Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Yesu Alikawia?

Kwa Nini Yesu Alikawia?

Wafundishe Watoto Wako

Kwa Nini Yesu Alikawia?

YESU amepata habari kuwa rafiki yake Lazaro ni mgonjwa sana. Mjumbe kutoka kwa Maria na Martha, dada za Lazaro amemletea Yesu habari hizo. Mjumbe huyo alitoka Bethania, mji ambamo Lazaro na dada zake wanaishi. Dada hao wanaamini kuwa Yesu ana uwezo wa kumponya ndugu yao, ingawa wanaishi mbali sana ng’ambo ya Mto Yordani. Wanajua kuwa Yesu amewahi kuwaponya watu akiwa mbali nao.—Mathayo 8:5-13; Yohana 11:1-3.

Mjumbe anapofikisha habari hizo za kuhuzunisha, Yesu hachukui hatua yoyote. Biblia inasema: ‘Alikaa siku mbili mahali alipokuwa.’ (Yohana 11:6) Je, unajua ni kwa nini Yesu hachukui hatua mara moja ili kumsaidia Lazaro?— * Acha tuzungumzie jambo hilo.

Yesu anajua kwamba Lazaro amekufa kutokana na ugonjwa wake. Hivyo, anawaambia hivi mitume wake: “Twendeni Yudea tena.” Nao wanapinga wakimwambia: “Juzijuzi tu Wayudea walikuwa wakitafuta kukupiga kwa mawe, na je, unaenda huko tena?” Kisha Yesu anawaeleza: “Lazaro rafiki yetu anapumzika, lakini ninafunga safari kwenda huko ili kumwamsha kutoka usingizini.”

Mitume wanamjibu: “Bwana, ikiwa anapumzika, atapona.” Yesu anawaambia: “Lazaro amekufa.” Kisha anasema maneno ambayo yanawashangaza sana: “Ninashangilia kwa sababu yenu kwamba sikuwa huko . . . Lakini twendeni kwake.”

Tomasi anasema hivi kwa ujasiri: ‘Acheni twende pia, ili tukafe pamoja na Yesu.’ Tomasi anajua kuwa maadui watajaribu kumuua Yesu, na mitume wake pia. Hata hivyo, wote wanaandamana na Yesu. Baada ya siku mbili hivi wanafika Bethania, mji wa nyumbani kwa Lazaro. Mji huu uko kilomita tatu hivi kutoka Yerusalemu.—Yohana 11:7-18.

Je, unajua ni kwa nini Yesu anafurahi kuwa hakufika mapema?—Yesu alikuwa amewafufua watu wengine hapo awali, lakini walikuwa wamekufa saa chache tu kabla ya Yesu kuwafufua. (Luka 7:11-17, 22; 8:49-56) Lakini mwili wa Lazaro umekaa siku nne kaburini. Kila mtu anajua kuwa amekufa fofofo!

Martha, dada ya Lazaro anaposikia kuwa Yesu yuko karibu na Bethania, anakimbia kukutana naye. Anasema hivi: “Bwana, kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Yesu anamhakikishia, “Ndugu yako atafufuka.” Martha anakimbia nyumbani na kumwambia hivi dada yake kwa siri: “Mwalimu yupo naye anakuita.”

Maria anaondoka upesi na kwenda kwa Yesu. Umati unamfuata Maria wakidhani kuwa anaenda kwenye kaburi. Yesu anapomwona Maria na umati ukilia, yeye naye ‘anatokwa na machozi.’ Kisha wanafika kwenye kaburi ambalo limefunikwa kwa jiwe kubwa. Yesu anaamuru hivi: “Liondoeni jiwe.” Lakini Maria anakataa akisema: “Bwana, kufikia sasa lazima awe ananuka, kwa maana ni siku nne.”

Watu wanamtii Yesu na kuondoa jiwe hilo. Kisha, anasali na kumshukuru Mungu kwa ajili ya nguvu ambazo anajua Mungu atampa ili amfufue Lazaro. Yesu anaita “kwa sauti kubwa: ‘Lazaro, njoo huku nje!’” Na Lazaro anatoka nje ‘akiwa amefungwa vitambaa.’ Kwa hivyo, Yesu anaagiza hivi: “Mfungueni, mmwache aende.”—Yohana 11:19-44.

Je, sasa unaelewa kwa nini Yesu alikawia?— Alijua kuwa angetoa ushahidi bora kumhusu Baba yake, Yehova. Na kwa sababu alichagua wakati mzuri, watu wengi waliamini. (Yohana 11:45) Je, unaona jambo tunaloweza kujifunza kutokana na mfano wa Yesu?—

Wewe pia unaweza kuchagua wakati unaofaa wa kutoa ushahidi kuhusu mambo mazuri ambayo Mungu amefanya na atakayofanya wakati ujao. Labda unaweza kuwaeleza wanafunzi wenzako au walimu wako kuyahusu. Hata wakiwa darasani, wanafunzi fulani wamepata nafasi ya kueleza kuhusu baraka ambazo Ufalme wa Mungu utawaletea wanadamu. Ni wazi kwamba huwezi kuwafufua wafu, lakini unaweza kuwasaidia watu wengine wamjue Mungu aliye na uwezo wa kuwafufua wapendwa wetu na ambaye atafanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.

MASWALI:

▪ Kwa nini Yesu anakawia kwenda kumsaidia Lazaro?

▪ Kwa nini Tomasi anasema: ‘Acheni twende pia, ili tukafe pamoja na Yesu’?

▪ Yesu alipata wapi nguvu za kumfufua Lazaro?

▪ Unaweza kufanya nini ili uonyeshe kuwa umejifunza kutokana na mfano wa Yesu?