Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Pesa Ndiyo Chanzo cha Furaha ya Kweli?

Je, Pesa Ndiyo Chanzo cha Furaha ya Kweli?

Je, Pesa Ndiyo Chanzo cha Furaha ya Kweli?

SONIA alizaliwa nchini Hispania. Alipokuwa mtoto alihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova pamoja na mama yake. Lakini alipokuwa mtu mzima alihamia London, nchini Uingereza, na akaanza kufanya kazi kama dalali wa wawekezaji.

Sonia alipenda kazi yake. Alikuwa akipata pesa nyingi na alishughulikia pesa nyingi za wateja wake. Kawaida Sonia alifanya kazi kwa saa 18 kila siku na nyakati nyingine alilala kwa saa mbili au tatu tu. Kazi ndiyo ilikuwa jambo muhimu maishani mwake. Kisha kwa ghafula mambo yakamwendea mrama. Sonia alipatwa na kiharusi kwa sababu ya maisha yake yenye mkazo sana. Alikuwa na umri wa miaka 30 tu.

Sonia alipooza upande mmoja wa mwili wake na madaktari hawakuwa na hakika ikiwa angewahi kuzungumza tena. Mama yake alisafiri mara moja kwenda Uingereza ili amtunze. Sonia alipoanza kutembea tena, mama yake alimwambia, “Ninaenda kwenye mikutano ya kutaniko, nawe utahitaji kuandamana nami kwa kuwa siwezi kukuacha peke yako.” Sonia alikubali kuandamana naye. Matokeo yakawaje?

“Kila kitu nilichosikia kilikuwa cha kweli. Kilikuwa kizuri kama nini,” Sonia anasema. “Nilikubali kujifunza Biblia na mmoja kati ya wengi walionisalimu mara ya kwanza nilipoenda kwenye Jumba la Ufalme. Rafiki zangu wa awali walikuwa wameacha kunitembelea lakini rafiki zangu wapya walikuwa wachangamfu na wenye kujali.”

Hatua kwa hatua, Sonia aliweza tena kuzungumza, na vilevile akafanya maendeleo ya kiroho haraka. Alibatizwa kabla ya mwaka mmoja kwisha. Wengi wa rafiki zake wapya walikuwa katika utumishi wa Kikristo wa wakati wote, na aliona jinsi walivyokuwa na furaha. ‘Ningependa kuwa kama wao,’ Sonia akajiambia. ‘Ningependa kumpa Yehova Mungu kilicho bora!’ Sasa Sonia anatumikia katika utumishi wa wakati wote.

Sonia alijifunza nini kutokana na maisha yake? “Ingawa nilikuwa nikipata pesa nyingi, mkazo na woga wa kupoteza kazi ulinifanya niwe na wasiwasi na nikose furaha. Nimetambua kwamba jambo muhimu maishani mwangu ni kuwa na uhusiano mzuri na Baba yangu wa mbinguni, Yehova. Sasa nina furaha ya kweli.”

“Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote,” akaandika mtume Paulo. “Kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:10) Sonia anakubaliana kabisa na ukweli wa maneno hayo.