Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utajiri Unaotoka kwa Mungu

Utajiri Unaotoka kwa Mungu

Utajiri Unaotoka kwa Mungu

IKIWA wewe ni mwaminifu kwa Mungu, je, atakubariki kwa utajiri? Huenda, lakini hatakupa utajiri unaotarajia. Kwa mfano, mfikirie Maria, mama ya Yesu. Malaika Gabrieli alimtokea na kumwambia alikuwa ‘amependelewa sana’ na Mungu na kwamba angemzaa Mwana wa Mungu. (Luka 1:28, 30-32) Hata hivyo, Maria hakuwa tajiri. Alipoenda kutoa dhabihu baada ya kumzaa Yesu, Maria alitoa “njiwa-tetere wawili au hua wachanga wawili,” toleo ambalo kwa kawaida maskini walimtolea Yehova.—Luka 2:24; Mambo ya Walawi 12:8.

Je, kwa kuwa Maria alikuwa maskini hilo linamaanisha hakubarikiwa na Mungu? La, tofauti na hilo alipoenda kumtembelea Elisabeti, mtu wake wa ukoo, “Elisabeti akajazwa roho takatifu, naye akapaaza sauti kubwa na kusema: ‘Wewe [Maria] ni mbarikiwa kati ya wanawake, na uzao wa tumbo lako la uzazi umebarikiwa!’” (Luka 1:41, 42) Maria alipendelewa kuwa mama wa kidunia wa Mwana mpendwa wa Mungu.

Yesu hakuwa tajiri. Zaidi tu ya kuzaliwa na kulelewa katika eneo na familia maskini, alikuwa maskini muda wote alioishi duniani. Wakati fulani alimwambia hivi mwanamume mmoja aliyetaka kuwa mwanafunzi wake: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Luka 9:57, 58) Isitoshe, kuja kwa Yesu Kristo duniani kuliwawezesha wanafunzi wake kupata utajiri mwingi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Alikuja kuwa maskini kwa ajili yenu, ili muwe matajiri kupitia umaskini wake.” (2 Wakorintho 8:9) Yesu aliwapa wanafunzi wake utajiri wa aina gani? Na vipi leo?

Utajiri wa Aina Gani?

Mara nyingi utajiri unaweza kumzuia mtu kuwa na imani, kwa kuwa tajiri anaweza kutegemea pesa zake badala ya kumtegemea Mungu. Yesu alisema: “Jinsi itakavyokuwa vigumu kwa wale wenye pesa kuingia katika ufalme wa Mungu!” (Marko 10:23) Basi, ni wazi kwamba utajiri ambao Yesu aliwapa wafuasi wake si wa kimwili.

Kwa kweli, watu wengi katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza walikuwa maskini. Mtu mmoja aliyezaliwa akiwa mlemavu alipomwomba Petro pesa, Petro alimwambia: “Fedha na dhahabu sina, lakini kile nilicho nacho ndicho ninachokupa: Katika jina la Yesu Kristo Mnazareti, tembea!”—Matendo 3:6.

Maneno ya mwanafunzi Yakobo pia yanaonyesha kwamba watu wengi katika kutaniko la Kikristo walikuwa maskini. Aliandika hivi: “Sikilizeni, ndugu zangu wapendwa. Mungu alichagua walio maskini kwa habari ya ulimwengu ili wawe matajiri katika imani na warithi wa ufalme, aliowaahidi wale wanaompenda, sivyo?” (Yakobo 2:5) Isitoshe, mtume Paulo alisema kwamba si wengi “wenye hekima katika njia ya kimwili” au “wenye nguvu” au “wa uzawa wa cheo” walioitwa wawe sehemu ya kutaniko la Kikristo.—1 Wakorintho 1:26.

Ikiwa utajiri ambao Yesu aliwapa wafuasi wake si wa kimwili, basi aliwapa utajiri wa aina gani? Katika barua ambayo Yesu alituma katika kutaniko la Smirna, alisema hivi: “Ninajua dhiki na umaskini wako—lakini wewe ni tajiri.” (Ufunuo 2:8, 9) Ingawa Wakristo huko Smirna walikuwa maskini, walikuwa na utajiri wenye thamani nyingi kuliko fedha au dhahabu. Walikuwa matajiri kwa sababu ya imani na utimilifu wao kwa Mungu. Imani ni kitu chenye thamani sana kwa kuwa “imani si mali ya watu wote.” (2 Wathesalonike 3:2) Wale ambao hawana imani ni maskini machoni pa Mungu.—Ufunuo 3:17, 18.

Utajiri Unaotokana na Imani

Hata hivyo, ni katika njia gani imani ni kitu chenye thamani? Wale walio na imani katika Mungu wananufaika kutokana na “utajiri wa fadhili zake na uvumilivu wenye subira na ustahimilivu.” (Waroma 2:4) Pia wanafurahia “msamaha wa makosa [yao]” kwa sababu wana imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. (Waefeso 1:7) Isitoshe, “neno la Kristo” linawapa hekima wote walio na imani. (Wakolosai 3:16) Wanaposali kwa Mungu wakiwa na imani, “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote” inalinda mioyo na akili zao, na kuwapa uradhi na furaha.—Wafilipi 4:7.

Mbali na faida hizo zote, wale wanaoweka imani katika Mungu kupitia kwa Mwana wake, Yesu Kristo, wana taraja zuri la kupata uzima wa milele. Maneno haya ya Yesu Kristo yanajulikana sana: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Taraja hilo lenye thamani linaimarishwa mtu anapopata ujuzi sahihi kumhusu Baba na Mwana, kwa kuwa Yesu alisema hivi pia: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Ingawa Mungu anatoa hasa baraka za kiroho, anawanufaisha watu kihisia na kimwili vilevile. Kwa mfano, mfikirie Dalídio anayeishi huko Brazili. Kabla ya kupata ujuzi sahihi wa kusudi la Mungu, alikuwa mlevi. Hilo liliathiri sana uhusiano katika familia yake. Zaidi ya hilo, alikuwa na matatizo ya kifedha. Kisha akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na akafanya mabadiliko makubwa.

Ujuzi ambao Dalídio alipata ulimsaidia kuacha mazoea yake mabaya. Alifanya mabadiliko makubwa kiroho hivi kwamba akasema, “Zamani nilikuwa nikienda baa kwa baa; sasa ninaenda nyumba kwa nyumba.” Alikuja kuwa mtumishi wa wakati wote wa Neno la Mungu. Badiliko hilo liliboresha afya yake na hali yake ya kiuchumi. Dalídio alisema, “Pesa nilizokuwa nikitumia kununua kileo, sasa ninazitumia kuwasaidia wenye uhitaji au kununua vitu ninavyohitaji.” Pia amekuwa na marafiki wengi wa kweli kwa sababu ya kushirikiana na watu wenye mtazamo kama wake wa kiroho. Sasa Dalídio ana amani ya akili na uradhi ambao hakuwahi kufikiria anaweza kupata kabla ya kumjua Mungu.

Mfikirie Renato ambaye pia maisha yake yameboreshwa kwa sababu ya kuwa na imani katika Yehova Mungu. Unapoona tabasamu lake changamfu, ni vigumu kuwazia ikiwa aliwahi kutendewa vibaya maishani mwake. Alipozaliwa tu, mama yake alimtupa. Alimweka katika mfuko na kumwacha chini ya benchi, akiwa amekwaruzwa na kuchubuka na akiwa bado na kiunga-mwana (kitovu) chake. Wanawake wawili walipitia hapo na kuona mfuko huo chini ya benchi ukisonga-songa. Mwanzoni walifikiri kwamba mtu alikuwa ameacha kitoto cha paka hapo. Walipogundua kwamba alikuwa mtoto aliyetoka tu kuzaliwa, walimchukua upesi na kumpeleka kwenye hospitali iliyokuwa karibu.

Mmoja katika ya wanawake hao alikuwa Shahidi wa Yehova, naye akamwambia Rita, Shahidi mwingine wa Yehova, kumhusu mtoto huyo. Rita alikuwa amezaa watoto kadhaa waliokufa, na alikuwa na binti mmoja tu. Alitaka sana kupata mtoto wa kiume, kwa hiyo akaamua kumlea Renato.

Renato alipokuwa bado mtoto mdogo Rita alimwambia kwamba yeye si mama yake halisi. Lakini alimlea kwa upendo mwingi na akajitahidi kumfundisha viwango vya kiroho. Alipokuwa mkubwa, alianza kupendezwa na Biblia. Alithamini sana jinsi maisha yake yalivyookolewa alipokuwa mtoto. Kila wakati anaposoma maneno haya ya mtunga-zaburi Daudi, machozi hujaa machoni mwake: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.”—Zaburi 27:10.

Renato alionyesha uthamini wake kwa yote ambayo Yehova amemfanyia kwa kubatizwa mnamo 2002 na kuwa mhudumu Mkristo wa wakati wote mwaka uliofuata. Bado hawajui wazazi wake halisi na huenda hatawahi kuwajua. Hata hivyo, Renato anahisi kwamba zawadi yenye thamani zaidi ambayo amewahi kupata ni kumjua na kumwamini Yehova Baba yake mwenye upendo na anayejali.

Labda unatamani kuwa na uhusiano wa karibu na wenye upendo pamoja na Mungu, jambo ambalo linaweza kuboresha sana maisha yako. Kila mtu, awe tajiri au maskini, anaweza kuwa na uhusiano kama huo pamoja na Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo. Ingawa huenda mtu asipate utajiri wa kimwili kwa kufanya hivyo, lakini atapata amani ya akili na uradhi ambao pesa zote ulimwenguni haziwezi kununua. Maneno yanayopatikana kwenye Methali 10:22 ni ya kweli kama nini: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”

Yehova Mungu anapendezwa sana na watu wanaokuja kwake: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:18) Na anaahidi kwamba wote wanaomwendea wakiwa na nia na mtazamo mzuri watathawabishwa kwelikweli: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.”—Methali 22:4.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kumwamini Mungu huleta amani, uradhi, na furaha

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Ingawa familia ya Yesu ya kidunia ilikuwa maskini, ilibarikiwa sana na Mungu