Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anakuahidi Utajiri?

Je, Mungu Anakuahidi Utajiri?

Je, Mungu Anakuahidi Utajiri?

‘Mungu anataka uwe tajiri, uwe na magari, biashara nzuri. Mwamini tu, mpe pesa zako, na umpe chochote unachoweza.’

HUO ndio ujumbe unaohubiriwa na vikundi fulani huko Brazili, kulingana na gazeti fulani linalochapishwa huko. Watu wengi wanachukua ujumbe huo kwa uzito. Gazeti Time linaripoti hivi kuhusu maoni yaliyokusanywa kutoka kwa watu wanaodai kuwa Wakristo nchini Marekani: “Asilimia 61 waliamini kwamba Mungu anataka watu wawe matajiri. Na asilimia 31 . . . walikubali kwamba ukimpa Mungu pesa zako, atakubariki kwa kukupa pesa nyingi zaidi.”

Imani kama hizo, ambazo mara nyingi zinaitwa theolojia ya ufanisi, zinaenea upesi sana hasa katika nchi za Amerika ya Latini, kama vile Brazili, na watu humiminika katika makanisa yanayoahidi kwamba mtu atapata mali kutoka kwa Mungu. Lakini je, Mungu anawaahidi utajiri wale wanaomtumikia? Je, watumishi wote wa Mungu wa nyakati za kale walikuwa matajiri?

Ni kweli kwamba katika Maandiko ya Kiebrania, mara nyingi wale waliobarikiwa na Mungu walikuwa matajiri. Kwa mfano, tunasoma hivi katika Kumbukumbu la Torati 8:18: “Nawe umkumbuke Yehova Mungu wako, kwa sababu yeye ndiye anayekupa nguvu za kufanyiza mali.” Hilo liliwahakikishia Waisraeli kwamba ikiwa wangemtii Mungu, wangekuwa taifa lenye ufanisi.

Vipi mtu mmoja-mmoja? Mwanamume mwaminifu Ayubu alikuwa na mali nyingi sana, na baada ya Shetani kumletea umaskini, Yehova alimrudishia Ayubu mali yake “mara mbili.” (Ayubu 1:3; 42:10) Pia Abrahamu alikuwa tajiri. Mwanzo 13:2 inasema kwamba alikuwa na “utajiri mwingi wa mifugo na fedha na dhahabu.” Majeshi yaliyoungana ya wafalme wanne wa Mashariki yalipomteka Loti, mpwa wa Abrahamu, Abrahamu “akakusanya watu wake waliozoezwa, watumwa mia tatu kumi na wanane waliozaliwa nyumbani mwake.” (Mwanzo 14:14) Akiwa na ‘watu wake 318 waliozoezwa’ ambao wangeweza kupigana, lazima iwe nyumba ya Abrahamu ilikuwa kubwa sana. Lazima Abrahamu awe alikuwa tajiri sana, mwenye makundi na mifugo, kwa kuwa angeweza kuandaa mahitaji ya familia kubwa hivyo.

Naam, watumishi wengi wa kale waaminifu wa Mungu kama vile, Abrahamu, Isaka, Yakobo, Daudi, Sulemani, na wengine, walikuwa matajiri. Hata hivyo, je, hilo linamaanisha kwamba Mungu atamfanya kila mtu anayemtumikia awe tajiri? Kwa upande ule mwingine, je, kwa kuwa mtu ni maskini hilo linamaanisha kwamba hana baraka za Mungu? Makala inayofuata itazungumzia maswali hayo.