Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Ni “Mtendaji wa Mambo Makuu”—Jinsi Nilivyotambua Jambo Hilo

Mungu Ni “Mtendaji wa Mambo Makuu”—Jinsi Nilivyotambua Jambo Hilo

Mungu Ni “Mtendaji wa Mambo Makuu”—Jinsi Nilivyotambua Jambo Hilo

Limesimuliwa na Maurice Raj

Familia yetu pamoja na maelfu ya wahamaji wengine, tulikimbia mojawapo ya mapigano makali zaidi wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Kwa siku kadhaa tulitembea kupitia msitu mkubwa nchini Burma, na kulala chini ya miti wakati wa usiku. Nilikuwa na umri wa miaka tisa. Nilibeba vitu vyangu vyote katika mfuko mdogo nilioufunga mgongoni. Lakini huo ulikuwa mwanzo tu.

ULIKUWA mwaka wa 1942. Ulimwengu ulikuwa vitani, na tulikuwa tunalikimbia jeshi la Wajapani lililokuwa linakaribia. Jeshi hilo lilikuwa limevamia Burma, ambayo sasa inaitwa Myanmar, na kuteka maeneo yenye mafuta ya Yenangyaung. Kabla ya kufika kwenye mpaka wa India, wanajeshi wa Japani walitufikia na kutulazimisha kurudi nyumbani.

Nilipokuwa mtoto, tuliishi Yenangyaung, ambako baba yangu alifanya kazi katika Kampuni ya Mafuta ya Burmah. Baada ya nchi ya Japani kuteka Yenangyaung, yale maeneo yenye mafuta mengi yalianza kushambuliwa kwa mabomu yaliyoangushwa na ndege za kivita za Uingereza. Wakati fulani, familia yetu ilijificha ndani ya handaki kwa siku tatu huku mabomu yakilipuka karibu nasi. Mwishowe tulikimbia kwa mashua mpaka Sale, mji mdogo kando ya Mto Ayeyarwady, au Irrawaddy. Tulifurahi kuwa hai, na tuliishi huko muda wote wa vita.

Msiba Wafanya Tupate Kweli

Ndugu yangu mdogo alizaliwa 1945, mwaka ambao Vita vya Pili vya Ulimwengu viliisha. Baba yangu alifurahi kupata mtoto akiwa katika umri wa uzee. Lakini furaha yake haikudumu. Miezi mitatu baadaye ndugu yangu alikufa. Naye Baba akafa muda mfupi baadaye kutokana na majonzi.

Marafiki waliokuwa na nia ya kunifariji waliniambia kuwa Mungu amewachukua baba na ndugu yangu ili aishi nao mbinguni. Nilitamani sana kuwa pamoja nao! Washiriki wa familia yetu walikuwa wafuasi wa kanisa Katoliki. Nilipokuwa mtoto nilipata mafunzo yangu ya kidini katika kanisa hilo. Nilifundishwa kwamba makasisi na watawa wanaenda moja kwa moja mbinguni, na watu wengine wanaenda toharani, yaani, mahali pa mateso ya muda ili wasafishwe dhambi zao. Nikiwa nimeazimia kujiunga tena na baba na ndugu yangu, niliamua kujiunga na seminari ya Kikatoliki huko Maymyo, mji ambao sasa unaitwa Pyin Oo Lwin, ulio umbali wa kilomita 210 hivi kutoka mahali nilikoishi.

Ili mtu apate kujiunga na seminari hiyo, alihitaji kuwa na elimu nzuri. Nikiwa mhamiaji, nilikuwa nimehudhuria shule kwa miaka miwili tu. Kisha shule zote zikafungwa wakati wa vita. Ingawa shule zilifunguliwa tena, familia yetu ilikuwa inakabili hali ngumu sana ya kiuchumi. Mama yangu alikuwa akinitunza mimi na ndugu zangu wawili na pia watoto watatu wa dada yake mdogo aliyekuwa amekufa. Hakuwa na uwezo wa kutusomesha sisi wavulana.

Kaka yangu alianza kufanya kazi, lakini mimi nilikuwa na umri wa miaka 13 tu, na singeweza kufanya mengi. Ndugu mdogo wa baba yangu, Manuel Nathan, aliishi Chauk, mji uliokuwa karibu na Sale. Niliwaza, ‘Ikiwa nitaondoka nyumbani, hesabu ya watoto wanaohitaji kulishwa itapungua.’ Hivyo, nikaenda Chauk kuishi na baba yangu mdogo, Nathan.

Sikujua kuwa baba yangu mdogo alikuwa amekutana na Mashahidi wa Yehova na alikuwa na hamu ya kuwaeleza wengine mambo aliyojifunza katika Biblia. Alinieleza mambo hayo pole kwa pole. Kwanza alinieleza kuhusu maana ya sala ya Baba Yetu, kama Wakatoliki wanavyoiita. Sala hiyo inaanza hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe.”—Mathayo 6:9, 10, Union Version.

“Kwa hiyo Mungu ana jina,” akanieleza. “Na jina hilo ni Yehova.” Kisha akanionyesha jina hilo katika Biblia. Nilitaka kujua mengi zaidi. Lakini singeweza kusoma vizuri, hata katika lugha yangu mwenyewe ya Tamil. Isitoshe, Biblia na vitabu vinavyotegemea Biblia ambavyo baba yangu mdogo alikuwa navyo vilikuwa katika lugha ya Kiingereza, ambayo sikuielewa vizuri. Ingawa nilikuwa na elimu ndogo, pole kwa pole nilielewa mafundisho ya Biblia. (Mathayo 11:25, 26) Nilianza kuelewa kuwa mafundisho mengi niliyokuwa nimefundishwa hayakutegemea Biblia. Mwishowe nilimwambia: “Baba mdogo, huu ndio ukweli!”

Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilianza kuwaeleza wengine mambo niliyojifunza. Wakati huo kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 77 tu nchini Myanmar. Muda mfupi baadaye, Robert Kirk, Shahidi mmishonari kutoka mji mkuu, Rangoon, ambao sasa unaitwa Yangon, alimtembelea baba yangu mdogo huko Chauk. Nilimwambia Robert kwamba nilikuwa nimejitoa ili kumtumikia Yehova. Hivyo, Desemba 24, 1949 (24/12/1949) nilibatizwa katika Mto Ayeyarwady, ili kuonyesha kuwa nimejitoa kwa Mungu.

Kushinda Vizuizi

Muda mfupi baadaye, nilihamia Mandalay ili kutafuta kazi nzuri. Nilikuwa na lengo la kuwa painia, kama watumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Siku moja nilipokuwa nikitazama mchezo wa mpira wa miguu, nilianguka. Kumbe, nilikuwa nimepatwa na ugonjwa wa kifafa, kwa hiyo nikalazimika kurudi kwa familia yetu ili wanitunze.

Tatizo hilo liliendelea kwa muda wa miaka minane. Nilipoanza kupata nafuu, niliweza kufanya kazi ya kuajiriwa. Ingawa Mama yangu alinizuia kuwa mtumishi wa wakati wote kwa sababu ya hali yangu, siku moja nilimwambia: “Siwezi kungoja zaidi. Ninataka kuwa painia. Yehova atanitunza!”

Mwaka wa 1957, nilihamia Yangon na kuanza upainia. Kwa kushangaza ugonjwa wangu haukunisumbua mpaka miaka 50 baadaye, katika mwaka wa 2007. Sasa ninaudhibiti kwa dawa. Katika mwaka wa 1958, niliwekwa kuwa painia wa pekee, na hilo lilimaanisha ningetumia saa 150 kila mwezi katika kazi ya kuhubiri.

Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa katika kijiji cha Kyonsha, kilicho umbali wa kilomita 110 hivi kaskazini-magharibi ya Yangon. Kulikuwa na kikundi kidogo cha watu waliokuwa wamesoma vitabu vyetu vinavyotegemea Biblia, nao walitaka kujua mengi zaidi. Mimi na Robert tulipowasili katika kijiji hicho, umati wa watu ulikusanyika. Tulijibu maswali yao mengi ya Biblia na tukawaonyesha jinsi ya kuongoza mikutano ya Biblia. Baada ya muda mfupi, baadhi yao walijiunga nasi katika kazi ya kuhubiri. Niliombwa niendelee kutumika katika kijiji hicho. Miezi michache baadaye, kile kikundi kidogo kilikua kwa haraka na kuwa kutaniko. Leo kuna Mashahidi zaidi ya 150 katika eneo hilo.

Baadaye nilipewa mgawo wa kuwa mhudumu anayesafiri, na nilitembelea makutaniko na vikundi mbalimbali kotekote Myanmar. Nilisafiri mamia ya kilomita nikiwa juu ya malori yaliyojaa mizigo, nikatembea katikati ya misitu, nikasafiri kwa mashua kwenye mito, na kuvuka safu za milima. Ingawa sikuwa mwenye nguvu kimwili, nilihisi kwamba Yehova alinipa nguvu za kuendelea.—Wafilipi 4:13.

“Yehova Atakusaidia”

Kisha katika mwaka wa 1962, nikahamishwa na kupelekwa katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Yangon, ambako Robert alianza kunifundisha kazi fulani. Muda mfupi baadaye, wakuu wa serikali walitoa agizo kwamba wamishonari wote ambao wamehamia Myanmar waondoke, na baada ya majuma machache wote wakaondoka. Jambo la kushangaza ni kuwa, nilipewa mgawo wa kusimamia ofisi hiyo ya tawi.

‘Nitafanya kazi hii namna gani?’ Nilijiuliza. ‘Sina elimu ya kutosha wala uzoefu wa kazi.’ Ndugu fulani wenye umri mkubwa walipotambua hangaiko langu, waliniambia, “Maurice, usiwe na wasiwasi. Yehova atakusaidia. Na sote tutakuwa pamoja nawe.” Maneno yao yalinitia moyo sana! Miezi michache baadaye, nilihitaji kuandika ripoti ya kila mwaka ya kazi ya kuhubiri nchini Myanmar ili ichapishwe kwenye Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1967. Kwa miaka 38, niliendelea kuandika ripoti hiyo ya kila mwaka kwa ajili ya nchi hiyo. Mara nyingi, matukio yalionyesha wazi kuwa Yehova kwa kweli anaongoza utendaji wetu.

Kwa mfano, nilipoomba kupata uraia wa Myanmar, nilikosa kyati 450 * zilizohitajika ili kulipia hati yangu ya uraia, hivyo nikaamua kungoja. Kisha, siku moja nilipokuwa nikipita karibu na ofisi ya kampuni iliyokuwa imeniajiri, mwajiri wangu wa zamani aliniona. Aliniita kwa sauti: “Raj, njoo uchukue pesa zako. Ulipoondoka ulisahau kuchukua pesa ulizokuwa ukitengewa kwa ajili ya malipo ya uzeeni.” Zilikuwa kyati 450.

Nilipokuwa ninaondoka katika ofisi hiyo, niliwaza jinsi nitakavyotumia kyati hizo 450. Lakini kwa kuwa zilikuwa pesa kamili nilizohitaji kulipia hati yangu ya uraia, nilihisi kwamba yalikuwa ni mapenzi ya Yehova nitumie pesa hizo kwa kusudi hilo. Uamuzi huo ulikuwa na faida kubwa. Nikiwa raia, ningeweza kukaa katika nchi hiyo, kusafiri bila vizuizi, kuingiza vitabu nchini, na kufanya mambo mengine muhimu kuhusiana na kazi ya kuhubiri nchini Myanmar.

Kusanyiko Lililofanywa Kaskazini

Kufikia mwaka wa 1969, kazi yetu ilikuwa inapanuka kwa haraka mjini Myitkyina, kaskazini mwa Myanmar, kwa hiyo, tukaamua kufanya kusanyiko letu la kwanza katika mji huo. Hata hivyo, tatizo letu kubwa lilikuwa kuandaa usafiri kwa ajili ya Mashahidi wote waliokuwa wakiishi kusini ili waweze kufika. Tulisali kisha tukaomba kampuni ya Reli ya Myanmar ituhifadhie mabehewa sita. Tulishangaa sana ombi letu lilipokubaliwa.

Mwishowe, kila kitu kilikuwa tayari kwa ajili ya kusanyiko. Siku ambayo wajumbe walitazamiwa kufika, tulienda kwenye kituo cha gari-moshi saa sita hivi, huku tukitazamia gari-moshi liwasili mwendo wa saa 8:30 alasiri. Tulipokuwa tunangoja, msimamizi wa kituo alitupa telegramu iliyosema: “Tumeondoa mabehewa sita ya Watch Tower Society.” Alisema kuwa gari-moshi lilishindwa kuvuta mabehewa hayo lilipokuwa likipanda mlima.

Tungefanya nini? Jambo la kwanza tulilofikiria ni kupanga upya kusanyiko. Lakini hilo lingemaanisha kuomba tena vibali vya kufanya kusanyiko, na ingechukua majuma kadhaa! Tulisali kwa Yehova kwa bidii, na tulipokuwa tukifanya hivyo, gari-moshi likawasili kwenye kituo. Hatukuamini macho yetu—gari-moshi lilikuwa na yale mabehewa sita yakiwa yamejaa Mashahidi! Walikuwa wakitabasamu na kutupungia mikono. Tulipowauliza kilichokuwa kimetukia, mmoja wao alitujibu: “Waliondoa mabehewa sita lakini si yale yetu!”

Kati ya mwaka wa 1967 na 1971, idadi ya Mashahidi nchini Myanmar iliongezeka mara mbili na kufikia 600 hivi. Kisha, katika mwaka wa 1978 ofisi ya tawi ikahamishwa hadi kwenye nyumba yenye ghorofa mbili. Miaka 20 baadaye idadi ya Mashahidi iliongezeka na kufikia zaidi ya 2,500. Upanuzi zaidi ulifanywa katika ofisi ya tawi, na mnamo Januari 22, 2000, John E. Barr, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, akaja kutoka Marekani na kutoa hotuba ya kuzindua jengo la ghorofa mbili, ambalo leo linatumika kwa ajili ya ofisi na vyumba vya kulala.

Baraka Nyingi Ambazo Nimepata

Leo, wajitoleaji 52 wanaishi na kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Yangon, na kuna Mashahidi 3,500 hivi wanaotumika katika makutaniko na vikundi 74 kotekote nchini. Ninafurahi kusema kuwa katika mwaka wa 1969, mama yangu mpendwa pia alipata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, muda mfupi kabla ya kifo chake.

Doris Ba Aye, mhudumu painia katika eneo hilo, alikuja kufanya kazi ya kutafsiri katika ofisi yetu ya tawi katikati ya miaka ya 1960. Katika mwaka wa 1959, alikuwa amehudhuria darasa la 32 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead), ambayo inawazoeza wamishonari wa Mashahidi wa Yehova. Urembo wake, utu wake mchangamfu, na hali yake nzuri ya kiroho iliteka moyo wangu. Tulioana mwaka wa 1970. Hadi leo, tumejitolea kwa Yehova na kwa mmoja na mwenzake.

Kwa zaidi ya miaka 60 sasa, nimeshuhudia jinsi ambavyo Mungu ametegemeza kazi ya kuhubiri katika nchi hii. Kwa kweli, yeye ni mkuu na wa kusifiwa sana. Yeye ni “Mtendaji wa mambo makuu,” kama ambavyo nimeshuhudia katika maisha yangu yote.—Zaburi 106:21.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 23 Wakati huo, Kyati hizo zilikuwa sawa na dola 95 hivi za Marekani, kiasi kikubwa cha pesa.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Katika utumishi, Rangoon, Burma, yapata mwaka wa 1957

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nikisafiri kwenda kwenye kusanyiko huko Kalemyo, Burma, mwishoni mwa miaka ya 1970

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ofisi yetu ya tawi yenye kupendeza iliyozinduliwa mwaka wa 2000

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na Doris leo

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tukihubiri nyumba kwa nyumba