Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Uovu na Kuteseka?

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Uovu na Kuteseka?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Uovu na Kuteseka?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Uovu ulianza jinsi gani?

Uovu ulianza duniani wakati Shetani aliposema uwongo wa kwanza. Shetani hakuwa mwovu alipoumbwa. Alikuwa malaika mkamilifu, lakini “hakusimama imara katika kweli.” (Yohana 8:44) Alikuza tamaa ya kutaka kuabudiwa ambayo ni haki ya Mungu pekee. Shetani alimdanganya mwanamke wa kwanza, Hawa, na akamshawishi amtii yeye badala ya Mungu. Adamu alijiunga na Hawa katika kutomtii Mungu. Uamuzi huo wa Adamu ulileta mateso na kifo.—Soma Mwanzo 3:1-6, 17-19.

Shetani alipomshawishi Hawa asimtii Mungu, alianzisha uasi dhidi ya utawala wa Mungu. Wanadamu wengi wamejiunga na Shetani katika kumkataa Mungu kuwa Mtawala. Hivyo, Shetani amekuwa “mtawala wa ulimwengu.”—Soma Yohana 14:30; Ufunuo 12:9.

2. Je, uumbaji wa Mungu ulikuwa na kasoro?

Wanadamu na malaika waliumbwa na Mungu wakiwa na uwezo kamili wa kutii matakwa yake. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Mungu alituumba tukiwa na uhuru wa kuchagua kufanya mema au mabaya. Uhuru huo unatupa nafasi ya kuonyesha upendo wetu kwa Mungu.—Soma Yakobo 1:13-15; 1 Yohana 5:3.

3. Kwa nini Mungu ameruhusu wanadamu waendelee kuteseka?

Kwa muda mrefu Mungu amevumilia uasi dhidi ya enzi kuu yake. Kwa nini? Ili kuthibitisha kwamba jitihada yoyote ya kutawala bila kumtegemea yeye haiwezi kuwanufaisha wanadamu. (Yeremia 10:23) Baada ya miaka 6,000 ya historia ya wanadamu, jambo hilo limethibitika kuwa kweli. Watawala wa kibinadamu wameshindwa kukomesha vita, uhalifu, ukosefu wa haki, na magonjwa.—Soma Mhubiri 7:29; 8:9; Waroma 9:17.

Kinyume cha hilo, wale wanaomkubali Mungu kuwa Mtawala wao wananufaika sana. (Isaya 48:17, 18) Hivi karibuni, Mungu ataziharibu serikali zote za wanadamu. Watu wanaochagua kutawaliwa na Mungu ndio tu watakaokaa duniani.—Isaya 2:3, 4; 11:9; Soma Danieli 2:44.

4. Subira ya Mungu inatoa nafasi gani?

Shetani alidai kwamba wanadamu hawawezi kumtii Yehova kwa ushikamanifu. Subira ya Mungu inatupa nafasi sisi sote kuonyesha ikiwa tunaunga mkono utawala wa Mungu au wa wanadamu. Tunaonyesha utawala tunaounga mkono kupitia jinsi tunavyoishi.—Soma Ayubu 1:8-11; Methali 27:11.

5. Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba tunamchagua Mungu kuwa mtawala?

Tunamchagua Mungu kuwa Mtawala tunapotafuta ibada ya kweli inayotegemea Neno lake, Biblia, na kuishi kulingana nayo. (Yohana 4:23) Pia, tunaepuka kujiingiza katika siasa na vita, kama Yesu alivyofanya.—Soma Yohana 17:14.

Shetani anatumia nguvu zake kuwachochea watu waishi maisha mapotovu na kufanya mambo yanayowaumiza wengine. Tunapokataa mazoea hayo, baadhi ya rafiki zetu na majirani wanaweza kutudhihaki au kutupinga. (1 Petro 4:3, 4) Hivyo, kuna maamuzi tunayopaswa kufanya. Je, tutashirikiana na watu wanaompenda Mungu? Je, tutatii sheria zake zenye hekima na upendo? Ikiwa tutafanya hivyo, tutathibitisha kwamba Shetani alidanganya alipodai kuwa hakuna mtu ambaye angemtii Mungu.—Soma 1 Wakorintho 6:9, 10; 15:33.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 11 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Adamu alifanya uamuzi mbaya

[Picha katika ukurasa wa 17]

Maamuzi yetu yanaonyesha ikiwa tunataka Mungu awe Mtawala wetu