Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ufalme wa Mungu Ni Hali ya Moyoni Tu?

Je, Ufalme wa Mungu Ni Hali ya Moyoni Tu?

Je, Ufalme wa Mungu Ni Hali ya Moyoni Tu?

“Ufalme wa Mungu unakuja kupitia moyo msikivu,” anasema Papa Benedict wa 16 katika kitabu chake, Jesus of Nazareth. Hivyo ndivyo watu fulani wanavyouelewa Ufalme wa Mungu, yaani, ni badiliko linalotokea ndani ya mtu anapomkubali Yesu Kristo na kuwa na imani kumwelekea. Je, Ufalme wa Mungu ni badiliko linalotokea ndani ya moyo wako, yaani, ufalme unakuwa ‘ndani ya moyo wako tu’?

UFALME ulikuwa jambo muhimu sana kwa Yesu. Ulikuwa “jambo kuu katika mahubiri yake,” anasema Papa Benedict. Katika huduma yake fupi, Yesu alitumia wakati wake mwingi kusafiri kotekote nchini ‘akihubiri habari njema ya ufalme.’ (Mathayo 4:23) Kupitia mafundisho na miujiza yake, Yesu alionyesha wazi kwamba Ufalme unamaanisha mengi zaidi ya mtu kumkubali na kumtii Mungu. Ufalme unatia ndani utawala, hukumu, na baraka za milele.

Utawala na Hukumu

Katika pindi moja mwishoni mwa huduma ya Yesu, mama ya Yakobo na Yohana—wanafunzi wa Yesu waliokuwa na ukaribu naye—alimwendea Yesu na kusema: “Toa agizo ili hawa wanangu wawili waketi, mmoja upande wako wa kuume na mmoja upande wako wa kushoto, katika ufalme wako.” (Mathayo 20:21) Bila shaka, hakuwa akizungumzia hali fulani iliyokuwa katika moyo wa watoto wake. Alielewa kwamba Ufalme ulihusisha kutawala pamoja na Yesu, na alitaka watoto wake washiriki katika utawala huo. Kwa kweli, Yesu aliwaahidi mitume wake waaminifu 11 kwamba watakuwa katika Ufalme wake na “kuketi juu ya viti vya ufalme” na “kuhukumu” pamoja naye. (Luka 22:30) Wafuasi wake walielewa kwamba Ufalme wa Yesu ungekuwa utawala au serikali halisi.

Namna gani kuhusu watu kwa ujumla katika siku za Yesu? Je, walielewa Ufalme kuwa badiliko linalotokea ndani ya moyo wa mtu, au walitazamia mengi zaidi? Muda mfupi kabla ya Pasaka ya 33 W.K. Yesu alipokuwa akiingia Yerusalemu akiwa amepanda mwana-punda, umati wa watu ulimkaribisha na baadhi yao wakapaza sauti: “Mwokoe Mwana wa Daudi, tunaomba!” (Mathayo 21:9) Kwa nini walisema hivyo? Yaelekea walitambua kuwa Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa na kwamba Mungu atampa Ufalme unaodumu milele, “kiti cha ufalme cha Daudi baba yake.” Walitamani ukombozi, amani, na haki ambayo Ufalme huo ungeleta.—Luka 1:32; Zekaria 9:9.

Baraka za Milele

Hata watu ambao hawakupendezwa na huduma ya Yesu walijua kwamba alifundisha kuhusu Ufalme. Wakati wa kuuawa kwa Yesu, mhalifu aliyekuwa ametundikwa kando yake alimsihi hivi: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu alimwambia nini? Alimhakikishia hivi mtu huyo aliyekuwa karibu kufa: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:42, 43.

Kwa wazi, mnyang’anyi huyo aliamini kwamba baada ya kufufuliwa, baadaye Yesu angepokea au kuingia katika Ufalme. Yesu angekuwa na mamlaka na pia tamaa ya kumfufua na kumsaidia mtu huyo—pamoja na mamilioni ya watu wengine—wafanye mabadiliko. Ndiyo, akiwa amewekwa kuwa Mtawala huko mbinguni, Yesu angeleta baraka za milele kwa wanadamu duniani pote kupitia Ufalme.—Yohana 5:28, 29.

Ufalme Katikati Yao

Je, Yesu hakusema kwamba “ufalme wa Mungu umo katikati yenu”? Ndiyo, maneno hayo ya Yesu yanapatikana katika andiko la Luka 17:21. Kwa kweli, baadhi ya tafsiri za Biblia zinasema kwamba “ufalme wa Mungu umo ndani yenu,” nazo nyingine zinasema “uko kati yenu.” (Kwa mfano, ona Union Version na Biblia Habari Njema.) Yesu alimaanisha nini aliposema maneno hayo?

Maneno yanayozunguka mstari huo yanaonyesha kwamba Yesu alielekeza maneno hayo kwa wafuasi wenye upinzani wa dini ya Kiyahudi walioitwa Mafarisayo. Walikuwa na matazamio fulani kuhusiana na Masihi na Ufalme wake. Kwa maoni yao, Masihi “angekuja na mawingu ya mbinguni” kama Mfalme mwenye utukufu, ili kuwakomboa Wayahudi kutoka kwa Waroma na kuurudisha ufalme wa Israeli. (Danieli 7:13, 14) Hata hivyo, Yesu, aliwaonyesha kuwa maoni yao yana makosa kwa kuwaambia: “Ufalme wa Mungu hautakuja kwa wonyesho wenye kutokeza sana.” Kisha akaongeza kusema hivi: “Tazama! ufalme wa Mungu umo katikati yenu.”—Luka 17:20, 21.

Ingawa Yesu alifundisha na kufanya miujiza iliyothibitisha kwamba alikuwa Mfalme aliyeahidiwa wa Ufalme huo, Mafarisayo wenye nia mbaya na wasiokuwa na imani waliendelea kumpinga hata zaidi. Walitilia shaka kwamba Yesu ndiye Masihi. Hivyo akawaeleza waziwazi: Ufalme uliowakilishwa na Mfalme aliyewekwa rasmi, ulikuwa ‘katikati yao.’ Hakumaanisha kwamba wajichunguze ndani yao. * Yesu na wanafunzi wake walikuwa wamesimama mbele yao. “Ufalme wa Mungu uko kati yenu,” akawaambia.—Luka 17:21, BHN.

Ufalme Ambao Ni Muhimu Kwako

Ingawa Ufalme wa Mungu haukai ndani ya mioyo ya wanadamu wenye dhambi, unapaswa kuwa jambo muhimu kwako. Kupitia mafundisho na miujiza yake, Yesu alijitahidi kuwasaidia wasikilizaji wake wawe na imani katika utawala mwadilifu ambao ungeleta amani na usalama wa kweli. Alitaka wawe na imani ambayo ingewasaidia kuboresha maisha yao. Hata aliwafundisha wasali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Wasikilizaji wengi wa Yesu waliguswa na maneno yake na wakawa na imani iliyowachochea kumfuata Yesu ili kuja kupata baraka za Ufalme wa Mungu.

Je, ungependa kuwa na imani ya aina hiyo? Basi, unapaswa kufanya nini ili usitawishe imani ya aina hiyo? Kumbuka maneno ya utangulizi ya Yesu katika Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mathayo 5:3) Tunakutia moyo ujifunze Biblia na Mashahidi wa Yehova waliokupa gazeti hili. Na utakuwa na tumaini, si katika badiliko fulani linalotokea katika moyo wako tu, bali katika utawala mwadilifu na wa haki—Ufalme utakaoleta amani na usalama kwa wote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Katika Kigiriki cha awali neno “yenu” kwenye fungu la maneno ambalo limetafsiriwa “kati yenu” katika Biblia fulani, liko katika hali ya wingi na linawarejelea Mafarisayo ambao Yesu alikuwa akizungumza nao. Kwa kweli, Yesu hakuwa akizungumza kuhusu badiliko fulani lililotokea ndani ya mioyo ya Mafarisayo, wala hakumaanisha kwamba walikuwa na mioyo misikivu.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Je, Ufalme wa Mungu ulikuwa katika mioyo ya wapinzani wa Yesu waliokuwa wakaidi na wauaji?