Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yesu Ndiye Yule Malaika Mkuu Mikaeli?

Je, Yesu Ndiye Yule Malaika Mkuu Mikaeli?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Yesu Ndiye Yule Malaika Mkuu Mikaeli?

▪ Kwa ufupi, jibu ni ndiyo. Katika tamaduni nyingi ni jambo la kawaida kutumia majina mbalimbali kumrejelea mtu yuleyule. Ndivyo ilivyo katika Biblia. Kwa mfano, mzee wa ukoo Yakobo pia anaitwa Israeli. (Mwanzo 35:10) Mtume Petro ana majina matano tofauti katika Biblia—Simioni, Simoni, Petro, Kefa, na Simoni Petro. (Mathayo 10:2; 16:16; Yohana 1:42; Matendo 15:7, 14) Je, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mikaeli ni jina lingine la Yesu? Ona uthibitisho wa Maandiko unaofuata.

Mikaeli, yule kiumbe wa roho mwenye nguvu, anatajwa mara tano katika Biblia, na tatu kati ya hizo, zinapatikana katika kitabu cha Danieli. Katika andiko la Danieli 10:13, 21, tunasoma kwamba malaika fulani aliyekuwa ametumwa, aliokolewa na Mikaeli ambaye anaitwa “mmoja wa hao wakuu wa mbele” na “yule mkuu wenu.” Pia, katika andiko la Danieli 12:1, tunasoma kwamba katika siku za mwisho, “Mikaeli atasimama wakati huo, yule mkuu anayesimama kwa ajili ya wana wa watu wako.”

Mikaeli pia anatajwa kwenye andiko la Ufunuo 12:7, linalosema kuwa “Mikaeli na malaika zake” wanapigana vita muhimu ambavyo matokeo yake ni kufukuzwa kwa Shetani Ibilisi na malaika waovu kutoka mbinguni.

Ona kwamba katika maandiko hayo, Mikaeli anaonyeshwa kuwa malaika shujaa wa vita anayewapigania na kuwalinda watu wa Mungu, na hata anapigana na Shetani, adui mkuu wa Yehova.

Katika Yuda mstari wa 9, Mikaeli anaitwa “yule malaika mkuu.” Jina “malaika mkuu” halitumiki katika wingi mahali popote katika Biblia. Jina hilo linatajwa tena tu katika andiko la 1 Wathesalonike 4:16, ambapo Paulo anasema hivi kumhusu Yesu aliyefufuliwa: “Bwana [Yesu] mwenyewe atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wenye amri, kwa sauti ya malaika mkuu na kwa tarumbeta ya Mungu.” Kwa hiyo, katika andiko hilo Yesu Kristo mwenyewe anatambulishwa kuwa malaika mkuu.

Kwa kuzingatia mambo hayo, tunaweza kufikia uamuzi gani? Yesu Kristo ndiye Mikaeli, yule malaika mkuu. Majina yote mawili—Mikaeli (linalomaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”) na Yesu (linalomaanisha “Yehova Ni Wokovu”)—yanakazia jukumu lake akiwa mtetezi mkuu wa enzi kuu ya Mungu. Andiko la Wafilipi 2:9 linasema: “Mungu alimpandisha [Yesu aliyetukuzwa] kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine.”

Ni muhimu kutambua kwamba maisha ya Yesu hayakuanza wakati alipozaliwa duniani. Kabla ya Yesu kuzaliwa, malaika alimtembelea Maria na kumwambia kuwa angechukua mimba kupitia roho takatifu na kwamba alipaswa kumwita mtoto huyo Yesu. (Luka 1:31) Wakati wa huduma yake, mara nyingi Yesu alizungumza kuhusu maisha yake kabla ya kuwa mwanadamu.—Yohana 3:13; 8:23, 58.

Kwa hiyo, Mikaeli, yule malaika mkuu ni Yesu kabla ya kuwa mwanadamu. Baada ya kufufuliwa na kurudi mbinguni, Yesu alirudia utumishi wake akiwa Mikaeli, yule malaika mkuu, “kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Wafilipi 2:11.