Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Mamajusi waliomtembelea mtoto Yesu walikuwa akina nani?

Kulingana na masimulizi ya kuzaliwa kwa Yesu katika Injili ya Mathayo, wageni kutoka “sehemu za mashariki” ambao walikuwa wameona nyota ya mfalme mpya, walimpa mtoto Yesu zawadi. Katika maandishi ya Kigiriki ya Injili hiyo wageni hao wanaitwa maʹgoi, yaani, “mamajusi.” (Mathayo 2:1) Tunajua nini kuwahusu?

Maandishi ya mwanahistoria Mgiriki, Herodoto, ndiyo ya zamani zaidi na sahihi zaidi kuhusu Mamajusi hao. Herodoto aliyeishi katika karne ya tano K.W.K., aliandika kwamba Mamajusi walikuwa washiriki wa jamii ya makuhani wa Uajemi waliokuwa na ujuzi mwingi sana katika mambo ya unajimu, ufasiri wa ndoto, na ulozi. Siku za Herodoto, Waajemi walifuata dini ya Zoroaster. Kwa hiyo, yaelekea Mamajusi wanaozungumziwa walikuwa makuhani wa Zoroaster. Kitabu kimoja cha marejeo (The International Standard Bible Encyclopedia) kinasema: “Kwa ujumla, katika ulimwengu wa Wagiriki mágos, [au mamajusi], alikuwa na ujuzi unaopita ule wa binadamu wa kawaida na nyakati nyingine alifanya mambo ya kichawi.”

Wafafanuzi kadhaa “Wakristo,” kama vile Justin Martyr, Origen, na Tertullian, walisema kuwa Mamajusi waliomtembelea Yesu walikuwa wanajimu. Kwa mfano, katika kitabu chake (On Idolatry), Tertullian aliandika: “Tunajua kuna uhusiano kati ya unajimu na uchawi. Kwa hiyo, wale wafasiri wa nyota, ndio waliokuwa wa kwanza . . . kumpa [Yesu] ‘zawadi.’” Kupatana na uelewaji huo, neno maʹgoi linatafsiriwa kuwa “wanajimu” katika Biblia nyingi.

Kwa nini Mathayo alitaja kwamba maneno fulani katika kitabu cha Zekaria ni ya nabii Yeremia?

Maneno hayo yanapatikana kwenye Mathayo 27:9, 10, ambapo Mathayo anazungumza kuhusu pesa ambazo Yuda Iskariote alipewa ili amsaliti Yesu. Andiko hilo linasema: “Ndipo ikatimizwa lililosemwa kupitia nabii Yeremia, akisema: ‘Nao walichukua vile vipande 30 vya fedha, ambavyo ni bei juu ya mtu aliyepigwa bei, . . . nao wakavitoa kwa ajili ya shamba la mfinyanzi.’” Unabii huo kuhusu vipande 30 vya fedha ulitolewa na Zekaria bali si Yeremia.—Zekaria 11:12, 13.

Inaonekana kuwa nyakati nyingine kitabu cha Yeremia, bali si cha Isaya, ndicho kilichokuwa cha kwanza katika mkusanyo wa vitabu vilivyoitwa “Manabii.” (Mathayo 22:40) Kwa hiyo, Mathayo alipomtaja “Yeremia,” alikuwa akirejelea vitabu vyote katika mkusanyo huo, ambao ulipewa jina la kitabu chake cha kwanza. Vitabu hivyo vilitia ndani kitabu cha Zekaria.

Vivyo hivyo, Yesu aliviita “Zaburi” vitabu kadhaa vya Biblia ambavyo pia vinaitwa Maandishi. Kwa hiyo, aliposema kuwa mambo yote yaliyoandikwa kumhusu “katika sheria ya Musa na katika Manabii na Zaburi” lazima yatimizwe, alikuwa akirejelea unabii katika Maandiko ya Kiebrania yote.—Luka 24:44.