Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Swali la 2: Ni Nini Kitakachonipata Nitakapokufa?

Swali la 2: Ni Nini Kitakachonipata Nitakapokufa?

ROMAN alipokuwa mvulana, rafiki yake wa karibu alikufa katika aksidenti ya gari. Alisema hivi: “Kifo cha rafiki yangu kilinishtua sana. Miaka mingi baada ya aksidenti hiyo, nilijiuliza nini hutupata tunapokufa.”

Kwa nini tuulize swali hilo?

Kifo cha binadamu ni jambo lisilo la kawaida. Hata tuwe na umri gani, sote hatupendi kufa. Wengi huogopa jambo linalotukia baada ya kifo.

Watu fulani wanafikiri jibu ni nini?

Wengi wanaamini kwamba mtu anapokufa sehemu fulani ya mtu huyo huendelea kuishi. Wanaamini kwamba watu wazuri watathawabishwa kwa kwenda mbinguni, huku wale waliokuwa wabaya wakiadhibiwa milele kwa sababu ya dhambi zao. Wengine wanafikiri kwamba mtu anapokufa haendi popote na mwishowe anasahaulika kabisa.

Majibu hayo yanamaanisha nini?

Jibu la kwanza linaonyesha kwamba wakati wa kifo mtu hafi kabisa. Jibu la pili linaonyesha kwamba maisha hayana kusudi. Wale wanaofikiri kwamba mtu anapokufa haendi popote, huenda wakawa na mtazamo huu hatari: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.”—1 Wakorintho 15:32.

Biblia inafundisha nini?

Biblia haifundishi kwamba baada ya kufa sehemu fulani ya mtu huendelea kuishi. Mungu alimwongoza Mfalme Sulemani kuandika hivi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Wale ‘wasiojua lolote’ hawajui kinachoendelea. Hawawezi kuhisi wala kutenda. Hivyo, watu waliokufa hawawezi kuwasaidia wala kuwadhuru walio hai.

Kinyume na jinsi watu wengi wanavyoamini, Mungu hakukusudia wanadamu wafe. Alimuumba mwanadamu wa kwanza, Adamu, akiwa na tarajio la kuishi milele duniani. Mungu alitaja kifo alipomwambia Adamu kuhusu adhabu ya kutotii. Alimkataza Adamu asile tunda la mti fulani kisha akamwonya kwamba ikiwa angekula tunda hilo ‘angekufa hakika.’ (Mwanzo 2:17) Ikiwa Adamu na Hawa wangeendelea kuwa watiifu wao pamoja na wazao wao ambao wangekuwa washikamanifu kwa Mungu, wangeishi milele duniani.

Adamu aliamua kupuuza onyo la Mungu. Alifanya dhambi alipokosa kumtii Mungu, hivyo akafa. (Waroma 6:23) Hakuna sehemu ya mwili wa Adamu iliyoendelea kuishi baada ya kufa. Badala yake, Adamu alipokufa hakuwepo. Mungu alimwambia Adamu hivi: “Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:19) Kwa kuwa wanadamu wote ni wazao wa Adamu, tumerithi dhambi na kifo kutoka kwake.—Waroma 5:12.

Ingawa Adamu alifanya uamuzi mbaya, Mungu atatimiza ahadi yake ya kujaza dunia na wazao wa Adamu. (Mwanzo 1:28; Isaya 55:11) Hivi karibuni, Yehova atawafufua watu wengi waliokufa. Akizungumza kuhusu wakati huo mtume Paulo alisema: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.

Roman, aliyetajwa mapema alijifunza Biblia na akatambua mambo inayofundisha kuhusu kifo na kumhusu Yehova Mungu. Mambo aliyojifunza yalimchochea sana. Soma simulizi lake katika ukurasa wa 11 wa gazeti hili.