Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati Wazee Watakapokuwa Vijana Tena

Wakati Wazee Watakapokuwa Vijana Tena

Mkaribie Mungu

Wakati Wazee Watakapokuwa Vijana Tena

NI NANI kati yetu anayefurahia madhara ya uzee—ngozi iliyokunjamana, macho yasiyoona vizuri, masikio yasiyosikia vizuri, na miguu isiyo na nguvu? Huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini Mungu alituumba tukiwa na uwezo wa kufurahia nguvu za ujana, kisha tunaanza kuwa na wasiwasi kuhusu madhara ya uzee?’ Jambo linalotia moyo ni kwamba halikuwa kusudi la Mungu tuzeeke. Hivyo, kwa upendo amekusudia kutuondolea uzee! Ona maneno ambayo mzee wa ukoo Ayubu, aliambiwa kwenye Ayubu 33:24, 25.

Fikiria hali ya Ayubu, mwanamume mshikamanifu aliyependwa na Yehova. Shetani alitilia shaka uaminifu wake bila Ayubu mwenyewe kujua. Alisema kuwa Ayubu alimtumikia Mungu kwa sababu za kibinafsi. Kwa kuwa Yehova alikuwa na imani na Ayubu na pia uwezo wa kuondoa madhara, alimruhusu Shetani amjaribu Ayubu. Ndipo Shetani “akampiga Ayubu kwa majipu hatari kuanzia wayo wa mguu wake mpaka kwenye utosi wa kichwa chake.” (Ayubu 2:7) Mwili wa Ayubu ulijaa funza, na ngozi yake ikafanyiza vikoko, ikawa nyeusi, na kuanguka. (Ayubu 7:5; 30:17, 30) Hebu wazia maumivu aliyokuwa nayo. Licha ya hayo, Ayubu aliendelea kuwa mwaminifu na kusema: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!”—Ayubu 27:5.

Hata hivyo, Ayubu alifanya kosa kubwa. Alipoona ni kama anakaribia kufa alianza kuhangaikia mno uadilifu wake, “a[ki]itangaza nafsi yake mwenyewe kuwa adilifu badala ya Mungu.” (Ayubu 32:2) Elihu msemaji wa Mungu alimkemea Ayubu na wakati huohuo pia akampa ujumbe huu mzuri kutoka kwa Mungu: “Mwachilie [Ayubu] ili asishuke chini kuingia shimoni [kaburi]! Nimepata fidia! Nyama yake na iwe laini kuliko wakati wa ujana; na arudi kwenye siku za nguvu za ujana wake.” (Ayubu 33:24, 25) Hapana shaka kuwa maneno hayo yalimpa Ayubu matumaini makubwa. Haikuwa lazima aendelee kuteseka mpaka kifo. Kama Ayubu angetubu, Mungu angefurahi kukubali fidia kwa ajili yake na angemwondolea misiba. *

Ayubu alikubali kwa unyenyekevu kurekebishwa, na alitubu. (Ayubu 42:6) Yehova alikubali fidia kwa ajili ya Ayubu na kuiruhusu ifunike kosa lake. Jambo hilo lilifanya iwezekane kwa Mungu kumbariki Ayubu na kumrudisha katika hali nzuri. Yehova “a[li]ubariki mwisho wa Ayubu baadaye kuliko mwanzo wake.” (Ayubu 42:12-17) Wazia kitulizo ambacho Ayubu alipata, wakati Mungu alipomwondolea ugonjwa wake mbaya na nyama yake ikawa “laini kuliko wakati wa ujana”! Hiyo ilikuwa mojawapo ya baraka nyingi alizopata.

Fidia ambayo Mungu aliikubali kwa ajili ya Ayubu ilikuwa na manufaa kidogo, kwa kuwa Ayubu bado alikuwa mtu asiye mkamilifu na baadaye alikufa. Sisi tuna fidia bora zaidi. Kwa upendo Yehova alimtoa Yesu, Mwana wake, ili awe fidia kwa ajili yetu. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16) Wote wanaoweka imani yao katika fidia hiyo, wana tazamio la kuishi milele katika dunia paradiso. Katika ulimwengu huo mpya unaokuja, Mungu atawaondolea uzee wanadamu waaminifu. Tunakutia moyo ujifunze mengi zaidi kuhusu jinsi unavyoweza kuishi katika wakati ambapo wazee wataona ‘nyama yao ikiwa laini kuliko wakati wa ujana.’

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Aprili (Mwezi wa 4):

Ayubu 16-37

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Neno “fidia” ambalo limetumiwa hapa linamaanisha “kufunika.” Katika kisa cha Ayubu, huenda fidia ilikuwa dhabihu ya mnyama, ambayo Mungu angeikubali ili kufunika, au kufanya upatanisho kwa ajili ya kosa lake.—Ayubu 1:5.