Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Ana Kusudi Gani Kuelekea Dunia?

Mungu Ana Kusudi Gani Kuelekea Dunia?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Mungu Ana Kusudi Gani Kuelekea Dunia?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Mungu ana kusudi gani kuelekea dunia?

Dunia ni makao ya mwanadamu. Baada ya Mungu kuumba malaika waishi mbinguni, alimuumba mwanadamu aifurahie dunia. (Ayubu 38:4, 7) Hivyo, Yehova alimweka mwanadamu wa kwanza katika paradiso yenye kupendeza iliyoitwa Edeni, na kumpa yeye na watoto ambao angepata tazamio la kufurahia maisha duniani milele.—Mwanzo 2:15-17; soma Zaburi 115:16.

Bustani ya Edeni ilikuwa katika sehemu ndogo tu ya dunia. Wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, walipaswa kuwa na watoto. Kadiri ambavyo familia ya kibinadamu ingeongezeka, ndivyo ambavyo ingeilima dunia na kuifanya iwe paradiso. (Mwanzo 1:28) Dunia haitaharibiwa kamwe.—Soma Zaburi 104:5.

2. Kwa nini dunia si paradiso leo?

Adamu na Hawa hawakumtii Mungu, hivyo wakafukuzwa kutoka katika Edeni. Wakati huo paradiso ilipotea, na hakuna mtu ambaye amefanikiwa kuirudisha. Biblia inasema: “Dunia imetiwa mkononi mwa mwovu.”—Ayubu 9:24; soma Mwanzo 3:23, 24.

Lakini Yehova hajasahau kusudi lake la awali, wala hawezi kushindwa. (Isaya 45:18) Atawarudisha wanadamu katika hali ambayo alikusudia wawe nayo.—Soma Zaburi 37:11.

3. Mungu atairudisha amani duniani jinsi gani?

Ili wanadamu wafurahie amani, ni lazima Mungu awaondoe watu waovu kwanza. Katika vita vya Har-Magedoni, malaika wa Mungu watawaharibu watu wote wanaompinga. Shetani atafungwa kwa kipindi cha miaka 1,000, lakini watu wanaompenda Mungu wataokoka ili wafurahie mfumo mpya wa mambo hapa duniani.—Soma Ufunuo 16:14, 16; 20:1-3; 21:3, 4.

4. Kuteseka kutaisha lini?

Katika kipindi hicho cha miaka 1,000, Yesu ataitawala dunia kutoka mbinguni na kuirudisha kuwa paradiso. Pia, atafuta dhambi za wale wanaompenda Mungu. Hivyo, Yesu ataondoa magonjwa, uzee, na kifo.—Soma Isaya 11:9; 25:8; 33:24; 35:1.

Mungu ataondoa uovu duniani lini? Yesu alitoa “ishara” ambayo ingeonyesha kuwa mwisho uko karibu. Hali duniani leo zinatishia uhai wa mwanadamu na zinaonyesha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.”—Soma Mathayo 24:3, 7-14, 21, 22; 2 Timotheo 3:1-5.

5. Ni nani watakaoishi katika Paradiso inayokuja?

Yesu aliwaagiza wafuasi wake wafanye wanafunzi na kuwafundisha njia za Mungu za upendo. (Mathayo 28:19, 20) Yehova anaandaa mamilioni ya watu ulimwenguni pote ili waje kuishi katika mfumo mpya wa mambo hapa duniani. (Sefania 2:3) Katika Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova, watu wanajifunza jinsi ya kuwa waume na wake bora, na pia wazazi bora. Watoto na wazazi hujifunza pamoja msingi wa kuwa na imani katika wakati ujao ulio bora.—Soma Mika 4:1-4.

Katika Jumba la Ufalme, utakutana na watu wanaompenda Mungu na wanaotaka kujifunza jinsi wanavyoweza kumpendeza.—Soma Waebrania 10:24, 25.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 3 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.