Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndoto Yangu Yaishia Kwenye Kiti cha Magurudumu

Ndoto Yangu Yaishia Kwenye Kiti cha Magurudumu

Ndoto Yangu Yaishia Kwenye Kiti cha Magurudumu

Limesimuliwa na Zoya Dimitrova

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilikuwa nikifurahia kutimia kwa ndoto yangu. Nilifurahia sana kusafiri na kufanya michezo ya kuigiza na kikundi cha wanasarakasi. Kisha, Septemba 4, 1970 (4/9/1970), nikapatwa na aksidenti. Mara nilikuwa juu hewani, kisha kufumba na kufumbua, nikajikuta nimeanguka chini.

NILIZALIWA Desemba 16, 1952 (16/12/1952), na niliishi na wazazi wangu na dada yangu mkubwa jijini Sofia, nchini Bulgaria. Wakati huo, Bulgaria ilikuwa nchi ya Kikomunisti ambayo ingawa iliruhusu dini ziwepo, iliwavunja watu moyo sana wasijiunge na dini. Watu wengi hawakumwamini Mungu, na waliomwamini, wengi wao walifanya hivyo kisiri. Ingawa watu wa familia yangu walidai kuwa Waothodoksi, sikufundishwa mambo ya dini wala sikuzingatia mambo ya Mungu.

Tangu nilipokuwa mdogo, ilikuwa wazi kwamba nilipenda sana michezo ya kila aina, hasa sarakasi. Nilipokuwa na umri wa miaka 13, mwanamume fulani alikuja shuleni kwetu akitafuta msichana ambaye angeweza kuzoezwa mchezo wa sarakasi. Mwalimu wangu wa sarakasi alinipendekeza kwa mwanamume huyo. Nilisisimuka kubebwa ndani ya gari la mkurugenzi lililotengenezewa Marekani, nikipelekwa kwa walimu wa mazoezi ili kuhojiwa na kufanyiwa mazoezi ya kuthibitisha kama ninastahili. Nilifurahi kwamba nilichaguliwa. Huo ulikuwa mwanzo wa mazoezi makali yaliyoendelea kwa zaidi ya miaka miwili. Kisha nilipokuwa na miaka 15, nikamaliza mazoezi yangu na kuanza kutembelea sehemu mbalimbali nikiwa na kikundi cha wanasarakasi. Mwanzoni, nilisafiri kotekote nchini Bulgaria kisha nikatembelea nchi zilizokuwa katika Muungano wa Sovieti. Pia nilitembelea Algeria, Hungaria, na nchi ambayo zamani iliitwa Yugoslavia.

Kwa miaka mitatu nilifurahia sana kuona ndoto yangu ikitimia. Kisha, nilipokuwa nikifanya onyesho fulani mjini Titov Veles, Makedonia, nikapatwa na aksidenti niliyotaja mwanzoni mwa makala hii. Nilikuwa nikifanya onyesho fulani la sarakasi na nilikuwa nimerushwa juu hewani. Mtu niliyekuwa nikifanya naye onyesho hilo alikuwa amening’inia miguu juu, na alinirusha juu hewani, akikusudia kunishika nilipokuwa nikishuka chini. Lakini nikakosa mikono yake, nayo kamba iliyokuwa ikinizuia nisianguke ikakatika, hivyo nikaanguka urefu wa mita 6 chini. Nilipelekwa hospitalini haraka, ambako ilipatikana kwamba nilikuwa nimevunjika mkono, mbavu kadhaa, na uti wa mgongo. Nilishtuka sana na kwa siku kadhaa sikuweza kukumbuka kilichotokea. Nilipopata nafuu kidogo, nilitambua kwamba nimepooza kuanzia kiunoni kwenda chini. Lakini kwa vile nilikuwa bado kijana, nilikuwa na matumaini kwamba nikifanyiwa matibabu au upasuaji, nitaweza kutembea tena na hata kuendelea na mchezo wa sarakasi.

Kwa miaka miwili na nusu iliyofuata, niliendelea kutibiwa katika hospitali kadhaa za kuwashughulikia wagonjwa wa muda mrefu, bado nikiwa na matumaini kwamba nitapona. Mwishowe, ilinibidi kukubali kwamba ndoto yangu ilikuwa imefikia mwisho. Sasa nilihitaji kubadili maisha yangu na kuzoea kutumia kiti cha magurudumu, maisha yaliyokuwa kinyume kabisa na ndoto yangu.

Naanza Maisha Mapya

Baada ya kuishi maisha yenye shughuli nyingi, nilifikiri kwamba singeweza kuzoea maisha hayo mapya. Kwa sababu sikuwa na tumaini lolote, nilishuka moyo sana. Kisha, katika mwaka wa 1977 mwanamume fulani anayeitwa Stoyan akanitembelea nyumbani kwangu. Nilipotambua kwamba alikuwa ndugu ya msichana niliyefanya kazi naye hapo awali, nilimkaribisha mara moja. Tulipokuwa tukizungumza, aliniuliza kama nina matumaini yoyote ya kupona. Kwa sababu ya kukata tamaa na maisha, nilimjibu kwamba sikuwa na matumaini yoyote. Aliponiambia kwamba ni Mungu pekee anayeweza kunisaidia, nilimjibu hivi kwa uchungu: “Basi, ikiwa kuna Mungu, kwa nini niko katika hali hii?”

Baada ya mazungumzo hayo, Stoyan, ambaye alikuwa tu amejifunza na kuwa Shahidi wa Yehova alipokuwa akifanya kazi Marekani kama mwanasarakasi, alinieleza kwa fadhili kuhusu ahadi nzuri za Biblia za wakati ujao. Nilisisimuka kujua kwamba hivi karibuni dunia itakuwa paradiso. Ahadi ya kwamba “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena,” ilinigusa moyo sana. (Ufunuo 21:4) Nilitamani sana kufurahia tena afya yangu nzuri! Nilikubali mara moja kujifunza Biblia kwa ukawaida na hivyo nikaanza maisha mapya. Mwishowe, nilikuwa nimepata msingi wa kuwa na tumaini halisi!

Kila juma nilingoja kwa hamu kujifunza Biblia. Kwanza nilijifunza na Stoyan, kisha na dada aliyeitwa Totka, Shahidi mwenye fadhili sana. Alinisaidia kuielewa Biblia haraka, na nikajitoa kumtumikia Yehova katika maisha yangu yote. Wakati huo, hakukuwa na mtu yeyote jijini Sofia aliyestahili kunibatiza, hivyo nikalazimika kungoja ndugu kutoka Makedonia. Mnamo Septemba 11, 1978, mwaka mmoja hivi baada kuanza kujifunza Biblia, nilibatizwa ndani ya beseni kubwa la kuogea katika nyumba yangu. Nilipobatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nilipata shangwe nyingi na maisha yangu yakawa na kusudi.

Kweli ya Biblia niliyojifunza iliwaka kama moto ndani yangu. Hivyo nilimweleza kila mtu aliyenitembelea kuhusu tumaini langu jipya. Inasikitisha kwamba hakuna mtu aliyechukua mambo hayo kwa uzito, labda walifikiri nilikuwa na tatizo la akili kwa sababu ya aksidenti iliyonipata.

Nafanya Kosa Kubwa

Wakati huo, Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku nchini Bulgaria, na walikuwa wachache sana nchini humo. Sikuweza kuhudhuria mikutano yoyote ya Kikristo, na sikushirikiana na Mashahidi wengine kwa ukawaida. Kwa sababu ya mambo hayo na pia kukosa kutambua hatari ya kushirikiana kwa ukaribu na watu ambao hawaishi kulingana na kanuni za Biblia, nilitenda kosa kubwa.

Dhamiri yangu ilinisumbua sana, na nilihisi maumivu makali moyoni kwa kutengwa na Yehova Mungu. Nikiwa nimevunjika moyo na kuaibika, nilisali kwa Yehova na kumweleza yote yaliyokuwa moyoni mwangu, nikimwomba msamaha. Baadaye, wazee Wakristo wenye upendo walinisaidia kusitawisha tena uhusiano mzuri pamoja na Yehova, na kupata tena shangwe katika kumtumikia. Ninathamini kama nini pendeleo la kumtumikia Yehova nikiwa na dhamiri safi na kushirikiana na watu wake ambao ni safi!

Nina Furaha Ingawa Nimelemaa

Aksidenti niliyopata miaka 40 iliyopita ilikatisha ndoto yangu ya kusafiri na kufanya maonyesho ya sarakasi, na nikalazimika kutumia kiti cha magurudumu. Hata hivyo, sina huzuni wala majuto, kana kwamba sikufaulu maishani. Kweli ya Biblia imenisaidia kutambua kwamba ile ndoto yangu ya kupata furaha na uradhi katika sarakasi, haingekuwa na manufaa kubwa ya kudumu. Nimeshuhudia jinsi ambavyo watu niliofanya kazi nao katika sarakasi wamekata tamaa maishani. Kwa upande mwingine, nimepata kitu chenye thamani sana—uhusiano wa karibu na Muumba wangu, Yehova Mungu. Hilo limeniletea furaha zaidi kuliko ile ambayo ningepata nikiwa mwanasarakasi.

Zaidi ya hayo, nimepata furaha ya kuona watu wengine wakijifunza kweli ya Biblia na kujitoa kumtumikia Yehova, Mungu wetu mwenye upendo, katika maisha yao. Nilipoanza kujifunza Biblia mwaka wa 1977, Mashahidi wa Yehova walikuwa wachache sana nchini Bulgaria. Hata mwaka wa 1991, wakati Mashahidi wa Yehova walipoandikishwa rasmi baada ya kuanguka kwa utawala wa Kikomunisti, kulikuwa na Mashahidi wasiozidi 100 nchini Bulgaria. Nimefurahi kama nini kuona idadi ya wahubiri wa Ufalme ikiendelea kuongezeka na kufikia kilele cha wahubiri 1,800 hivi.

Bado kuna kazi nyingi inayopaswa kufanywa nchini Bulgaria. Wengi wanataka kujifunza Neno la Mungu. Hilo linaweza kuonekana wazi kutokana na idadi kubwa ya watu 3,914 waliohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka wa 2010. Ninasisimka ninapotafakari kuhusu mambo yanayothibitisha kwamba Yehova amebariki mwanzo mdogo nchini Bulgaria. Nimeshuhudia kwa macho yangu mwenyewe “mdogo” akiongezeka na kuwa “taifa lenye nguvu,” kama ilivyotabiriwa katika Isaya 60:22.

Kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kibulgaria ni jambo lingine muhimu sana ambalo limeniletea furaha maishani mwangu. Biblia hiyo ilitolewa Agosti 2009 katika Kusanyiko la Wilaya lenye kichwa, “Endeleeni Kukesha!,” lililofanywa jijini Sofia. Kutolewa kwa Biblia hiyo katika lugha yangu ya mama ni ndoto iliyotimia! Bila shaka, itakuwa kifaa muhimu cha kuwasaidia wengine waijue kweli ya Biblia nchini Bulgaria.

Ingawa ulemavu wangu hunizuia nisitimize mengi katika kazi ya kuhubiri habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu, ninapata furaha nyingi kwa kuwaeleza jirani zangu na mtu mwingine yeyote anayenitembelea kweli za Biblia. Siku moja nilipokuwa barazani nilimkaribisha jirani fulani aliyekuwa akipita karibu na kwangu. Alikubali mwaliko wangu, na baada ya kumweleza mambo machache yenye kutia moyo kutoka katika Biblia, akakubali mara moja kujifunza Biblia. Nilifurahi sana wakati alipobatizwa na kuwa dada yangu wa kiroho. Nimekuwa na pendeleo la kuwasaidia watu wanne ambao wamefanya maendeleo na kujitoa kumtumikia Yehova maishani mwao.

Yaelekea kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida pamoja na ndugu na dada zaidi ya mia moja, ambao ni kama familia kwangu, ndilo jambo linalonitia moyo na kuniletea furaha kubwa zaidi. Ni vigumu kwangu kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa sababu ninaishi katika nchi ambayo hakuna huduma maalumu za usafiri kwa ajili ya walemavu na wazee. Lakini ninathamini sana msaada wenye upendo wa ndugu mmoja kijana. Wakati tunapokuwa na mkutano, ananisaidia kutoka nyumbani kwangu hadi kwenye gari lake, kisha kutoka kwenye gari hadi kwenye Jumba la Ufalme. Baada ya mikutano ananirudisha nyumbani. Ninamshukuru Yehova kama nini kwa pendeleo la kuwa sehemu ya familia ya kiroho yenye upendo.

Ninapokumbuka yaliyopita, ninaona kwamba mambo yamebadilika na kuwa tofauti na ndoto niliyokuwa nayo nikiwa kijana. Kumtumikia Yehova kumeniletea furaha kubwa sana sasa na tumaini zuri la wakati ujao. Ninathamini sana ahadi ya Mungu kwamba katika dunia paradiso, “kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya.” (Isaya 35:6) Ninatazamia kwa hamu na kwa uhakika kabisa siku ambayo nitaruka kutoka kwenye kiti changu cha magurudumu, nikiwa na nguvu na afya kamili.

[Blabu katika ukurasa wa 30]

‘Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida ndilo jambo linalonitia moyo na kuniletea furaha kubwa zaidi’

[Blabu katika ukurasa wa 31]

‘Kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kibulgaria ni jambo muhimu sana maishani mwangu’

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nilianza kufanya maonyesho ya sarakasi nikiwa na miaka 15