo. 5:41) Wewe pia unaweza kuyaona mateso kuwa nafasi ya kumwiga Petro na kufuata hatua za Yesu kwa kuonyesha roho ya kujidhabihu. (Soma 1 Petro 2:20, 21.) Mtazamo huo unaweza kukusaidia hata wazee wanapokutia nidhamu unayohitaji. Unapotiwa nidhamu, iga mfano wa Petro badala ya kuudhika.​—Mhu. 7:9.

17, 18. (a) Tunaweza kujiuliza swali gani kuhusu miradi yetu ya kiroho? (b) Tunaweza kufanya nini tukigundua kwamba kwa kadiri fulani tuna mwelekeo wa ubinafsi moyoni mwetu?

17 Unaweza pia kunufaika kutokana na mfano wa Petro inapohusu miradi ya kiroho. Unaweza kufuatilia miradi hiyo kwa njia inayoonyesha roho ya kujidhabihu. Hata hivyo, uwe mwangalifu usifanye hivyo ili kupata umashuhuri. Jiulize hivi: ‘Je, inawezekana kwamba ninatamani kuboresha au kuongeza utumishi wangu kwa Yehova ili niwe mashuhuri au kupata mamlaka, mtazamo ambao huenda Yakobo na Yohana walikuwa nao?’

18 Ukigundua kwamba una mwelekeo wa ubinafsi moyoni mwako, mwombe Yehova akusaidie kurekebisha maoni na hisia zako; kisha ujitahidi kukazia fikira utukufu wake badala ya kujitafutia utukufu. (Zab. 86:11) Unaweza pia kufuatilia miradi ambayo haitakufanya uwe mashuhuri. Kwa mfano, unaweza kusitawisha kikamili zaidi sifa fulani ya tunda la roho ambayo si rahisi kwako kuonyesha. Au ikiwa unatayarisha kwa bidii migawo yako kutanikoni lakini hupendi sana kufanya usafi wa Jumba la Ufalme, unaweza kujiwekea lengo au mradi wa kutumia shauri la Waroma 12:16.​—Soma.

19. Tunaweza kufanya nini ili tusivunjike moyo tunapotumia Neno la Mungu kujitazama kama kioo?

19 Huenda tukavunjika moyo tunapojichunguza kwa makini katika kioo cha Neno la Mungu na kuona kasoro kama vile ubinafsi. Ukihisi hivyo, mkumbuke mtu mwenye furaha anayetajwa na Yakobo. Yakobo hakusema mtu huyo alirekebisha haraka kadiri gani matatizo aliyoona au ikiwa aliweza kurekebisha kila kasoro; badala yake, Yakobo anasema kwamba mtu huyo ‘alidumu ndani ya sheria kamilifu.’ (Yak. 1:25) Mtu huyo alikumbuka alichoona alipojitazama katika kioo, naye aliendelea kufanya marekebisho. Naam, endelea kuwa na maoni yanayofaa na yenye usawaziko kuhusu hali yako ya kutokamilika. (Soma Mhubiri 7:20.) Endelea kuichunguza sheria kamilifu na ujitahidi kudumisha roho yako ya kujidhabihu. Yehova yuko tayari kukusaidia, kama tu anavyowasaidia ndugu zetu wengi ambao, ingawa si wakamilifu, wanaweza kupata na tayari wana kibali na baraka za Mungu.