Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mzoeze Mtoto Wako Amtumikie Yehova

Mzoeze Mtoto Wako Amtumikie Yehova

“Tafadhali, yule mtu wa Mungu wa kweli . . . na arudi kwetu tena, atufundishe yale tunayopaswa kumtendea huyo mtoto atakayezaliwa.”—AMU. 13:8.

NYIMBO: 88, 120

1. Manoa alitendaje alipoambiwa kwamba atapata mtoto?

MANOA na mke wake hawakutarajia kupata mtoto maishani mwao. Mke alikuwa tasa, kwa hiyo walijua wazi kwamba jambo hilo haliwezekani. Hata hivyo, malaika wa Yehova alimtokea mke wa Manoa na kumwambia jambo la kushangaza; alisema kwamba yeye na mume wake, watapata mtoto! Bila shaka Manoa alifurahi, lakini pia alitambua kwamba angekuwa na jukumu zito. Wangewezaje kumlea mtoto wao ili amtumikie Mungu katika taifa lililojaa uovu? Manoa “akaanza kumsihi Yehova,” akisema: “Nakuomba radhi, Yehova. Tafadhali, yule mtu wa Mungu wa kweli [malaika] ambaye ulimtuma na arudi kwetu tena, atufundishe yale tunayopaswa kumtendea huyo mtoto atakayezaliwa.”—Amu. 13:1-8.

2. Kumzoeza mtoto kunahusisha nini? (Tazama pia sanduku lenye kichwa “ Wanafunzi Wako Muhimu Zaidi.”)

2 Ikiwa wewe ni mzazi, bila shaka unaelewa vizuri ombi la Manoa. Wewe pia una jukumu zito la kuwasaidia watoto wako wamjue na kumpenda Yehova. (Met. 1:8) Ili wafanikiwe, wazazi Wakristo wanajitahidi kupanga Ibada ya Familia kwa njia itakayowasaidia watoto wao wakue kiroho. Hata hivyo, ili kuwasaidia watoto wapende kweli za Biblia, unahitaji kufanya mengi zaidi ya kuongoza ibada ya familia kila juma. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:6-9.) Unawezaje kukabiliana na changamoto mbalimbali unapomfundisha kweli mtoto wako? Katika makala hii na ile inayofuata, tutazungumzia jinsi wazazi wanavyoweza kumwiga Yesu. Ingawa Yesu hakuwa na mtoto, wazazi wanaweza kuiga njia yake ya kufundisha kwa sababu aliwafundisha na kuwazoeza wanafunzi wake kwa upendo, unyenyekevu, na ufahamu. Acheni tuchunguze sifa hizo, moja baada ya nyingine.

MPENDE MTOTO WAKO

3. Yesu alionyeshaje kwamba anawapenda wanafunzi wake?

3 Yesu hakusita kuwaambia wanafunzi wake kwamba anawapenda. (Soma Yohana 15:9.) Pia, alionyesha kwamba anawapenda kwa kushirikiana nao kwa ukaribu na kwa ukawaida. (Marko 6:31, 32; Yoh. 2:2; 21:12, 13) Yesu hakuwa tu mwalimu; alikuwa pia rafiki yao. Hivyo, hawakuwa na shaka hata kidogo kwamba anawapenda. Unawezaje kuiga njia ya Yesu ya kufundisha?

4. Unaweza kuwahakikishiaje watoto wako kwamba unawapenda? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

4 Waambie watoto wako kwamba unawapenda, na uwaonyeshe mara kwa mara jinsi unavyowathamini. (Met. 4:3; Tito 2:4) Samuel, anayeishi Australia, anasema hivi: “Nilipokuwa mdogo, Baba alinisomea Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kila jioni. Alijibu maswali yangu, alinikumbatia, alinibusu na kunitakia usiku mwema. Baadaye, nilishangaa sana nilipogundua kwamba Baba alilelewa katika familia ambayo haikuwa na kawaida ya kukumbatiana na kubusiana! Hata hivyo, alijitahidi sana kuonyesha jinsi anavyonipenda. Kwa sababu hiyo, tulikuwa na uhusiano wa karibu sana na nilijihisi nikiwa salama.” Mfanye mtoto wako ahisi hivyo kwa kumwambia mara kwa mara, “Ninakupenda.” Onyesha hivyo kwa matendo. Zungumza nao, kula nao, na ucheze nao.

5, 6. (a) Yesu huwafanya nini wale anaowapenda? (b) Unawezaje kumtia nidhamu mtoto wako kwa njia inayofaa?

5 Yesu alisema hivi: “Wale wote ninaowapenda, mimi huwakaripia na kuwatia nidhamu.” * (Ufu. 3:19) Ingawa wanafunzi wa Yesu walibishana tena na tena kuhusu ni nani aliyekuwa mkubwa kati yao, Yesu hakuvunjika moyo. Naye hakuwapuuza waliposhindwa kufuata ushauri wake. Kwa upendo na kwa upole, Yesu aliwarekebisha kwa wakati unaofaa na mahali panapofaa.—Marko 9:33-37.

6 Onyesha kwamba unawapenda watoto wako kwa kuwatia nidhamu. Wakati mwingine inatosha tu kueleza kwa nini jambo fulani ni zuri au baya. Lakini ufanye nini ikiwa bado mtoto wako hatii? (Met. 22:15) Mwige Yesu. Ukiwa mahali panapofaa na kwa wakati unaofaa, mtie nidhamu mtoto wako kwa upendo na kwa upole; mpatie mwongozo, mazoezi, na umrekebishe kwa subira. Dada Elaine kutoka Afrika Kusini anasema, “Wazazi wangu walitoa nidhamu kwa uthabiti.” Anaongeza hivi: “Ikiwa wangenieleza matokeo ya kufanya jambo fulani lisilofaa, sikuzote wangeshikamana na uamuzi wao. Lakini hawakuwahi kunitia nidhamu kwa hasira au bila kueleza sababu. Kwa hiyo, nilihisi nikiwa salama. Nilijua mipaka yangu, na nilielewa kile walichotaka nifanye.”

UWE MNYENYEKEVU

7, 8. (a) Sala za Yesu zinaonyeshaje kwamba alikuwa mnyenyekevu? (b) Unawezaje kutumia sala kuwafundisha watoto wako wamtegemee Mungu?

7 Wazia jinsi wanafunzi wa Yesu walivyohisi baada ya kutambua kwamba Yesu alisema hivi katika moja ya sala alizotoa mwishoni mwa maisha yake akiwa mwanadamu: “Abba, Baba, mambo yote yanawezekana kwako; niondolee kikombe hiki. Lakini si lile ninalotaka, bali lile unalotaka.” * (Marko 14:36) Bila shaka, wafuasi wake walijifunza jambo zuri sana. Ikiwa Mwana mkamilifu wa Mungu alisali kwa unyenyekevu ili kuomba msaada, wao pia walipaswa kufanya vivyo hivyo.

8 Sala zako zinawafundisha nini watoto wako? Ni kweli kwamba kusudi kuu la kusali si kuwafundisha watoto wako. Hata hivyo, unaposali kwa unyenyekevu mbele yao, unawafundisha kumtegemea Yehova. Ana, anayeishi nchini Brazili, anasema hivi: “Tulipokuwa na matatizo, kama vile babu na nyanya walipougua, wazazi wangu walimwomba Yehova awape nguvu za kukabiliana na hali hiyo na hekima ya kufanya maamuzi mazuri. Hata walipokuwa na mkazo mkubwa, waliacha matatizo yao mikononi mwa Yehova. Hilo lilinifundisha kumtegemea Yehova.” Unaposali pamoja na watoto wako, usisali tu kwa niaba yao. Mwombe Yehova akusaidie wewe pia. Kwa mfano, unaweza kumwomba Yehova akupe ujasiri wa kumhubiria jirani yako, kuzungumza na mwajiri wako ili akupe ruhusa ya kuhudhuria kusanyiko, au jambo lingine. Uwe mnyenyekevu na umtegemee Mungu, na watoto wako watajifunza kufanya hivyo.

9. (a) Yesu aliwafundishaje wanafunzi wake kuwa wanyenyekevu? (b) Ukiwa tayari kuwatumikia wengine, watoto wako watajifunza nini?

9 Kwa maneno na matendo, Yesu aliwazoeza wanafunzi wake wawe wanyenyekevu na wawahudumie wengine. (Soma Luka 22:27.) Aliwafundisha mitume wake wajidhabihu wanapomtumikia Yehova na kuwasaidia waabudu wenzao. Unaweza kuwafundisha watoto wako jambo hilohilo ikiwa utakuwa mnyenyekevu na kuwa tayari kujidhabihu. Debbie, mama mwenye watoto wawili, anasema hivi: “Sikuwa na wivu mume wangu alipotumia muda wake kuwasaidia wengine akiwa mzee. Nilijua kwamba familia yetu ilipomhitaji, alikuwa tayari kutusaidia.” (1 Tim. 3:4, 5) Mume wake, Pranas, anaongeza hivi: “Baadaye, watoto wetu walipenda sana kuhusishwa katika makusanyiko na miradi ya kitheokrasi. Walifanya maendeleo, wakapata marafiki, na walihisi kwamba wao ni sehemu ya kutaniko.” Sasa familia nzima inamtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote. Inaelekea watoto wako watajifunza kuwatumikia wengine wanapoona unyenyekevu wako na jinsi unavyojidhabihu.

TUMIA UFAHAMU

10. Yesu alitumiaje ufahamu watu walipomfuata huko Galilaya?

10 Yesu alikuwa na ufahamu. Hakufikiria tu mambo ambayo watu wanafanya, bali pia alitambua kwa nini wanayafanya. Wakati fulani, baadhi ya wasikilizaji wake huko Galilaya walionekana wanapenda kumfuata. (Yoh. 6:22-24) Lakini Yesu anaweza kusoma mioyo, naye alitambua kwamba watu hao walipenda zaidi chakula cha kimwili badala ya mafundisho yake. (Yoh. 2:25) Alitambua tatizo, aliwarekebisha, na aliwaeleza jinsi wanavyoweza kufanya maendeleo.—Soma Yohana 6:25-27.

Je, mtoto wako anafurahia kuhubiri? (Tazama fungu la 11)

11. (a) Toa mfano unaoonyesha jinsi ufahamu unavyoweza kukusaidia kutambua ikiwa mtoto wako anafurahia huduma au la. (b) Unaweza kumsaidiaje mtoto wako afurahie kuhubiri?

11 Ingawa huwezi kusoma moyo, unaweza kutumia ufahamu ili kutambua mtoto wako anahisije kuhusu huduma ya shambani. Wanapokuwa katika huduma pamoja na watoto wao, wazazi wengi hutenga wakati wa kupumzika ili kupata chakula au vinywaji. Hata hivyo, unaweza kutambua maoni ya mtoto wako kwa kujiuliza hivi: ‘Je, mtoto wangu anafurahia huduma au anafurahia tu wakati wa mapumziko?’ Ukitambua kwamba mtoto wako hapendezwi sana na huduma, basi fanyeni mambo yatakayomsaidia aifurahie. Uwe mbunifu na umshirikishe ili ahisi kwamba anahusika akiwa mwandamani wako.

12. (a) Yesu alitumiaje ufahamu kuwaonya wafuasi wake kuhusu ukosefu wa maadili? (b) Kwa nini onyo la Yesu lilikuwa muhimu sana?

12 Yesu alitumia ufahamu pia kueleza hatua zinazoweza kumfanya mtu atende dhambi. Kwa mfano, wafuasi wake walijua kwamba uasherati ni dhambi. Hata hivyo, Yesu aliwaonya kuhusu hatua zinazoweza kumwongoza mtu kufanya uasherati aliposema hivi: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake. Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe ulitupilie mbali nawe.” (Mt. 5:27-29) Maneno hayo yalikuwa muhimu sana kwa Wakristo walioishi chini ya utawala wa Roma. Mwanahistoria mmoja alisema kwamba wakati huo “macho na masikio yaliona na kusikia mambo machafu” katika majumba ya michezo ya Waroma. Naye aliongeza hivi: “Maonyesho machafu zaidi ndiyo yaliyoshangiliwa zaidi.” Naam, Yesu aliwapenda wafuasi wake na alitumia ufahamu kuwaonya kuhusu mambo yanayoweza kuwachafua kiadili!

13, 14. Unaweza kuwasaidiaje watoto wako waepuke burudani zisizofaa?

13 Ufahamu utakusaidia kuwalinda kiroho watoto wako. Leo, watoto wanaweza kupata ponografia na habari nyingine zisizofaa tangu wakiwa wadogo. Bila shaka, wazazi Wakristo wanawaonya watoto wao kuhusu burudani chafu. Hata hivyo, ufahamu utakusaidia pia kuelewa kwamba mtoto wako anaweza kudadisi habari za ponografia. Jiulize hivi: ‘Ni nini kinachoweza kumshawishi mtoto wangu atazame ponografia? Je, anajua madhara ya ponografia? Je, yuko huru kuzungumza nami na kuniomba msaada anaposhawishiwa kutazama ponografia?’ Unaweza kuwaambia hivi watoto wako, hata ikiwa bado ni wadogo: “Ukishawishiwa kutazama habari fulani isiyofaa kwenye intaneti, tafadhali uwe huru kuzungumza nami. Usione aibu. Ninataka kukusaidia.”

14 Isitoshe, ufahamu utakusaidia kuchagua burudani kwa hekima. Pranas, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Muziki, filamu, au vitabu ambavyo wazazi wanasoma vinaathiri familia nzima.” Anaongeza hivi: “Unaweza kusema mambo mengi sana, lakini watoto wako wataangalia kile unachofanya na kukuiga.” Watoto wako wakiona kwamba unachagua kwa makini burudani zinazofaa, inaelekea watafanya vivyo hivyo.—Rom. 2:21-24.

MUNGU WA KWELI ATAWASIKILIZA

15, 16. (a) Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakusaidia kuwazoeza watoto wako? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

15 Ni nini kilichotokea Manoa alipomwomba Mungu msaada wa kumlea mtoto? “Mungu wa kweli akaisikiliza sauti ya Manoa.” (Amu. 13:9) Wazazi, Yehova atawasikiliza ninyi pia. Atajibu sala zenu na kuwasaidia mnapowazoeza watoto wenu. Nanyi mnaweza kufanikiwa, mkifanya hivyo kwa upendo, unyenyekevu, na ufahamu.

16 Zaidi ya kuwasaidia wazazi wanapowazoeza watoto wadogo, Yehova anaweza kuwasaidia pia wanapowazoeza vijana waliobalehe. Makala inayofuata itaeleza jinsi wazazi wanavyoweza kuiga upendo, unyenyekevu, na ufahamu wa Yesu wanapowazoeza vijana wao kumtumikia Yehova.

^ fu. 5 Kulingana na Biblia, nidhamu hutolewa kwa upendo nayo inahusisha kutoa mwongozo, mazoezi, rekebisho, na wakati mwingine adhabu—lakini kamwe haihusishi hasira.

^ fu. 7 Kitabu kimoja kinasema hivi: “Katika mazungumzo ya kawaida katika siku za Yesu, neno ‘abbāʼ lilitumiwa hasa na watoto wenye heshima waliokuwa na uhusiano wa karibu na baba zao.”—The International Standard Bible Encyclopedia.