Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa na Furaha na Tumaini Licha ya Umaskini

Kuwa na Furaha na Tumaini Licha ya Umaskini

Barua Kutoka Bolivia

Kuwa na Furaha na Tumaini Licha ya Umaskini

NINATUMIKIA nikiwa mmishonari katika nchi inayositawi nami huona umaskini mwingi na watu wasio na tumaini. Ninatamani kuwaona watu wote wakiacha kuteseka mara moja. Lakini ninajua kwamba ni Ufalme wa Mungu tu utakaotatua matatizo hayo. Hata hivyo, mara nyingi nimeona watu wanaotii Neno la Mungu wanapata furaha licha ya hali ngumu. Sabina ni mmoja wao.

Miaka mingi iliyopita, Sabina, akiwa amewabeba binti zake wawili wachanga, alimwona mume wake akipanda basi kuukuu ili akatafute kazi yenye mshahara mzuri katika nchi nyingine. Alimngojea arudi, miaka nenda miaka rudi, lakini hakurudi. Tangu alipoondoka, Sabina alilazimika kufanya kazi kwa bidii ili ajiruzuku na binti zake, Milena na Ghelian.

Nilikutana na Sabina alasiri moja alipokuwa akiwahudumia wateja wake wasio na subira katika duka la dada yake. Ningeweza kuona katika macho ya Sabina yenye uchovu kwamba alikuwa amefanya kazi ngumu siku nzima. Nilimwuliza ikiwa yeye na binti zake wangependa niwafunze Biblia. “Ningependa,” akasema, “lakini nina shughuli nyingi. Hata hivyo, ningependa ujifunze pamoja na wasichana wangu.” Nilikubali. Tulipoendelea kujifunza pamoja na binti zake, nilikuja kumfahamu Sabina, na nikaelewa hali yake ngumu.

Sabina huamka saa 10:00 usiku. Huku binti zake wakiwa wamelala katika nyumba yao ya chumba kimoja, Sabina huwasha moto na kuwekelea sufuria kubwa iliyozeeka juu yake. Anapika nyama ambazo atajaza ndani ya vitu kama sambusa atakazouza ili kuiruzuku familia yake. Usiku, Sabina alikuwa amekanda unga kwa ajili ya sambusa hizo tamu.

Kwa uangalifu, Sabina anapakia vifaa vyote atakavyotumia kwenye mkokoteni alioazima. Vifaa hivyo vinatia ndani, mwavuli, jiko linalotumia gesi, mtungi wa gesi, meza, viti vidogo, sufuria, na mafuta, pamoja na nyama na unga aliokanda na lita kadhaa za maji ya matunda aliyotengenezea nyumbani.

Saa 12:00 asubuhi, Sabina na binti zake wawili wako tayari kuondoka. Wanafunga mlango kwa kufuli. Hawazungumzi wala kucheka. Wanakazia fikira kazi iliyo mbele yao. Nimewatazama watu wengi wakiondoka nyumbani kwa njia hiyohiyo kutoka kwenye dirisha la makao yetu ya wamishonari. Naam, Sabina ni mmoja kati ya wanawake wengi ambao hutoka nyumbani kabla ya jua kuchomoza ili wakauze chakula na vinywaji kwenye mitaa ya Bolivia.

Saa 12:30, jua linapochomoza juu ya mlima, Sabina na binti zake wanafika mahali wanapofanyia biashara. Bila kusema chochote, wanapakua vitu kutoka kwenye mkokoteni na kutayarisha jiko lao. Sambusa ya kwanza inatiwa ndani ya mafuta yanayochemka. Harufu nzuri inatanda hewani na kuwavutia wateja wenye njaa.

“Ungependa ngapi?” Sabina anamwuliza mteja wa kwanza. Bila hata kumtazama, mwanamume mwenye lepe la usingizi anamwinulia vidole viwili, na anampa sambusa mbili moto. Anachukua pesa kidogo anazompa. Sabina atafanya hivyo mara nyingi sana siku nzima. Wanapouza sambusa ya mwisho, wanafunganya vitu vyao na kuelekea nyumbani. Ingawa miguu ya Sabina inamuuma kwa sababu ya kazi ya asubuhi, anaenda kufanya kazi yake ya pili kwenye duka la dada yake.

Nilipofika kwenye duka hilo ili nijifunze Biblia na binti zake kwa mara ya kwanza, benchi mbili zilikuwa zimewekwa kwenye kona fulani. Tangu mwanzo, Milena na Ghelian, ambao wakati huo walikuwa na umri wa miaka 9 na 7, walitazamia kwa hamu sana kila funzo na walijitayarisha vizuri. Hatua kwa hatua, wasichana hao wenye haya walianza kujihisi huru na wakaniruhusu niwe rafiki yao. Jambo hilo liliugusa sana moyo wa Sabina. Ingawa alikuwa na kazi ya kuchosha sana, aliamua kwamba ataanza kujifunza Biblia pamoja nami.

Kadiri Sabina alivyoendelea kujifunza Biblia, ndivyo upendo wake kwa Yehova Mungu ulivyoongezeka. Alianza kuwa mwenye furaha, jambo ambalo hakuwa amewahi kuhisi! Ingawa hapo awali alikuwa anaonekana mchovu na mwenye huzuni sasa alionekana tofauti kabisa. Alianza kuwa mchangamfu na macho yake yaling’aa. “Sasa Sabina anatabasamu kila wakati,” akasema dada yake. “Hakuwa hivyo zamani.” Wengine pia waliona kwamba Sabina na binti zake wamebadilika. Uhitaji wa kiroho aliokuwa nao kwa muda mrefu ulikuwa umetoshelezwa.

Sabina alifurahia kujifunza, lakini ratiba yake yenye shughuli nyingi ilimzuia kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Mwishowe, alikubali mwaliko wa kutembelea Jumba la Ufalme. Baada ya hapo, hakuacha kuhudhuria mikutano. Sabina alipata marafiki wa kweli kutanikoni. Pia alijionea kwamba Yehova huwaandalia kikweli wale wanaompenda na kujidhabihu ili kumtumikia.—Luka 12:22-24; 1 Timotheo 6:8.

Sabina alipenda mambo aliyokuwa akijifunza, na akatamani kuwaeleza wengine mambo hayo. Lakini alisema, “Mimi hutetemeka kila ninapofikiri kuhusu kuwahubiria watu.” Alijiambia hivi, ‘Mwanamke mwenye haya na asiye na elimu kama mimi anawezaje kumfundisha mtu mwingine?’ Hata hivyo, fadhili alizoonyeshwa na maendeleo makubwa aliyokuwa amefanya maishani yalimchochea kupiga hatua hiyo. Pia alitambua kwamba binti zake walimtazamia awawekee mfano mzuri. Kwa hiyo, alianza kuwaambia wengine kuhusu habari njema. Binti zake walijiunga naye kwa uchangamfu.

Leo, Sabina si mwanamke yule aliyekuwa hana furaha akifanya kazi yenye kuchosha siku baada ya siku. Hali yake ya kiuchumi haijabadilika sana. Kitu ambacho kimebadilika ni mtazamo wake kuhusu maisha. Sasa, akiwa Mkristo aliyebatizwa, yeye huwaambia wengine habari njema za Ufalme wa Mungu, ambao ndio utaondoa kabisa umaskini na hali zinazowafanya watu wakate tamaa.—Mathayo 6:10.

Ni saa 11:00 alfajiri, na Sabina yuko tayari kuondoka kwenye nyumba yake ya chumba kimoja. Lakini asubuhi ya leo haendi kuuza sambusa. Anakutana na Wakristo wenzake ili wakahubiri barabarani. Amepata furaha sana kwa kutenga wakati kila juma kuwasaidia wengine. Anafunga mlango wake akiwa na tabasamu usoni na kuelekea barabarani. Badala ya kusukuma mkokoteni, amebeba mfuko mkubwa. Ndani ya mfuko wake ana Biblia na vichapo vya Biblia ambavyo atatumia kuwaambia wengine kuhusu ujumbe wenye tumaini. Huku akiwa na tabasamu, Sabina anawaambia, “Sikudhani nitaweza kuzungumza na watu kuhusu Biblia.” Anaongezea hivi, “Ninafurahia sana kufanya kazi hii.”