Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Gogu wa Magogu anayetajwa katika kitabu cha Ezekieli ni nani?

Kwa miaka mingi, machapisho yetu yalieleza kuwa Gogu wa Magogu ni jina alilopewa Shetani Ibilisi baada ya kufukuzwa mbinguni. Ufafanuzi huo ulitegemea maelezo ya kitabu cha Ufunuo yanayomtambulisha Shetani Ibilisi kuwa kiongozi wa mashambulizi ya ulimwenguni pote dhidi ya watu wa Mungu. (Ufu. 12:1-17) Kwa hiyo, ilidhaniwa kwamba Gogu ni jina lingine la kinabii la Shetani.

Hata hivyo, ufafanuzi huo umezusha maswali fulani muhimu. Kwa nini? Fikiria hili: Akizungumza kuhusu kushindwa kwa Gogu, Yehova anasema hivi: “Nitakutoa uwe chakula cha ndege wenye kuwinda, na ndege wa kila namna ya bawa, na wanyama wa mwituni.” (Eze. 39:4) Kisha, Yehova anaongezea: “Na itatukia kwamba katika siku hiyo, nitampa Gogu mahali huko, kaburi katika Israeli . . . Nao watalazimika kumzika Gogu na umati wake wote huko.” (Eze. 39:11) Lakini inawezekanaje kiumbe wa roho kuliwa na “ndege wa kila namna ya bawa, na wanyama wa mwituni”? Shetani anawezaje kupewa “kaburi” hapa duniani? Biblia inaonyesha wazi kwamba Shetani atafungwa ndani ya abiso kwa miaka 1,000, na si kuliwa wala kuzikwa.—Ufu. 20:1, 2.

Tunaambiwa kuwa mwishoni mwa miaka 1,000, Shetani atafunguliwa kutoka ndani ya abiso, “naye ataenda kuyapotosha yale mataifa yaliyo katika pembe nne za dunia, Gogu na Magogu, kuwakusanya pamoja kwa ajili ya vita.” (Ufu. 20:8) Basi Shetani anawezaje kumpotosha Gogu ikiwa yeye mwenyewe ndiye Gogu? Hivyo “Gogu” anayetajwa katika unabii wa Ezekieli au kitabu cha Ufunuo si Shetani.

Basi Gogu wa Magogu ni nani? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kuchunguza Maandiko ili tujue ni nani anayewashambulia watu wa Mungu. Biblia haizungumzii tu shambulizi la ‘Gogu wa Magogu,’ bali inataja pia shambulizi la “mfalme wa kaskazini” na la “wafalme wa dunia.” (Eze. 38:2, 10-13; Dan. 11:40, 44, 45; Ufu. 17:14; 19:19) Je, hayo ni mashambulizi tofauti? Huenda sivyo. Inaonekana Biblia inazungumzia shambulizi lilelile lakini kwa kutumia majina tofauti. Kwa nini tunasema hivyo? Kwa sababu Maandiko yanatueleza kwamba mataifa yote ya dunia yatahusika katika shambulizi hilo la mwisho ambalo litachochea kuanza kwa vita vya Har–Magedoni.—Ufu. 16:14, 16.

Tunapolinganisha Maandiko yote hayo yanayohusu shambulizi la mwisho dhidi ya watu wa Mungu, ni wazi kwamba Gogu wa Magogu si Shetani bali ni muungano wa mataifa. Je, muungano huo utaongozwa na “mfalme wa kaskazini” wa mfano? Hatuna uhakika kuhusu jambo hilo. Lakini wazo hilo linapatana na jambo ambalo Yehova anasema kuhusu Gogu: “Nawe hakika utakuja kutoka mahali pako, kutoka sehemu za mbali zaidi za kaskazini, wewe na vikundi vingi vya watu pamoja nawe, hao wote wakiwa wamepanda farasi, kutaniko kubwa, naam, jeshi kubwa sana.”—Eze. 38:6, 15.

Vivyo hivyo, nabii Danieli, aliyeishi wakati mmoja na Ezekieli, anasema hivi kuhusu mfalme wa kaskazini: “Lakini kutakuwako habari ambazo zitamsumbua, kutoka upande wa mashariki na kutoka kaskazini, naye ataenda kwa ghadhabu kubwa ili kuangamiza na kuharibu wengi. Naye atasimamisha mahema yake makubwa kati ya ile bahari kuu na mlima mtakatifu wa lile Pambo; naye ataenda mpaka mwisho wake, wala hatakuwa na wa kumsaidia.” (Dan. 11:44, 45) Jambo hilo linapatana na kile ambacho kitabu cha Ezekieli kinasema kuhusu utendaji wa Gogu.—Eze. 38:8-12, 16.

Ni nini kitakachotokea baada ya shambulizi hilo? Danieli anatueleza hivi: “Na Mikaeli [Yesu Kristo] atasimama wakati huo [wa Har–Magedoni], yule mkuu anayesimama [tangu 1914] kwa ajili ya wana wa watu wako. Na kutakuwa na wakati wa taabu [dhiki kuu] ambayo haijapata kutokea tangu kuwapo kwa taifa lolote mpaka wakati huo. Na wakati huo watu wako wataponyoka, kila mmoja anayepatikana ameandikwa katika kile kitabu.” (Dan. 12:1) Jambo hilo ambalo Yesu anafanya linafafanuliwa pia kwenye Ufunuo 19:11-21.

Lakini “Gogu na Magogu” anayetajwa kwenye Ufunuo 20:8 ni nani? Wakati wa jaribu la mwisho ambalo litatokea mwishoni mwa Miaka Elfu Moja, wale watakaomwasi Yehova wataonyesha mtazamo wa uuaji kama ule wa ‘Gogu wa Magogu,’ yaani yale mataifa yatakayowashambulia watu wa Mungu mwishoni mwa dhiki kuu. Makundi yote mawili yatapata matokeo yaleyale, yaani, yataangamizwa milele! (Ufu. 19:20, 21; 20:9) Hivyo basi, inafaa kwamba wale wote watakaoasi mwishoni mwa Miaka Elfu Moja wanaitwa “Gogu na Magogu.”

Tukiwa wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu, tunasubiri kwa hamu kuona ni nani atakayekuwa “mfalme wa kaskazini” hivi karibuni. Hata hivyo, haidhuru ni nani atakayeongoza muungano huo wa mataifa, sisi tuna uhakika na mambo mawili: (1) Gogu wa Magogu na majeshi yake watashindwa na kuangamizwa; na (2) Mfalme wetu anayetawala, Yesu Kristo, atawaokoa watu wa Mungu na kuwaingiza katika ulimwengu mpya wenye amani na usalama wa kweli.—Ufu. 7:14-17.