Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Paradiso Inayotajwa Katika Biblia Iko Wapi?

Paradiso Inayotajwa Katika Biblia Iko Wapi?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Paradiso Inayotajwa Katika Biblia Iko Wapi?

▪ Yesu alimwahidi hivi mwanamume aliyekaribia kufa na ambaye kwa ujasiri alionyesha imani kwake: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Mwanamume huyo atakuwa naye wapi? Je, Paradiso hiyo itakuwa mbinguni, duniani, au mahali pengine ambapo wanadamu wanangoja hukumu?

Wazazi wetu wa kale waliishi katika Paradiso. Biblia inatueleza hivi: “Yehova Mungu akapanda bustani katika Edeni, kuelekea mashariki, na hapo akamweka mtu ambaye alikuwa amemfanya. . . . Na Yehova Mungu akamchukua mtu na kumweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.” (Mwanzo 2:8, 15) Maneno hayo yalipotafsiriwa katika Kigiriki, “bustani” hiyo iliitwa pa·raʹdei·sos, yaani, “paradiso” katika Kiswahili.

Kama tu vile mume na mke wanavyoweza kuongeza nyumba yao watoto wanapoongezeka, ndivyo wazazi wetu wa kwanza walivyotazamiwa kuipanua Paradiso na kupita mipaka ya Edeni kadiri familia ya kibinadamu ilivyoongezeka. Mungu aliwaambia: “[Jazeni] dunia na kuitiisha.”—Mwanzo 1:28.

Hivyo basi, kusudi la Muumba wetu, lilikuwa wanadamu waishi na kuzaa watoto katika Paradiso hapa duniani. Wangeishi milele katika bustani ya kidunia wakiwa hawahitaji makaburi yoyote. Dunia ingekuwa makao ya kudumu kwa wanadamu wote. Si ajabu kwamba uumbaji unatupendeza sana. Tuliumbwa tuishi katika dunia maridadi.

Je, kusudi la Mungu limebadilika? Hapana. Kwa sababu Yehova anatuhakikishia: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza.” (Isaya 55:11) Zaidi ya miaka 3,000 baada ya mwanadamu kuumbwa, Biblia ilisema kumhusu “Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake” kwamba “hakuiumba tu bila sababu,” bali “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Kusudi la Mungu halijabadilika. Bado dunia itakuwa paradiso.

Jambo la kushangaza ni kwamba masimulizi mengi kuhusu Paradiso ni maelezo tu kuhusu maisha duniani. Kwa mfano, unabii fulani katika kitabu cha Isaya unasema: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.” (Isaya 65:21) Nyumba hujengwa wapi na mizabibu hupandwa wapi? Matunda huliwa wapi? Duniani. Andiko la Methali 2:21 linataja hivi waziwazi: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani.”

Pia Yesu alisema kuhusu paradiso ya kidunia. Ni kweli kuwa aliahidi pia paradiso ya kimbingu, lakini hiyo ni kwa ajili ya watu wachache waliochaguliwa. (Luka 12:32) Baada ya kifo, watu hawa wanafufuliwa na kwenda katika Paradiso ya kimbingu na kujiunga na Kristo ili kutawala Paradiso itakayokuwa duniani. (Ufunuo 5:10; 14:1-3) Watu hao watakaotawala pamoja na Kristo mbinguni watahakikisha kuwa Paradiso ya kidunia, itasimamiwa na kutunzwa vizuri kulingana na kanuni za Mungu.

Yesu alijua kuwa hilo ndilo kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia, kwa kuwa alikuwa pamoja na Baba yake wakati bustani ya Edeni ilipoandaliwa. Kila mtu anayemwamini Yesu leo anaweza kuishi katika paradiso ya kidunia inayokuja. (Yohana 3:16) Yesu anatoa ahadi hii kwa watu kama hao: ‘Mtakuwa pamoja nami katika Paradiso.’—Luka 23:43.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 25]

© FORGET Patrick/SAGAPHOTO.COM/Alamy