Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Abrahamu—Mwanamume Mnyenyekevu

Abrahamu—Mwanamume Mnyenyekevu

Abrahamu​—Mwanamume Mnyenyekevu

Abrahamu anaketi katika hema lake, akifurahia kivuli wakati wa joto kali la mchana. Anapotazama kwenye upeo wa macho, Abrahamu anaona wanaume watatu wanaozuru eneo hilo. * Bila kusita, anakimbia kuwalaki wageni hao, akiwahimiza wapumzike kidogo na kufurahia ukarimu wake. Anawaambia atawapa “kipande cha mkate,” lakini anatayarisha mlo mkubwa wa mikate iliyookwa, siagi, maziwa, na nyama nzuri nyororo. Anapowaandalia wageni wake chakula hicho, Abrahamu anaonyesha ukarimu usio na kifani na pia, kama tutakavyoona, unyenyekevu wa kweli.—Mwanzo 18:1-8.

UNYENYEKEVU NI NINI? Unyenyekevu ni kutokuwa na kiburi au majivuno. Mtu mnyenyekevu anafahamu kwamba kila mtu ni bora kuliko yeye katika njia moja au nyingine. (Wafilipi 2:3) Anasikiliza maoni ya wengine, na yuko tayari kufanya kazi za hali ya chini kwa niaba yao.

ABRAHAMU ALIONYESHAJE UNYENYEKEVU? Abrahamu aliwahudumia wengine kwa furaha. Kama ilivyotajwa mwanzoni, Abrahamu alipowaona wale wageni watatu, alianza kushughulikia mahitaji yao mara moja. Mke wake, Sara, alianza kutayarisha chakula bila kupoteza wakati. Hata hivyo, ona ni nani aliyefanya kazi nyingi zaidi: Abrahamu ndiye aliyekimbia kukutana na wageni hao, ndiye aliyejitolea kuwapa chakula, ndiye aliyekimbia kwenye mifugo na kuchagua mnyama wa kuchinjwa, na ndiye aliyeweka chakula chote mbele ya wageni hao. Badala ya kuwagawia watumishi wake kazi zote, mwanamume huyo mnyenyekevu alifanya chochote kilichohitajiwa. Hakuliona kuwa jambo la kujishusha kuwatumikia wengine.

Abrahamu alisikiliza maoni ya watu waliokuwa chini ya mamlaka yake. Biblia inataja tu mazungumzo machache kati ya Abrahamu na Sara. Hata hivyo, tunasoma mara mbili kwamba Abrahamu alisikiliza maoni ya Sara na kutenda kulingana nayo. (Mwanzo 16:2; 21:8-14) Katika mojawapo ya pindi hizo, mwanzoni ‘Abrahamu hakupendezwa hata kidogo’ na maoni ya Sara. Lakini Yehova alipozungumza naye na kumwambia kwamba maoni ya Sara ni mazuri, Abrahamu alikubali kwa unyenyekevu na kutenda kupatana na maoni hayo.

TUNAJIFUNZA NINI? Ikiwa sisi ni wanyenyekevu moyoni, tutafurahia kuwatumikia wengine. Tutapata shangwe tunapofanya yote tuwezayo ili kufanya maisha yao yawe yenye furaha zaidi.

Tunaweza pia kuonyesha unyenyekevu kupitia jinsi tunavyosikiliza maoni ya wengine. Badala ya kukataa maoni ya wengine kwa sababu sio sisi tulioyatoa, ni jambo la hekima kukubali maoni hayo. (Methali 15:22) Mtazamo huo wa kuwa tayari kukubali maoni ya wengine huwanufaisha hasa wale walio na mamlaka ya kadiri fulani. “Nimetambua kwamba msimamizi mzuri hufanya watu wajihisi huru kutoa maoni yao,” anasema msimamizi mwenye uzoefu aitwaye John. Anaongeza kusema: “Lazima uwe mnyenyekevu ili kutambua kwamba mtu fulani unayemsimamia anaweza kufanya mambo kwa njia nzuri zaidi yako. Na tena, haiwezekani kwamba mtu mmoja tu ndiye anayeweza kutoa maoni yanayofaa, hata kama yeye ndiye msimamizi.”

Tunapomwiga Abrahamu kwa kusikiliza maoni ya wengine na kufanya kazi za hali ya chini kwa niaba yao, tunapata kibali cha Yehova. Hiyo ni kwa sababu “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”—1 Petro 5:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Wageni hao walikuwa malaika waliotumwa na Mungu, ingawa huenda mwanzoni Abrahamu hakujua hilo.—Waebrania 13:2.