Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri Unayoweza Kuwaambia Wengine

Siri Unayoweza Kuwaambia Wengine

Wafundishe Watoto Wako

Siri Unayoweza Kuwaambia Wengine

JE, UMEWAHI kuambiwa siri?— * Kuna siri moja ningetaka kukuambia. Katika Biblia inaitwa “siri takatifu ambayo imewekwa katika siri tangu nyakati za zamani za kale.” (Waroma 16:25) Mwanzoni ni Mungu pekee aliyejua hiyo “siri takatifu.” Hebu tuchunguze jinsi Mungu alivyowajulisha wengine siri hiyo.

Kwanza, Je, unajua maana ya neno “takatifu”?— Linamaanisha kitu kitakatifu, safi, au cha kipekee. Kwa hiyo, siri hiyo inaitwa siri takatifu kwa kuwa inatoka kwa Mungu, ambaye ni mtakatifu. Unafikiri ni nani waliotaka kujua kuhusu siri hiyo ya pekee?— Malaika walitaka kujua. Biblia inasema: “Malaika wanatamani kuchungulia ndani ya mambo hayo.” Ndiyo, walitaka kuelewa siri hiyo takatifu.—1 Petro 1:12.

Yesu alipokuja duniani, alizungumza kuhusu siri hiyo takatifu na akaanza kuielezea. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi mmepewa siri takatifu ya ufalme wa Mungu.” (Marko 4:11) Je, umetambua siri takatifu inahusisha nini?— Inahusisha Ufalme wa Mungu ambao Yesu alitufundisha tusali uje!—Mathayo 6:9, 10.

Sasa acha tuchunguze kwa nini Ufalme wa Mungu ulikuwa siri “tangu nyakati za zamani za kale” mpaka Yesu alipokuja duniani na kuanza kuielezea. Baada ya Adamu na Hawa kuvunja sheria ya Mungu na kuwekwa nje ya shamba la Edeni, watumishi wa Mungu walitambua kuwa kusudi la Mungu bado lilikuwa kuifanya dunia yote iwe paradiso. (Mwanzo 1:26-28; 2:8, 9; Isaya 45:18) Watumishi hao waliandika kuhusu jinsi ambavyo watu wangefurahia maisha duniani chini ya Ufalme wa Mungu.—Zaburi 37:11, 29; Isaya 11:6-9; 25:8; 33:24; 65:21-24.

Sasa, fikiria kuhusu Mtawala wa Ufalme wa Mungu. Je, unajua Mungu alimchagua nani kuwa Mtawala?— Mwana wake “Mkuu wa Amani,” Yesu Kristo. Biblia inasema, “Utawala wa ukuu utakuwa juu ya bega lake.” (Isaya 9:6, 7) Mimi na wewe lazima tupate ‘ujuzi wa siri takatifu ya Mungu, yaani, Kristo.’ (Wakolosai 2:2) Tunapaswa kujua kuwa Mungu alichukua uhai wa malaika wa kwanza (Mwana wa roho) ambaye alimuumba, na kuuweka ndani ya tumbo la Maria. Mwana huyo ambaye alikuwa malaika mwenye nguvu, ndiye aliyetumwa na Mungu kuja duniani kama dhabihu ili tupate uzima wa milele.—Mathayo 20:28; Yohana 3:16; 17:3.

Hata hivyo, kuna mengi ambayo tunahitaji kujua kuhusu siri hiyo zaidi ya kujua tu kuwa Mungu amemchagua Yesu kuwa Mtawala wa Ufalme Wake. Sehemu ya siri hiyo ni kwamba kuna wanaume na wanawake ambao watakuwa mbinguni pamoja na Yesu aliyefufuliwa. Watatawala pamoja naye mbinguni!—Waefeso 1:8-12.

Acha tujifunze majina ya baadhi ya watu watakaotawala pamoja na Yesu mbinguni. Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu kuwa anaenda kuwaandalia mahali. (Yohana 14:2, 3) Ukisoma maandiko yafuatayo, utaona majina ya wanaume na wanawake wachache ambao watatawala na Yesu katika Ufalme wa Baba yake.—Mathayo 10:2-4; Marko 15:39-41; Yohana 19:25.

Kwa muda mrefu, haikujulikana ni watu wangapi ambao wangetawala mbinguni pamoja na Yesu wakiwa sehemu ya Ufalme wake. Lakini sasa tunajua idadi yao. Je, wewe unaijua?— Biblia inasema ni 144,000. Hii pia ni sehemu ya siri hiyo takatifu.—Ufunuo 14:1, 4.

Je, unakubali kuwa “siri takatifu ya ufalme wa Mungu” ndio siri nzuri zaidi ambayo mtu anaweza kujua?— Ikiwa ndivyo, na tujitahidi kujifunza yote tunayoweza kuhusu siri hiyo ili tuweze kuwaelezea watu wengi tuwezavyo kuihusu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.

MASWALI:

▪ Tumejifunza kuhusu siri gani, na kwa nini inaitwa hivyo?

▪ Siri hiyo ni nini, na ni nani aliyekuwa wa kwanza kuwafundisha watu kuihusu?

▪ Umejifunza mambo gani kuhusu siri hiyo?

▪ Unaweza kumweleza rafiki yako jinsi gani kuhusu siri hiyo?

[Picha katika ukurasa wa 31]

Unafikiri malaika walikuwa wakijaribu kujua kuhusu nini?