Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Kukumbuka Upendo Wangu wa Kwanza Kumenisaidia Kuvumilia

Kukumbuka Upendo Wangu wa Kwanza Kumenisaidia Kuvumilia

ILIKUWA mwanzo wa majira ya joto mwaka wa 1970. Nilikuwa nimelazwa katika Hospitali Kuu ya Valley Forge, Phoenixville, Pennsylvania, Marekani. Muuguzi wa kiume alinipima shinikizo la damu kila baada ya nusu saa. Nilikuwa mwanajeshi mwenye umri wa miaka 20 na nilisumbuliwa na ugonjwa mbaya sana wa kuambukiza. Muuguzi huyo, ambaye alinizidi umri kidogo, alikuwa mwenye wasiwasi sana. Shinikizo langu la damu lilipoendelea kushuka, nilimwambia, “Hujawahi kumwona mtu akifa, sivyo?” Akiwa amehuzunika alinijibu hivi, “Sijawahi.”

Sikuwa na tumaini hata kidogo wakati huo. Ilikuwaje nikalazwa hospitali? Acheni niwasimulie kwa ufupi historia ya maisha yangu.

NAANZA KUSHUHUDIA MATOKEO YA VITA

Niliugua ugonjwa huo nilipokuwa mhudumu katika chumba cha upasuaji wakati wa vita vya Vietnam. Nilipenda kuwasaidia wagonjwa na wale waliojeruhiwa, na nilikuwa na lengo la kuwa daktari wa upasuaji. Niliwasili Vietnam mnamo Julai 1969. Kwa kuwa nilikuwa mfanyakazi mpya, nilipewa juma moja la kufahamu mazingira ya kazi na kuzoea joto kali.

Muda mfupi baada ya kufika kwenye kituo cha kazi, katika hospitali ya upasuaji iliyokuwa kwenye eneo la Delta ya Mekong, huko Dong Tam, helikopta nyingi zilizojaa majeruhi ziliwasili. Nilikuwa mzalendo na nilipenda sana kufanya kazi, hivyo nilitaka kuanza kazi mara moja. Majeruhi walitayarishwa na kupelekwa kwenye vyumba vidogo vyenye viyoyozi, vilivyojengwa kwa kuta za chuma, ambavyo vilitumiwa kama vyumba vya upasuaji. Kila chumba kilikuwa na daktari wa upasuaji, mtaalamu wa unusukaputi, muuguzi msaidizi, na muuguzi aliyesimamia shughuli nzima ya upasuaji, wote wakijitahidi kuokoa uhai wa watu. Niliona mizigo fulani iliyokuwa ndani ya mifuko myeusi ambayo haikuwa imepakuliwa kutoka kwenye helikopta. Niliambiwa kuwa mifuko hiyo ilikuwa na viungo vya miili ya wanajeshi waliolipuliwa na mabomu vitani. Hapo ndipo nilianza kushuhudia matokeo ya vita.

KUMTAFUTA MUNGU

Nilipokuwa kijana nilisikia kwa kiasi fulani kweli ambazo Mashahidi wa Yehova hufundisha

Nilipokuwa kijana, nilisikia kwa kiasi fulani kweli ambazo Mashahidi wa Yehova hufundisha. Mama yangu mpendwa alifundishwa Biblia na Mashahidi, lakini hakufanya maendeleo kufikia ubatizo. Nilifurahia sana kusikiliza mama yangu alipokuwa akijifunza. Siku moja nilipita karibu na Jumba la Ufalme pamoja na baba yangu wa kambo. Nilimuuliza, “Hilo ni nini?” Akajibu, “Usijihusishe kabisa na watu hao!” Kwa kuwa nilimpenda na kumwamini baba yangu wa kambo, nilifuata ushauri wake. Hivyo, niliacha kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova.

Baada ya kurudi kutoka Vietnam, nilianza kuhisi namhitaji Mungu katika maisha yangu. Kumbukumbu mbaya ziliniathiri kihisia. Ilionekana ni kana kwamba hakuna aliyeelewa kilichokuwa kikiendelea huko Vietnam. Nakumbuka watu waliandamana na kuwaita wanajeshi wa Marekani wauaji wa watoto kwa sababu ya ripoti za kuuawa kwa watoto wasio na hatia vitani.

Ili kutosheleza njaa yangu ya kiroho, nilianza kuhudhuria ibada za makanisa mbalimbali. Sikuzote nilimpenda Mungu lakini sikupendezwa na mambo niliyojionea kwenye makanisa. Hatimaye, nilienda kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova huko Delray Beach, Florida. Ilikuwa Jumapili, Februari 1971.

Nilipoingia, hotuba ya watu wote ilikuwa inakaribia kwisha, hivyo nilikaa kusikiliza funzo la Mnara wa Mlinzi lililofuata. Sikumbuki kilichozungumziwa katika funzo hilo, lakini bado ninakumbuka watoto wadogo wakifungua Biblia zao ili kusoma maandiko. Hilo lilinivutia sana! Nilisikiliza kwa makini na kuangalia kinachoendelea. Nilipokuwa nikiondoka Jumba la Ufalme Ndugu Jim Gardner, aliyekuwa na umri wa miaka 80 hivi, alinifuata. Alitoa kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele na kuniambia, “Chukua kitabu hiki tafadhali.” Tulipanga kukutana Alhamisi asubuhi ili kuanza kujifunza Biblia.

Usiku wa Jumapili hiyo nilipaswa kuwa kazini. Niliajiriwa kwenye hospitali binafsi huko Boca Raton, Florida, ambapo nilifanya kazi kwenye idara iliyoshughulikia hali za dharura. Zamu yangu ilianza saa tano usiku hadi saa moja asubuhi. Kwa kuwa usiku huo ulikuwa mtulivu, niliweza kusoma kitabu Kweli. Muuguzi mkuu alinifuata, akaninyang’anya kitabu, akatazama jalada lake na kuniambia kwa sauti kubwa, “Usiniambie unataka kujiunga na watu hawa!” Nilichukua kitabu changu na kumwambia, “Nimesoma nusu ya kitabu hiki, na inaonekana nitajiunga nao!” Aliondoka, na nikamaliza kusoma kitabu chote usiku huo.

Mwalimu wangu wa Biblia alikuwa Jim Gardner, ndugu mtiwa-mafuta aliyemfahamu Charles Taze Russell

Siku niliyoanza kujifunza na Ndugu Gardner nilimuuliza, “Kwa hiyo, tutajifunza nini?” Akanijibu, “Kile kitabu nilichokupa.” Nikamwambia, “Tayari nimemaliza kukisoma.” Ndugu Gardner alinijibu kwa upole, “Ni sawa, acha tuchunguze hii sura ya kwanza.” Nilishangaa kujua kumbe kuna mambo mengi sikuwa nimeyaelewa. Aliniambia nisome maandiko mengi kwenye Biblia yangu. Hatimaye nilijifunza kumhusu Mungu wa kweli, Yehova. Ndugu Gardner, ambaye nilimwita Jim, alinifundisha sura tatu za kitabu Kweli asubuhi hiyo. Kuanzia siku hiyo tulijifunza sura tatu kila Alhamisi asubuhi. Nilifurahia sana kujifunza. Ilikuwa baraka iliyoje kujifunza na ndugu huyo mtiwa-mafuta ambaye alifahamiana na Charles T. Russell!

Baada ya majuma machache, nilikubaliwa kuwa mhubiri wa habari njema. Jim alinisaidia kushughulikia mambo mengi yaliyonihangaisha, kutia ndani changamoto ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. (Mdo. 20:20) Jim alipoendelea kunisaidia, nilianza kuipenda kazi ya kuhubiri. Bado naona kuwa ni heshima kubwa sana kukabidhiwa huduma. Inafurahisha sana kuwa mfanyakazi mwenzi wa Mungu!—1 Kor. 3:9.

UPENDO WANGU WA KWANZA KWA YEHOVA

Acheni niwaeleze jambo fulani la kibinafsi, yaani, upendo wangu wa kwanza kwa Yehova. (Ufu. 2:4) Upendo huo umenisaidia nisilemewe na kumbukumbu mbaya za vita na majaribu mengine.—Isa. 65:17.

Kumpenda Yehova kumenisaidia nisilemewe na kumbukumbu mbaya za vita na majaribu mengine

Nilibatizwa Julai 1971 katika kusanyiko la wilaya lenye kichwa “Jina la Kimungu,” kwenye Uwanja wa Yankee

Ninakumbuka siku moja ya pekee mwaka wa 1971. Nilikuwa nimefukuzwa kwenye nyumba ambayo wazazi wangu walikuwa wameniruhusu niishi. Baba yangu wa kambo hakutaka Shahidi wa Yehova aishi kwenye nyumba yake. Sikuwa na pesa za kutosha wakati huo. Katika hospitali niliyofanya kazi nilipewa mshahara kila baada ya majuma mawili, na nilikuwa nimetumia karibu pesa zote kununua nguo kwa ajili ya utumishi ili kumwakilisha vizuri Yehova. Nilikuwa nimehifadhi kiasi fulani cha pesa, lakini zilikuwa kwenye benki huko Michigan, jimbo nililolelewa. Hivyo, ilibidi nilale kwenye gari langu kwa siku kadhaa. Nilinyoa ndevu na kuoga kwenye vyoo vya vituo vya mafuta.

Siku moja, nilipokuwa naishi kwenye gari langu, nilifika Jumba la Ufalme saa kadhaa kabla ya kikundi chetu kukutana kwa ajili ya utumishi wa shambani. Nilikuwa nimemaliza zamu yangu hospitalini. Nilipokuwa nimekaa nyuma ya Jumba la Ufalme ambapo hakuna aliyeniona, nilianza kukumbuka mambo niliyoona katika vita vya Vietnam—harufu ya miili ya binadamu iliyoungua na damu iliyoganda. Akilini mwangu, niliwaona na kuwasikia vijana wakiniuliza, “Nitapona kweli? Nitapona kweli?” Nilijua wangekufa, lakini nilijitahidi kuwafariji kadiri nilivyoweza huku nikijitahidi kutoonyesha ukweli kupitia uso wangu. Nikiwa nimekaa hapo, nililemewa na hisia.

Nimefanya kila niwezalo, hasa ninapokabili majaribu na hali ngumu, kutopoteza upendo wangu wa kwanza kwa Yehova

Nilisali huku nikitiririkwa na machozi. (Zab. 56:8) Nilianza kufikiria kwa uzito kuhusu tumaini la ufufuo. Kisha wazo likanijia: Kupitia ufufuo, Yehova Mungu ataondoa madhara yaliyosababishwa na mauaji hayo makubwa na maumivu yangu ya kihisia na ya watu wengine. Mungu atawarudishia uhai vijana hao, na watapata nafasi ya kujifunza kumhusu. (Mdo. 24:15) Jambo hilo liligusa sana hisia zangu na kunifanya nimpende sana Yehova. Bado siku hiyo ni ya pekee sana kwangu. Tangu siku hiyo, nimefanya kila niwezalo, hasa ninapokabili majaribu na hali ngumu, kutopoteza upendo wangu wa kwanza kwa Yehova.

YEHOVA AMEKUWA MWEMA KWANGU

Wakati wa vita, watu hufanya mambo mabaya sana. Hata mimi pia nilifanya mambo hayo. Lakini kutafakari maandiko mawili ninayoyapenda sana kumenisaidia. Andiko la kwanza ni Ufunuo 12:10, 11, linalosema kuwa Ibilisi hushindwa, si tu kwa kutoa kwetu ushahidi bali pia kwa sababu ya damu ya Mwana-Kondoo. Andiko la pili ni Wagalatia 2:20. Kutokana na andiko hilo, ninajua kwamba Kristo Yesu alikufa “kwa ajili yangu.” Kwa msingi wa damu ya Yesu, Yehova amenisamehe mambo niliyofanya. Kujua jambo hilo kumenisaidia kuwa na dhamiri safi na kumenichochea kufanya yote ninayoweza ili niwasaidie wengine wajue ukweli kumhusu Mungu wetu mwenye rehema, Yehova!—Ebr. 9:14.

Ninapofikiria maisha yangu, ninamshukuru sana Yehova kwa kunitunza. Kwa mfano, Jim alipotambua kuwa naishi kwenye gari langu, alinipeleka kwa dada fulani aliyekuwa na nyumba ya kupangisha. Ninaamini kabisa kwamba Yehova alimtumia Jim na dada huyo mpendwa kuniandalia sehemu nzuri ya kuishi. Yehova ni mwenye fadhili sana! Anawatunza watumishi wake waaminifu.

KUJIFUNZA KUWA MWENYE BUSARA

Mnamo Mei 1971, nililazimika kwenda Michigan ili kushughulikia mambo fulani. Kabla ya kuondoka katika Kutaniko la Delray Beach katika jimbo la Florida, nilijaza machapisho kwenye buti la gari langu, na kisha nikasafiri kupitia barabara kuu inayoelekea upande wa kaskazini. Kabla ya kufika nusu ya safari machapisho yote yalikuwa yameisha. Nilihubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme katika sehemu mbalimbali. Nilihubiri kwenye magereza na hata niliwaachia trakti wanaume niliokutana nao katika maeneo yenye vyoo vya umma. Hadi leo, huwa najiuliza ikiwa kuna mbegu yoyote kati ya zile nilizopanda ilichipuka.—1 Kor. 3:6, 7.

Nilipoanza kujifunza kweli sikuwa na busara, hasa nilipoongea na watu wa karibu wa familia yangu. Kwa kuwa upendo wangu wa kwanza kwa Yehova uliwaka ndani yangu, niliwahubiria kwa ujasiri lakini bila busara. Ninawapenda sana kaka zangu, John na Ron, na hivyo niliwalazimisha waikubali kweli. Baadaye ilibidi niwaombe msamaha kwa kutojali hisia zao. Hata hivyo, sikuzote ninasali ili waikubali kweli. Tangu wakati huo, Yehova amenielimisha, hivyo nimekuwa na busara zaidi ninapohubiri na kufundisha.—Kol. 4:6.

WATU WENGINE NINAOWAPENDA MAISHANI MWANGU

Ninajua kwamba ninampenda Yehova, hata hivyo siwasahau watu wengine ninaowapenda pia. Mtu mwingine ninayempenda ni mke wangu, Susan. Nilihitaji mwenzi ambaye angenisaidia kutimiza kazi ya Ufalme. Susan ni mwanamke mwenye nguvu kiroho. Ninakumbuka siku niliyomtembelea tulipokuwa marafiki. Alikuwa ameketi kwenye varanda ya nyumbani kwao huko Cranston, Rhode Island. Alikuwa akisoma gazeti la Mnara wa Mlinzi na Biblia yake. Kilichonivutia sana ni kwamba alikuwa akisoma makala za ziada na maandiko yaliyotajwa. Nilijiambia hivi, ‘Huyu ni mwanamke wa kiroho!’ Tulifunga ndoa Desemba 1971, na ninashukuru sana kwamba tangu wakati huo amekuwa pamoja nami na kuniunga mkono. Ninampenda Susan kwa sababu anampenda sana Yehova.

Nikiongoza mkutano wa utumishi wa shambani nilipokuwa mwangalizi wa mzunguko

Mimi na Susan tumebarikiwa kupata watoto wawili, Jesse na Paul. Yehova alikuwa pamoja nao walipokuwa wakikua. (1 Sam. 3:19) Kwa sababu wamefanya kweli iwe mali yao, wanatuletea sifa nzuri mimi na Susan. Wanaendelea kumtumikia Yehova kwa sababu wanakumbuka upendo wao wa kwanza kwake. Kila mmoja amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 20. Pia, ninajivunia sana binti-wakwe zangu, Stephanie na Racquel, ambao ninawaona kuwa binti zangu. Watoto wangu wote wameoa wanawake wa kiroho wanaompenda Yehova kwa moyo na nafsi yao yote.—Efe. 6:6.

Nikiwa na mke wangu, Susan, na watoto wetu, Paul na Jesse

Baada ya kubatizwa, nilitumikia kwa miaka 16 katika jimbo la Rhode Island, ambapo nilipata marafiki wa kweli. Nilifurahia sana kutumikia huko pamoja na wazee wenye uzoefu. Kwa kuongezea, ninawashukuru sana waangalizi wengi wanaosafiri ambao walinichochea sana. Ni heshima kubwa kufanya kazi pamoja na wanaume waliodumisha upendo wao wa kwanza kwa Yehova! Mwaka wa 1987, tulihamia North Carolina ili kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa, na huko tulipata marafiki wengine wazuri. *

Tulifurahia kuhubiri pamoja katika eneo lisilohubiriwa kwa ukawaida

Agosti 2002, mimi na Susan tulikubali mwaliko wa kujiunga na familia ya Betheli ya Patterson nchini Marekani. Nilifanya kazi katika Idara ya Utumishi, na Susan alifanya kazi ya dobi. Aliipenda sana kazi hiyo! Kisha, Agosti 2005, nilipata mwaliko wa kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Nilihisi nimenyenyekezwa sana kwa sababu ya mgawo huo. Mke wangu mpendwa alihisi amelemewa sana alipofikiria majukumu yanayohusika katika kazi hiyo na jinsi ambavyo tungesafiri mara nyingi. Susan hajawahi kupenda safari za ndege, lakini tunasafiri kwa ndege mara nyingi! Anasema kwamba anatiwa sana moyo anapozungumza na wake wa washiriki wengine wa Baraza Linaloongoza, hivyo ameazimia kuniunga mkono kadiri inavyowezekana. Kwa hakika amefanya hivyo, na hilo linafanya nimpende sana.

Ofisini kwangu kuna picha nyingi ninazozithamini sana! Zinanikumbusha maisha mazuri niliyofurahia. Nimepata baraka nyingi sana kwa sababu ya kufanya yote niwezayo ili kukumbuka upendo wangu wa kwanza kwa Yehova!

Kutumia wakati pamoja na familia yangu huniletea shangwe sana

^ fu. 31 Habari zaidi kuhusu utumishi wa wakati wote wa Ndugu Morris zinapatikana katika ukurasa wa 26 wa gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2006.