Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu—Kwa Nini Alikufa?

Yesu—Kwa Nini Alikufa?

Yesu​—Kwa Nini Alikufa?

“Mwana wa binadamu alikuja . . . kutoa nafsi yake [au, uhai] iwe fidia badala ya wengi.”—MARKO 10:45.

YESU alijua mambo ambayo yangempata. Alielewa kuwa hangeishi kwa amani. Badala yake, uhai wake ungekatizwa akiwa bado katika umri wa miaka 30 hivi, naye alikuwa amejitayarisha kabisa kukabili kifo chake.

Biblia inaonyesha kuwa kifo cha Yesu kilikuwa na umuhimu mkubwa. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kuwa kifo cha Yesu kinatajwa moja kwa moja mara 175 hivi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo au Agano Jipya. Hata hivyo, kwa nini Yesu alipaswa kuteseka na kufa? Tunahitaji kujua jambo hilo kwa kuwa kifo chake kinaweza kuwa na uvutano mkubwa katika maisha yetu.

Yesu alitazamia kupatwa na nini? Katika mwaka wa mwisho wa maisha yake, Yesu aliwaeleza mara kadhaa wanafunzi wake kuhusu mateso na kifo ambacho kingempata. Alipokuwa njiani kwenda Yerusalemu kuadhimisha Pasaka yake ya mwisho, aliwaambia hivi mitume wake 12: “Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani, na waandishi, nao watamhukumia kifo na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa, nao watamdhihaki, watamtemea mate, watampiga mijeledi na kumuua.” * (Marko 10:33, 34) Kwa nini alikuwa na uhakika kuhusu mambo ambayo yangempata?

Yesu alijua unabii mwingi katika Maandiko ya Kiebrania uliotabiri jinsi ambavyo maisha yake yangefikia kikomo. (Luka 18:31-33) Fikiria baadhi ya unabii huo pamoja na Maandiko yanayoeleza jinsi ulivyotimizwa.

Masihi . . .

▪ Angesalitiwa kwa vipande 30 vya fedha.—ZEKARIA 11:12; MATHAYO 26:14-16.

▪ Angepigwa na kutemewa mate.—ISAYA 50:6; MATHAYO 26:67; 27:26, 30.

▪ Angetundikwa.—ZABURI 22:16; MARKO 15:24, 25.

▪ Angetukanwa akiwa juu ya mti wa mateso.—ZABURI 22:7, 8; MATHAYO 27:39-43.

▪ Angeuawa bila mfupa wake wowote kuvunjwa.—ZABURI 34:20; YOHANA 19:33, 36.

Yesu hangeweza kupanga jinsi unabii huo wote ungeweza kutimizwa. Hata hivyo, alitimiza unabii huo na mwingine mwingi na hivyo kuthibitisha kuwa alitumwa na Mungu. *

Hata hivyo, kwa nini ilikuwa muhimu kwa Yesu kuteseka na kufa?

Yesu alikufa ili kutoa majibu kwa masuala muhimu Yesu alijua kuhusu masuala muhimu yanayohusu ulimwengu mzima yaliyotokezwa katika bustani ya Edeni. Kwa kushawishiwa na kiumbe wa roho muasi, Adamu na Hawa walichagua kutomtii Mungu. Uasi wao ulifanya kuwe na shaka kuhusu haki ya Mungu ya kutawala, au njia yake ya kutawala. Dhambi yao pia ilitokeza suala la ikiwa mwanadamu yeyote anaweza kuwa mwaminifu kwa Mungu anapojaribiwa.—Mwanzo 3:1-6; Ayubu 2:1-5.

Yesu alitoa jibu kamili kabisa kwa masuala yote mawili—enzi kuu ya Yehova na utimilifu wa wanadamu. Kupitia utii wake mkamilifu “mpaka kifo . . . juu ya mti wa mateso,” Yesu aliitetea enzi kuu ya Mungu. (Wafilipi 2:8) Pia, Yesu alithibitisha kuwa mwanadamu mkamilifu anaweza kudumisha utimilifu kamili kwa Yehova hata akikabili majaribu makali kadiri gani.

Yesu alikufa ili kuwakomboa wanadamu Nabii Isaya alitabiri kuwa kuteseka na kufa kwa Masihi aliyeahidiwa kungeandaa upatanisho kwa ajili ya dhambi za wanadamu. (Isaya 53:5, 10) Yesu alielewa jambo hilo waziwazi, na kwa hiari akatoa “nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Kifo chake cha kidhabihu kiliwawezesha wanadamu wasio wakamilifu wawe na uhusiano mzuri na Yehova na waweze kukombolewa kutoka katika dhambi na kifo. Kifo cha Yesu kinatupa nafasi ya kupata kile ambacho Adamu na Hawa walipoteza—tumaini la kuishi milele katika hali kamilifu duniani. *Ufunuo 21:3, 4.

Unayoweza kufanya Katika mfulululizo huu, tumechunguza yale ambayo Biblia inasema kumhusu Yesu—alitoka wapi, aliishi jinsi gani na kwa nini alikufa. Kujua kweli hizo kumhusu Yesu kunaweza kutusaidia katika njia nyingi zaidi kuliko tu kurekebisha maoni yenye makosa kumhusu. Kutenda kulingana na kweli hizo kunaweza kutuletea baraka nyingi—maisha mazuri sasa na uzima wa milele wakati ujao. Biblia inatueleza mambo tunayopaswa kufanya ili kupata baraka hizo.

▪ Kujifunza mengi kumhusu Yesu Kristo na jukumu lake katika kusudi la Yehova.—YOHANA 17:3.

▪ Kuwa na imani katika Yesu na kuonyesha kupitia maisha yako kuwa unamkubali kuwa Mwokozi wako.—YOHANA 3:36; MATENDO 5:31.

Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza mengi zaidi kumhusu Yesu Kristo, ‘Mwana mzaliwa-pekee’ wa Mungu, ambaye kupitia yeye tunaweza kupata zawadi ya “uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Mara nyingi Yesu alijiita “Mwana wa binadamu.” (Mathayo 8:20) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yesu alikuwa binadamu kamili na pia “mwana wa binadamu” anayerejelewa katika unabii wa Biblia.—Danieli 7:13, 14.

^ fu. 13 Kwa habari zaidi kuhusu unabii uliotimizwa na Yesu, ona nyongeza yenye kichwa “Yesu Kristo—Masihi Aliyeahidiwa” ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 17 Kwa habari zaidi kuhusu thamani ya dhabihu ambayo Yesu alitoa kupitia kifo chake, ona sura ya 5, “Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu,” ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?