Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kugunduliwa Kwa Hazina ya Biblia

Kugunduliwa Kwa Hazina ya Biblia

Kugunduliwa Kwa Hazina ya Biblia

KARNE nyingi zilizopita, vifaa vya kuandikia havikupatikana kwa urahisi kama ilivyo leo. Maandishi ambayo hayakuhitajiwa yaliyokuwa kwenye ngozi au vifaa vingine yalifutwa ili vifaa hivyo vitumiwe tena. Hata maandishi ya Biblia yalikwanguliwa kutoka kwenye ngozi nyembamba ili zitumiwe kuandika habari nyingine.

Moja kati ya maandishi hayo muhimu ya Biblia ni Kodeksi ya Efraemi Syri rescriptus, neno rescriptus likimaanisha “maneno yaliyoandikwa juu ya maneno mengine.” Kodeksi hiyo ni muhimu sana kwa kuwa ni moja kati ya nakala za zamani sana za sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ambayo bado yanapatikana. Kwa sababu hiyo, maandishi hayo ni muhimu ili kuonyesha usahihi wa sehemu hiyo ya Neno la Mungu.

Maandiko yaliyokuwapo kwenye kodeksi hiyo ya karne ya tano yaliondolewa katika karne ya 12 W.K. na tafsiri ya Kigiriki ya hotuba 38 za msomi Msiria Ephraem zikaandikwa mahali pake. Wataalamu waligundua Maandiko hayo ya Biblia yaliyofutwa mwishoni mwa karne ya 17. Miaka kadhaa iliyofuata, maendeleo yalifanywa ili kutambua maandishi ya awali kutoka kwenye hati hiyo. Hata hivyo, ilikuwa vigumu sana kusoma maandishi yote kwa sababu ya wino uliofutwa, ngozi iliyokuwa imeraruka, na herufi fulani zililingana kabisa na zile zilizofutwa. Kemikali fulani zilitumiwa ili kujaribu kuibua na kusoma maandishi hayo ya Biblia, lakini mbinu hiyo haikufanikiwa sana. Wasomi wengi walifikia mkataa kwamba maandishi hayo yaliyofutwa hayangeweza kusomwa.

Mapema katika miaka ya 1840, Konstantin von Tischendorf, Mjerumani aliyekuwa mtaalamu wa lugha alijitahidi kuchunguza kodeksi hiyo. Tischendorf alitumia miaka miwili kuchunguza hati hiyo. Kwa kuwa wengine walishindwa, ni nini kilichomwezesha kusoma maandishi hayo?

Tischendorf alikuwa na ujuzi wa kuelewa mwandiko wa Kigiriki wa herufi kubwa zilizounganishwa na zilizotenganishwa. * Kwa kuwa alikuwa na uwezo mzuri wa kuona, aligundua kwamba kwa kuinua tu ngozi hiyo kuelekea mwangaza angeweza kutambua maandishi hayo ya awali. Leo ili wasomi wafanye kazi kama hiyo, wao hutumia vifaa vya macho vilivyo na infrared, miale ya urujuanimno, na kadhalika.

Katika mwaka wa 1843 na 1845, Tischendorf alichapisha fasiri yake ya Kodeksi ya Efraemi. Hilo lilifanya ajulikane kuwa mtaalamu mkuu wa kuchunguza mwandiko wa kale wa Kigiriki.

Kodeksi ya Efraemi ina urefu wa sentimita 30 hivi na upana wa sentimita 25 hivi, na ni mojawapo ya hati za zamani sana zilizokuwa na maandishi kwenye safu moja tu ya kila ukurasa. Kati ya kurasa 209 zilizopatikana za hati hiyo, 145 ni sehemu za vitabu vyote vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo isipokuwa 2 Wathesalonike na 2 Yohana. Kurasa hizo nyingine ni tafsiri ya Kigiriki ya sehemu fulani za Maandiko ya Kiebrania.

Leo, Kodeksi hiyo imewekwa katika Maktaba ya Taifa huko Paris, Ufaransa. Haijulikani hati hiyo ilitoka wapi, ingawa Tischendorf alifikiria kwamba ilitoka Misri. Wasomi wameorodhesha Kodeksi ya Efraemi kuwa kati ya hati nne muhimu za Biblia ya Kigiriki zilizoandikwa kwa mkono, hati nyingine ni Hati ya Sinai, Hati ya Aleksandria, Hati ya Vatikani 1209, ambazo ni za karne ya nne na tano W.K.

Ujumbe wa Maandiko Matakatifu umehifadhiwa vizuri katika njia nyingi kwa ajili yetu. Ingawa katika kisa hiki, mtu fulani asiyethamini maandishi ya Biblia alijaribu kuyafuta, ujumbe wake umedumu. Hilo linatuthibitishia ukweli wa maneno haya ya mtume Petro: “Neno la Yehova linadumu milele.”—1 Petro 1:25.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 6 Tischendorf anajulikana kuwa ndiye aliyegundua moja kati ya hati za zamani sana za tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania katika makao ya watawa ya Mt. Catherine yaliyo chini ya Mlima Sinai. Hati hiyo inaitwa Kodeksi ya Sinai.

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 16]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Kodeksi ya Efraemi Syri rescriptus, maandishi muhimu yaliyogunduliwa na Tischendorf (1815-1874)

MAANDIKO YA AWALI

HOTUBA YA KIGIRIKI ILIYOANDIKWA JUU YA MAANDIKO YA AWALI

[Hisani]

© Bibliothèque nationale de France

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kodeksi ya Sinai, iliyogunduliwa katika makao ya watawa ya Mt. Catherine

[Picha katika ukurasa wa 17]

Tischendorf