Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nimeamini”

“Nimeamini”

Igeni Imani Yao

“Nimeamini”

MARTHA angeweza kuwazia kaburi la ndugu yake—pango lililokuwa limefunikwa kwa jiwe. Alilemewa na huzuni nyingi sana. Hangeweza kuamini kuwa ndugu yake mpendwa Lazaro amekufa. Zile siku nne zilizokuwa zimepita tangu Lazaro afe zilionekana kuwa kipindi kirefu cha huzuni. Katika kipindi hicho walitembelewa na wageni wengi na kupokea rambirambi nyingi.

Na sasa Yesu, mtu ambaye Lazaro alimpenda sana, alikuwa amesimama mbele yake. Kumwona Yesu tena kulimwongezea huzuni hata zaidi, kwa kuwa Yesu pekee ndiye ambaye angeweza kumwokoa ndugu yake. Hata hivyo, Martha alifarijika kwa kadiri fulani kuwa pamoja na Yesu nje ya mji mdogo wa Bethania uliokuwa kwenye kilima. Baada ya kuwa pamoja na Yesu kwa muda mfupi, Martha alitiwa moyo na fadhili na huruma za Yesu. Yesu alimuuliza maswali ambayo yalimsaidia kufikiria kwa uzito tumaini la ufufuo. Mazungumzo hayo yalimfanya Martha atamke maneno haya muhimu: “Nimeamini kwamba wewe ndiye Kristo Mwana wa Mungu, Yule anayekuja ulimwenguni.”—Yohana 11:27.

Martha alikuwa mwanamke mwenye imani yenye nguvu. Yale machache ambayo Biblia inatuambia kumhusu yanaweza kutusaidia kuimarisha imani yetu. Ili kuelewa jambo hilo, acheni tufikirie simulizi la kwanza katika Biblia kumhusu Martha.

‘Kuhangaika na Kusumbuka’

Ilikuwa miezi kadhaa mapema. Bado Lazaro alikuwa hai na mwenye afya njema. Alikuwa akitazamia kumkaribisha Yesu Kristo, mgeni muhimu kuliko wote, nyumbani kwake Bethania. Familia ya Lazaro, Martha, na Maria ilikuwa ya pekee—ndugu na dada wawili, watu wazima ambao waliishi pamoja. Baadhi ya watafiti wamedokeza kwamba huenda Martha alikuwa ndiye mkubwa kati yao, kwa kuwa ndiye aliyekuwa akifanya maandalizi kwa ajili ya wageni na wakati fulani anatajwa kwanza. (Yohana 11:5) Si rahisi kujua ikiwa yeyote kati yao alifunga ndoa. Vyovyote vile, walikuwa marafiki wa karibu wa Yesu. Wakati wa huduma yake huko Yudea, ambako alipata upinzani na uhasama mkubwa, Yesu aliishi katika nyumba yao. Bila shaka, alithamini sana utulivu, amani, na utegemezo alioupata katika nyumba hiyo.

Martha alichangia sana hali nzuri na ukarimu katika nyumba yao. Martha alikuwa mwanamke mwenye bidii, na mara nyingi alikuwa na shughuli nyingi sana. Hata kwenye pindi hii ambapo Yesu aliwatembelea, bado Martha alikuwa mwenye shughuli nyingi. Mara moja alipanga kutayarisha mlo wa pekee, yaani, vyakula vya aina mbalimbali kwa ajili ya mgeni wake maalumu, na pia labda watu walioandamana naye. Wakati huo, lilikuwa jambo muhimu sana kumkaribisha mgeni. Mgeni alipowasili, alikaribishwa kwa busu, akavuliwa viatu, akaoshwa miguu, na kupakwa mafuta yenye marashi kichwani. (Luka 7:44-47) Ilikuwa ni desturi kuwatunza wageni vizuri, kuwaandalia mahali pazuri pa kulala, na kuwapa chakula kizuri.

Martha na Maria walikuwa na kazi nyingi ya kumtunza mgeni wao maalumu. Bila shaka, Maria ambaye nyakati nyingine anafikiriwa kuwa msikivu na mwenye kutafakari zaidi, alimsaidia dada yake mwanzoni. Hata hivyo, Yesu alipofika, mambo yalibadilika. Yesu alitumia vizuri pindi hiyo kuwafundisha watu waliokuwapo. Tofauti na viongozi wa dini wa nyakati hizo, Yesu aliwaheshimu wanawake na alikuwa tayari kuwafundisha kuhusu Ufalme wa Mungu, kichwa kikuu cha mahubiri yake. Maria alifurahia pindi hiyo, hivyo akakaa miguuni pa Yesu na kumsikiliza kwa makini sana.

Tunaweza kuwazia mfadhaiko ambao Martha alikuwa nao moyoni. Kwa vile alikuwa akitayarisha vyakula vya aina mbalimbali na kufanya mambo mengi kwa ajili ya wageni wake, Martha aliendelea kufadhaika hata zaidi na kutokazia fikira mambo muhimu. Alipokuwa akipita-pita na kumwona dada yake ameketi tu bila kumsaidia, je, uso wake ulibadilika rangi kidogo, akashusha pumzi kwa nguvu, au hata kukunja uso? Hilo lisingeshangaza. Hangeweza kufanya kazi zote hizo peke yake!

Hatimaye Martha hakuweza kuendelea kuvumilia. Alimkatiza Yesu na kufoka: “Bwana, hujali kwamba dada yangu ameniacha peke yangu kushughulikia mambo? Kwa hiyo, mwambie aje anisaidie.” (Luka 10:40) Hayo yalikuwa maneno mazito. Baadhi ya Biblia hutafsiri swali lake hivi: “Bwana, huoni vibaya . . . ?” Kisha akamwomba Yesu amrekebishe Maria na kumwagiza amsaidie.

Huenda jibu la Yesu lilimshangaza Martha, kama ambavyo limewashangaza wasomaji wengi wa Biblia tangu wakati huo. Kwa upole alisema: “Martha, Martha, wewe unahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi. Ingawa hivyo, mambo machache ndiyo yanayohitajiwa, au moja tu. Yeye, Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa kwake.” (Luka 10:41, 42) Yesu alimaanisha nini? Je, alimaanisha kwamba Martha alihangaikia zaidi mambo ya kimwili? Je, alikuwa akipuuza kazi yake ngumu ya kutayarisha mlo mzuri?

Hapana. Yesu alijua vizuri kwamba Martha alikuwa mwenye upendo na nia nzuri. Zaidi ya hilo, hakuona kwamba ilikuwa vibaya kuonyesha ukarimu mwingi hivyo. Alikuwa amehudhuria kwa hiari “karamu kubwa” ambayo Mathayo alikuwa amemwandalia wakati fulani mapema. (Luka 5:29) Suala kuu halikuwa mlo ambao Martha aliandaa; badala yake, lilikuwa jambo alilotanguliza. Martha alikazia uangalifu sana mlo wake uliohusisha mambo mengi hivi kwamba alikosa kufikiria jambo lililokuwa muhimu zaidi. Jambo gani hilo?

Yesu, Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova Mungu, alikuwa katika nyumba ya Martha akifundisha kweli. Hakukuwa na jambo lingine—kutia ndani mlo wake mzuri na matayarisho yake—lililokuwa muhimu zaidi ya hilo. Bila shaka, Yesu alihuzunika kwamba Martha alikuwa akipoteza nafasi hiyo ya pekee ya kuimarisha imani yake, lakini akamruhusu afanye uamuzi wake mwenyewe. Hata hivyo, Martha hakupaswa kumwomba Yesu amlazimishe Maria apoteze nafasi hiyo pia.

Hivyo, kwa upole alimrekebisha Martha, akirudia jina lake kwa utulivu ili kumtuliza asiwe na mfadhaiko, na kumhakikishia kwamba hakukuwa na haja ya ‘kuhangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi.’ Mlo usiohusisha mambo mengi unatosha, hasa kunapokuwa na karamu ya kiroho. Hivyo, hangeweza kumpokonya Maria “fungu jema” ambalo alikuwa amechagua, yaani, kufundishwa na Yesu!

Simulizi hili linaloeleza yaliyotokea nyumbani mwa Martha lina mambo mengi ambayo wafuasi wa Kristo leo wanaweza kujifunza. Hatupaswi kuruhusu chochote kitunyime nafasi ya kutosheleza ‘uhitaji wetu wa kiroho.’ (Mathayo 5:3) Ingawa tungependa kuiga ukarimu wa Martha na bidii yake, hatupaswi kamwe ‘kuhangaika na kusumbuka’ kuhusu mambo yasiyo muhimu tunapokaribisha wageni. Tunashirikiana na waamini wenzetu ili kutiana moyo na kupeana zawadi za kiroho, bali si kuandaa chakula kingi na cha gharama ya juu. (Waroma 1:11, 12) Hata chakula kisichohusisha mambo mengi kinaweza kufanya pindi hizo ziwe zenye kujenga.

Ndugu Mpendwa Afa na Kufufuliwa

Je, Martha alikubali rekebisho lenye upole la Yesu na kujifunza kutokana nalo? Hatuhitaji kutafuta jibu. Anapoanza kuelezea simulizi kumhusu ndugu ya Martha, mtume Yohana anasema: “Basi Yesu alimpenda Martha na dada yake na Lazaro.” (Yohana 11:5) Miezi kadhaa ilikuwa imepita tangu Yesu atembelee Bethania. Kwa wazi, Martha hakununa wala hakuwa na kinyongo baada ya kushauriwa na Yesu. Aliliweka shauri hilo moyoni. Kuhusu jambo hilo pia, Martha alituwekea mfano mzuri wa imani, kwani mara kwa mara sote tunahitaji kurekebishwa.

Ndugu yake alipoanza kuugua, Martha alijitahidi kumtunza. Alifanya kila alichoweza ili kupunguza maumivu yake na kumsaidia apone. Hata hivyo, hali ya Lazaro ilizidi kuzorota. Kila siku dada zake walikuwa kando yake wakimtunza. Hebu wazia Martha akiutazama uso mchovu wa ndugu yake, akikumbuka miaka mingi waliyokuwa pamoja, shangwe na huzuni walizopitia pamoja.

Ilipoonekana wazi kwamba hali ya Lazaro inazidi kuwa mbaya hata zaidi, Martha na Maria walimtumia Yesu ujumbe. Yesu alikuwa akihubiri katika eneo ambalo angehitaji kutembea siku mbili ili afike. Ujumbe wao ulikuwa mfupi: “Bwana, ona! yule unayempenda ni mgonjwa.” (Yohana 11:1, 3) Walijua kwamba Yesu alimpenda ndugu yao, na walikuwa na imani kwamba Yesu angefanya chochote awezacho ili kumsaidia rafiki yake. Je, walikuwa na tumaini kwamba Yesu angewasili kabla ya ndugu yao kufa? Ikiwa ndivyo, tumaini lao halikutimia kwani Lazaro alikufa.

Martha na Maria walimwombolezea ndugu yao, wakapanga mazishi yake na kupokea wageni wengi kutoka Bethania na maeneo jirani. Hata hivyo, hakukuwa na ujumbe wowote kutoka kwa Yesu. Bila shaka, Martha alizidi kuchanganyikiwa. Hatimaye, siku nne baada ya Lazaro kufa, Martha alisikia kwamba Yesu alikuwa akikaribia kuingia mjini. Akiwa mwanamke mwenye bidii, hata katika pindi hiyo ya huzuni, Martha aliinuka na bila kumwambia Maria, akakimbia kukutana na Yesu.—Yohana 11:20.

Alipomwona Yesu, akasema mambo yaliyokuwa yakiwasumbua yeye na Maria kwa siku kadhaa: “Bwana, kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Bado Martha alikuwa na imani na tumaini. Akaongeza hivi: “Hata hivyo sasa ninajua kwamba mambo mengi kadiri unayomwomba Mungu, Mungu atakupa.” Hivyo, mara moja Yesu akasema maneno haya ili kuimarisha tumaini lake: “Ndugu yako atafufuka.”—Yohana 11:21-23.

Martha alifikiri kwamba Yesu anazungumzia ufufuo wa wakati ujao, hivyo akajibu: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:24) Imani yake katika ufufuo ilikuwa imara. Baadhi ya viongozi wa dini ya Kiyahudi wanaoitwa Masadukayo, walikuwa wakipinga kwamba kutakuwa na ufufuo hata ingawa jambo hilo limeelezwa waziwazi katika Maandiko yaliyoongozwa na roho. (Danieli 12:13; Marko 12:18) Hata hivyo, Martha alijua kwamba Yesu alikuwa akifundisha kuhusu tumaini la ufufuo na hata aliwafufua watu—ingawa hakuwahi kumfufua mtu yeyote aliyekuwa amekufa kwa muda mrefu kama Lazaro. Hakujua mambo ambayo yalikuwa karibu kutukia.

Kisha, Yesu akasema maneno haya yasiyoweza kusahaulika: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” Kwa kweli, Yehova Mungu amempa Mwana wake mamlaka ya kufufua watu duniani pote wakati ujao. Yesu alimuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Martha akatoa jibu lililozungumziwa katika utangulizi wa makala hii. Alikuwa na imani kuwa Yesu ndiye Kristo, au Masihi, kwamba ndiye Mwana wa Yehova Mungu, na kwamba manabii walikuwa wametabiri kwamba angekuja ulimwenguni.—Yohana 5:28, 29; 11:25-27.

Je, Yehova Mungu na Yesu Kristo, Mwana wake, wanathamini imani kama hiyo? Mambo ambayo hatimaye Martha aliyaona yanatoa majibu yaliyo wazi. Martha alikimbia kumwita dada yake. Kisha akaona Yesu akiwa na huzuni sana alipokuwa akizungumza na Maria na waombolezaji wengi waliokuwa pamoja naye. Akamwona Yesu akitokwa na machozi kwa sababu ya huzuni inayoletwa na kifo. Akamsikia akitoa agizo ili jiwe lililokuwa limefunika kaburi la ndugu yake liondolewe.—Yohana 11:28-39.

Akiwa mtu asiyesita kuchukua hatua, Martha alipinga kwamba mwili ulikuwa unanuka, kwa kuwa siku nne zilikuwa zimepita tangu Lazaro afe. Ndipo Yesu akamkumbusha hivi: “Je, sikukuambia kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?” Martha aliamini na kuona utukufu wa Yehova Mungu. Papo hapo, Mungu akamwezesha Mwana wake amfufue Lazaro! Fikiria mambo yaliyobaki katika kumbukumbu la Martha hadi alipokufa: Yesu akiita kwa sauti, “Lazaro, njoo huku nje!”; sauti iliyosikika kwa mbali pangoni wakati Lazaro alipoinuka na kutembea polepole kuelekea mlango wa pango, huku akiwa bado amefungwa vitambaa vilivyotumiwa kufungia mwili wake; agizo la Yesu kwamba ‘wamfungue na kumwacha aende’; na bila shaka, msisimuko ambao yeye na dada yake Maria walikuwa nao walipokumbatiana na ndugu yao. (Yohana 11:40-44) Huzuni iliyokuwa moyoni mwa Martha ikaisha!

Simulizi hilo linaonyesha kuwa ufufuo wa wafu si ndoto tu, bali ni fundisho la Biblia lenye kugusa moyo. Pia, ufufuo ni hakika na umewahi kutokea. Kama walivyofanya katika kisa cha Martha, Maria, na Lazaro, Yehova na Mwana wake wanafurahia kuwapa thawabu watu wenye imani. Watakupa zawadi kama hiyo ikiwa utakuwa na imani yenye nguvu kama ile ya Martha. *

“Martha Alikuwa Akihudumu”

Biblia inamtaja tena Martha mara moja. Ilikuwa ni juma la mwisho la Yesu kuwa hai hapa duniani. Akijua wazi hali ngumu iliyokuwa ikimkabili, Yesu alichagua tena kukaa katika yale makao yenye amani na utulivu huko Bethania. Kutoka huko angeweza kutembea kilomita tatu hadi Yerusalemu. Yesu na Lazaro walikuwa wakila katika nyumba ya Simoni mwenye ukoma, hapo ndipo tunaposoma kumhusu Martha kwa mara ya mwisho: “Martha alikuwa akihudumu.”—Yohana 12:2.

Kwa kweli, mwanamke huyo alikuwa na bidii! Tunaposoma mara ya kwanza kumhusu katika Biblia, anafanya kazi; tunapomaliza kusoma simulizi lake, bado anafanya kazi, akifanya yote awezayo kuwahudumia wengine. Makutaniko ya wafuasi wa Kristo leo yamebarikiwa kuwa na wanawake kama Martha—wenye bidii na ukarimu, siku zote wakionyesha imani yao kwa matendo wanapojitoa. Yaelekea hivyo ndivyo Martha alivyoendelea kufanya. Ikiwa ndivyo, alitenda kwa busara, kwa kuwa bado kulikuwa na vikwazo mbele yake.

Baada ya siku chache, Martha alihitaji kuvumilia kifo kibaya cha Yesu. Zaidi ya hayo, wauaji walewale wanafiki ambao walimuua Yesu waliazimia kumuua Lazaro pia, kwa kuwa ufufuo wa Lazaro ulikuwa unaimarisha imani ya wengi. (Yohana 12:9-11) Hatimaye kifo kilitenganisha upendo uliomwunganisha Martha na wadogo zake. Hatujui hilo lilitokea wakati gani au jinsi gani, lakini tunaweza kuwa na uhakika kwamba imani yenye thamani ya Martha ilimsaidia kuvumilia hadi mwisho. Ndio maana leo Wakristo wanajaribu kuiga imani ya Martha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 27 Ili kujifunza mengi juu ya fundisho la Biblia kuhusu ufufuo, ona sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Hata alipokuwa akiomboleza, Martha alimruhusu Yesu amsaidie kufikiria mambo yenye kuimarisha imani

[Picha katika ukurasa wa 12]

Hata ingawa alikuwa ‘akihangaika na kusumbuka,’ kwa unyenyekevu Martha alikubali kurekebishwa

[Picha katika ukurasa wa 15]

Imani ya Martha katika Yesu ilithawabishwa alipoona ndugu yake akifufuliwa