Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Katika Njia Gani Yesu na Baba Yake Ni Kitu Kimoja?

Ni Katika Njia Gani Yesu na Baba Yake Ni Kitu Kimoja?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Ni Katika Njia Gani Yesu na Baba Yake Ni Kitu Kimoja?

“Mimi na Baba ni kitu kimoja,” akasema Yesu. (Yohana 10:30) Watu fulani hunukuu andiko hilo kuthibitisha kwamba Yesu na Baba yake ni sehemu ya Utatu. Je, hivyo ndivyo Yesu alivyomaanisha aliposema maneno hayo?

Acheni tuchunguze muktadha. Katika mstari wa 25, Yesu alisema kwamba anatenda kazi katika jina la Baba yake. Kuanzia mstari wa 27 hadi 29, alisema kuhusu kondoo wa mfano ambao Baba yake alimpa. Maneno hayo ya Yesu hayangekuwa na maana yoyote kwa wasikilizaji wake ikiwa yeye na Baba wangekuwa mtu yuleyule mmoja. Badala yake, Yesu alikuwa akisema hivi, ‘Mimi na Baba yangu tuna uhusiano wa karibu sana hivi kwamba mtu hawezi kuninyang’anya kondoo wangu kama tu vile mtu hawezi kumnyang’anya Baba.’ Ni kama tu mtoto akimwambia adui ya baba yake, ‘Ukimshambulia baba yangu, utakuwa ukinishambulia mimi.’ Hakuna yeyote anayeweza kukata kauli kwamba mtoto huyo na baba ni mtu mmoja. Lakini kila mtu angetambua kwamba wana uhusiano wa karibu sana.

Pia, Yesu na Baba yake, Yehova Mungu, ni “kitu kimoja” katika maana ya kwamba wanakubaliana kabisa inapohusu nia na viwango. Tofauti na Shetani Ibilisi na wale wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, Yesu hakutaka kamwe kujitegemea mwenyewe bila msaada wa Mungu. Yesu alieleza hivi: “Mwana hawezi kufanya hata jambo moja kwa uamuzi wake mwenyewe, ila tu lile analomwona Baba akifanya. Kwa maana mambo yoyote yale ambayo Yule hufanya, mambo hayo Mwana pia hufanya vivyo hivyo.”—Yohana 5:19; 14:10; 17:8.

Hata hivyo, uhusiano huo wa karibu sana haumfanyi Mungu na Mwana wake Yesu wawe mtu yuleyule. Wao ni watu wawili tofauti. Kila mmoja ana utu wake wa kipekee. Yesu ana hisia na mawazo yake mwenyewe, na pia kuna mambo ambayo amejionea mwenyewe, na ana uhuru wa kufanya mapenzi yake mwenyewe. Hata hivyo, aliamua kupatanisha mapenzi yake na yale ya Baba yake. Kulingana na Luka 22:42, Yesu alisema: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” Maneno hayo hayangekuwa na maana yoyote ikiwa Yesu hangekuwa na uwezo wa kufanya maamuzi tofauti na ya Baba yake. Ikiwa Yesu na Baba yake ni mtu yuleyule, kwa nini Yesu alisali kwa Mungu na kwa unyenyekevu akakubali kwamba hajui mambo ambayo Baba yake peke yake anayajua?—Mathayo 24:36.

Washiriki wa dini nyingi huabudu miungu ambayo huonyeshwa ikibishana na kupigana na watu wa familia yao yenyewe. Kwa mfano, katika hekaya za Kigiriki, Cronus alipindua mamlaka ya baba yake anayeitwa Uranus na kuwala watoto wake mwenyewe. Hilo ni tofauti kama nini na umoja tunaoona kati ya Yehova Mungu na Mwana wake Yesu, unaotegemea upendo wa kweli! Na umoja huo unatufanya tuwapende kama nini! Kwa kweli, tuna pendeleo lisilo na kifani la kuwa na uhusiano pamoja na Watu hao wawili wakuu zaidi katika ulimwengu wote. Yesu alisali hivi kuwahusu wafuasi wake: “Ninawaombea . . . wote wapate kuwa kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe, Baba, umo katika muungano pamoja na mimi na mimi nimo katika muungano pamoja na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano pamoja na sisi.”—Yohana 17:20, 21.

Hivyo, Yesu aliposema, “Mimi na Baba ni kitu kimoja,” hakuwa akizungumza kuhusu Utatu wa kifumbo, bali alikuwa akizungumza kuhusu umoja wenye kupendeza, yaani, uhusiano wa karibu zaidi unaoweza kuwapo kati ya watu wawili.